Sunday, October 23, 2016

Siku ya Mashujaa wa Kenya, Rochester, Minnesota

Jana nilikwenda mjini Rochester, Minnesota, kuhudhuria sherehe ya siku ya Mashujaa wa Kenya. Hii ni sikukuu ambayo wa-Kenya huifanya kila mwaka tarehe 20 Oktoba, kuwakumbuka mashujaa wa tangu enzi za kupigania uhuru hadi leo. Sherehe ya jana iliandaliwa na jumuia ya wa-Kenya waishio Rochester.

Nilipata taarifa ya sikukuu hii kutoka kwa Olivia Njogu, m-Kenya aishiye Rochester, na mwanabodi wa Rochester International Association. Anaonekana pichani hapa kushoto, wa pili kutoka kulia. Chama hiki huandaa tamasha la kimataifa kila mwaka, na Olivia tulifahamiana niliposhiriki tamasha hilo mwaka huu, kama nilivyoelezea katika blogu hii. Baada ya tamasha, Olivia alisoma kitabu changu Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, na kisha akaniandikia kunielezea alivyokipenda. Taarifa hiyo niliiandika katika blogu hii.

 .


Hii haikuwa mara yangu ya kwanza kuhudhuria sherehe za wa-Kenya hapa Marekani. Daima nimependezwa kujumuika nao, kama nilivyowahi kuandika katika blogu yangu ya ki-Ingereza. Hali ilikuwa hivyo hivyo jana. Nilivyokuwa ninapaki gari kwenye eneo la sherehe, walikuja wa-Kenya kadhaa kunipokea, ingawa hatukuwa tunafahamiana. Tulitambulishana na hima tukazama katika maongezi ya dhati na michapo.













Hii ilikuwa ni sherehe iliyojumuisha watoto vijana na watu wazima. Pamoja na maongezi yasiyo kikomo, vicheko na chereko, kulikuwa na vyakula tele na muziki. Nilivutiwa kwa namna ya pekee na muziki wa Kenya, nikakumbuka safari zangu za Kenya kuanzia mwaka 1989, za utafiti juu ya tungo za zamani na utamaduni wa wa-Swahili.














Picha hapa kushoto ni ushahidi wa hali ya furaha iliyotawala.






























Wengi waliohudhurua sherehe ya jana sikuwa nimefahamiana nao kabla, ingawa wachache walinikumbuka kwa kuwa waliniona katika tamasha la kimataifa la Rochester la mwaka huu.

Sherehe hii haikuwa ya wa-Kenya pekee. Ingawa sikuweza kuongea na kila mtu, nilipata fursa ya kuongea na watu wawili wa mataifa mengine: mmoja kutoka Nigeria na mwingine kutoka Uganda.




Katika kuishi kwangu hapa Minnesota, nimeweza kufahamiana na wa-Afrika wengi waishio Minneapolis, St. Paul, na maeneo ya jirani. Sasa ninafurahi kuweza kujenga mtandao wa aina hiyo maeneo ya Rochester.

Wanadiaspora wa Afrika tuna wajibu wa kujenga mshikamano miongoni mwetu, kama msingi wa ushirikiano katika bara letu. Waliotutangulia huku ughaibuni, kama akina Peter Abrahams, Jomo Kenyatta, na Kwame Nkrumah walifanya hivyo. Kwangu kama mwandishi na mwalimu, hizi zote ni fursa za kielimu. Darasa ni popote, kama nilivyowahi kuandika katika blogu hii.


No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...