Friday, September 30, 2016

M-Kenya Kaniandikia Kuhusu Kitabu Changu

Nimefurahi sana, tangu usiku wa kuamkia leo, kupata maoni ya msomaji wa kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Msomaji huyu ni mama m-Kenya ambaye anaishi hapa Minnesota, Marekani. Aliniandikia katika Facebook ujumbe huu:

I did not tell you how precious your book is. My friend and I were reading it to our kids during a sleep over and it is amazing how your culture is similar to ours. You did well and it was very easy to understand and flow with. You are gifted Mwalimu. God bless you more. Thank you again for the great gift.

Huyu mama tulikutana tarehe 30 Aprili, mwaka huu, kwenye tamasha mjini Rochester. Alikuja kwenye meza yangu, tukasalimiana na kuongea. Alivutiwa na kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, akaulizia namna ya kukipata siku nyingine, kwa kuwa hakuja na hela. Hapo hapo nilimpa nakala ya bure. Alishangaa, akashukuru sana.

Nimefurahi kuwa ameniandikia maoni yake kuhusu kitabu hicho. Ninamfananisha na wa-Tanzania kadhaa ambao, baada ya kuniomba, nimewapa nakala za bure za kitabu hiki. Nilitegemea na ningefurahi iwapo wangeniletea neno kuhusu kitabu, lakini sikuwasikia tena. Nawajibika kusema kuwa sioni kama huu ni uungwana.

Ninapowazia jambo hilo, ninapata hisia kuwa huenda hao watu hawakusoma kitabu hicho. Wazo hilo linanifikia kwa kuzingatia ukweli kwamba utamaduni wa kusoma vitabu hauonekani katika jamii ya wa-Tanzania. Hili ni jambo ambalo limelalamikiwa na linaendelea kulalamikiwa na wadau wa vitabu kama vile waandishi na wachapishaji.

Kwa upande wa wa-Kenya, nimejionea kuwa wanao utamaduni wa kupenda vitabu, kama nilivyowahi kuandika katika blogu hii. Hali hiyo ninaishuhudia sio tu huku nje ya Afrika, bali pia  nchini mwao. Ushahidi moja wa wazi ni kuwa makala kuhusu vitabu si jambo geni katika magazeti ya Kenya. Kwa upade wa Tanznia, sijui ni lini niliwahi kuona gazeti la aina hiyo.

Hainifurahishi kusema mambo hayo kuhusu wa-Tanzania, lakini ninachosema ni ukweli nilivyouona. Ukweli unapaswa kusemwa, hata kama unauma. Hainishangazi kwamba hata katika soko la ajira, iwe ni Afrika Mashariki au kwingineko, wanajiamini kuliko wa-Tanzania.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...