Wednesday, April 12, 2017

Blogu Yangu Imepanda Chati Ghafla

Tangu wiki mbili zilizopita, blogu yangu hii imepanda chati ghafla. Ninaongelea kigezo cha "pageviews," ambazo ninaziangalia kila nitakapo. Kwa miaka na miaka, "pageviews" za blogu hii kwa siku zilikuwa kama 130, sio zaidi sana na sio pungufu sana.

Lakini, kuanzia wiki mbili hivi zilizopita, "pageviews" zimeongezeka ghafla kwa kiwango kikubwa, na sasa ni yapata 900 au zaidi kila siku. Sielewi ni nini kimesababisha ongezeko hilo. Mkondo wa mada zangu haujabadilika. Kwa kiasi kikubwa ninashughulika na masuala ya elimu na utamaduni.

Nimeona kuwa ongezeko hilo la "pageviews," limetokea hapa Marekani. Kwa nchi zingine, kama vile Tanzania na Kenya, hali haijabadilika. Ni ajabu kiasi kwamba blogu ya ki-Swahili inasomwa zaidi Marekani kuliko Afrika Mashariki.

Mtu unaweza kujiuliza ni watu gani wanaosoma hii blogu ya ki-Swahili kwa wingi namna hii hapa Marekani. Ukweli ni kuwa kuna watu wengi hapa, hasa kutoka Kenya na Tanzania, wanaokifahamu ki-Swahili. Wako pia watu kutoka Burundi, Uganda, Rwanda, na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

Vile vile, kuna wa-Marekani ambao wameishi Afrika Mashariki na wanakifahamu ki-Swahili. Pia kuna wa-Marekani wengi ambao wamejifunza au wanajifunza ki-Swahili katika vyuo vikuu mbali mbali hapa hapa Marekani. Ninahisi kuwa hao nao ni kati ya wasomaji wa blogu hii.

Ninavyowazia suala hili la ukuaji wa idadi ya "pageviews" katika blogu, ninawazia jinsi watu wanavyotumia blogu kwa matangazo, hasa ya biashara. Katika ulimwengu wa leo ambamo tekinolojia za mawasiliano zinaendelea kusambaa na kuimarika, wafanya biashara na wajasiriamali wanatumia fursa za mitandao kama vile blogu kutangaza shughuli zao.

Kwa upande wangu, sijajiingiza katika matumizi haya ya blogu, ukiachilia mbali matangazo ya vitabu vyangu na mihadhara ninayotoa au matamasha ninayoshiriki. Lakini, endapo nitabadili msimamo, bila shaka nitakaribisha matangazo ya waandishi, wachapishaji, na wauzaji wa vitabu, kwa sababu blogu yangu inajitambulisha kwa masuala ya aina hiyo.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...