Wednesday, April 13, 2016

Nawazia Mwongozo wa "The African Child"

Tangu miaka ya sabini na kitu, nilivutiwa na wazo la kuandika miongozo ya kazi maarufu za fasihi ya Afrika. Nilianza kujijengea uzoefu kwa kuandika mwongozo wa tamthilia ya Arthur Miller, A View From the Bridge. Niliandika mwongozo ule, ambao niliutaja katika blogu hii, kwa kuombwa na mwalimu Egino Chale, ambaye alikuwa mratibu katika Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima, Tanzania.

Baadaye, kutokana na mashauriano na ndugu A.S. Muwanga wa Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili, niliandaa mwongozo wa Things Fall Apart na The African Child. Hiyo miongozo miwili ilichapishwa kama kitabu kimoja.

Hatimaye, niliamua kuushughulikia upya mwongozo wa Things Fall Apart, na kuuchapisha peke yake, kama nilivyoelezea katika blogu hii. Wazo langu lilikuwa kwamba hatimaye niushughulikie pia mwongozo wa The African Child na kuuchapisha peke yake.

Lakini badala ya kuushughulikia mwongozo wa The African Child, niliamua kuandika mwongozo wa Song of Lawino. Taarifa za shughuli hiyo nimeandika siku chache zilizopita katika blogu hii. Sasa maadam nimeshachapisha mwongozo huo, nitaelekeza mawazo yangu katika kuandaa mwongozo wa The African Child.

Kitabu hiki ambacho kinasimulia maisha ya Camara Laye ni kati ya vitabu vilivyotuvutia sana tulipokuwa vijana tukisoma sekondari. Ingawa ni tafsiri kutoka ki-Faransa, kitabu hiki kina mvuto wa pekee kwa yale kinachoelezea na pia kwa upande wa namna yanavyoelezwa. Ninategemea kubainisha hayo katika mwongozo wangu ambao siwezi kusema nitaukamilisha lini, kwa sababu, kama ilivyo kawaida yangu, ninaandika vitu mbali mbali wakati wote.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...