Friday, December 2, 2016

Ndugu wa Uganda Anataka Kitabu

Kama ilivyo kawaida katika blogu hii, ninapenda kujiwekea kumbukumbu mbali mbali. Jana niliwatembelea akina mama wawili wa-Kenya waishio Brooklyn Park, Minnesota, ambao walitaka tukutane ili niweze kuwapa ushauri kuhusu fursa za kujiendeleza kielimu ya juu na katika ajira. Wakati tulipokuwa katika maongezi, waliwasiliana na bwana mmoja wa kutoka Uganda, wakamwita kuja kuungana nasi.

Tulizungumza kuhusu masuala mbali mbali, yakiwemo masuali waliyoniuliza juu ya ufundishaji na uandishi wangu. Mmoja wa hao akina mama nilikuwa nimemwahidi kumpa nakala ya kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Huyu jamaa wa Uganda aliniulizia namna ya kukipata kitabu kile, nikamweleza kuwa anaweza kukipata mtandaoni Amazon.com au lulu.com/spotlight/mbele, au kutoka kwangu. Nikamshauri kwamba kwa upnde wa gharama, ni rahisi zaidi kukinunua Amazon.com. Lakini yeye alisisitiza kuwa nimpelekee, akanipa na anwani yake.
,
M-Ganda huyu amenikumbusha wa-Ganda wengine niliokutana nao hapa Minnesota, wakajiptia kitabu changu. Mmoja ni Steven Kaggwa ambaye alikuwa anamiliki mgahawa wa Tam Tam. Baada ya kukisoma kitabu hiki, aliniambia kuwa aliwaelezea wafanya kazi wake. Mmoja wao, Sally, hakuishia tu kujinunulia nakala, bali alinunua nakala nyingine ambayo aliniambia alikuwa anampelekea mkuu wake wa kazi, ambaye ni m-Marekani. Niliguswa na taarifa ya huyu mama, kama nilivyoguswa miaka michache baadaye, wakati mama mmoja kutoka Togo alivyonunua nakala za kitabu hiki kwa ajili ya wakuu wa kazini kwake, kama nilivyoripoti katika blogu hii.

M-Ganda mwingine ninayemkumbuka nilikutana naye katika tamasha la vitabu ambalo nilikuwa ninashiriki. Alikuwa amefika kikazi hapa Minnesota, lakini alikuja kwenye tamasha hilo, na ndipo tulipofahamiana. Bila kusita alinunua kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differenes, akaenda zake. Yeye na hao wengine wameniacha nikitafakari jinsi hao wenzetu walivyo. Ninaona kuwa sio tu wameenda shule, bali wameelimika, kwani uthibitisho wa kuelimika ni kuwa na hamu ya kutafuta elimu hata baada ya kumaliza shule.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...