Tuesday, October 4, 2016

Wadau wa Vitabu Vyangu Kwenye Mkutano wa Africa Network

Jana jioni nilirudi kutoka Ohio, katika Chuo cha Denison, ambako nilikwenda kushiriki mkutano wa Africa Network kama nilivyoripoti katika blogu hii. Nina mengi ya kusema kuhusu mkutano ule, na hapa napenda kusema neno juu ya maprofesa wanaoonekana nami pichani hapa kushoto, ambao wote walinigusa kwa namna walivyoongelea vitabu vyangu.

Huyu aliyeko kushoto ni Stephen Volz, profesa wa Chuo cha Kenyon. Tumefahamiana miaka kadhaa katika mikutano ya Africa Network. Aliwahi kuishi Botswana akijitolea chini ya mpango wa Peace Corps. Juzi, nilipowasili kwenye ukumbi wa mkutano, ulikuwa wakati wa chakula cha jioni. Nilienda kukaa kwenye meza ambayo ilikuwa na kiti cha ziada. Mmoja wa watu waliokuwa wameketi hapo ni Profesa Volz.

Baada ya kusalimiana, profesa Volz alianza hima kutuambia kuwa alikuwa anajiandaa kwenda Botswana na wanafunzi wa Associated Colleges of the Midwest (ACM), na kwamba atatumia kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences katika programu hiyo. Nilifurahi kusikia hivyo, ingawa sikushangaa, kwa sababu msukumo mojawapo wa mimi kuandika kitabu hiki ulianzia kwenye mikutano ya bodi ya ACM nilipoombwa kuandika chochote cha kusaidia ufahamu wa tamaduni. Niliwahi kuelezea msukumo huo katika blogu hii.

Kulia hapo pichani ni Profesa Kristofer Olsen wa Chuo Kikuu cha Montana. Huyu naye tumefahamiana kwa miaka kadhaa. Nilimfahamu wakati wa mkutano mojawapo wa Africa Network uliofanyika katika Chuo cha Denison, alipokuwa moja wa watumbuizaji katika kikundi cha ngoma za kiafrika. Baada ya hapo tulikuwa marafiki katika Facebook.

Siku moja aliniandikia ujumbe kuwa alikuwa anafundisha kozi ya "Mythologies," na kati ya vitabu walivyokuwa wanasoma ni kitabu changu cha Matengo Folktales. Aliniulizia kama ningekuwa tayari kuongea na wanafunzi wake kutumia Skype, nami nilikubali, tukapanga siku na tukafanikisha darasa hilo kama nilivyoandika hapa.


Katika mhadhara wake kwenye mkutano wa juzi, kama anavyoonekana hapa kushoto, Profesa Olsen aliongelea kozi yake, akasema kuwa mwanzoni, watu waliposikia anapangia kutunga na kufundisha kozi ya "Mythologies," walidhani alikuwa anamaanisha jadi za Wagriki na Warumi wa kale. Hawakutegemea kuwa alikuwa anataka kufundisha jadi za mataifa mbali mbali hata wa leo. Ndipo akaamua kutumia kitabu cha Matengo Folktales, ambacho alikifahamu tangu alipokuwa mwanafunzi katika Chuo cha St. Olaf.

Profesa Olsen alituelezea kwamba wanafunzi wake walivutiwa kuonana na kuongea nami tulipojumuika kwa Skype. Walivutiwa kuniona mimi mwandishi wa kitabu cha Matengo Folktales walichokuwa wanasoma na pia kunisikia nikiimba nyimbo zilizomo katika hadithi hizo.

Maelezo ya Profesa Olsen yaliwagusa wasikilizaji. Hatimaye, mkutano ulipoisha, wanabodi wenzangu wa Africa Network waliniomba niandae video kutokana na Matengo Folktales ili iwekwe kwenye tovuti ya Africa Network. Nilikubali wazo hilo.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...