Suali hili linaweza kuonekana kuwa rahisi, lakini kwangu ni suali tata. Kifupi ni kuwa mimi nafundisha katika idara ya ki-Ingereza ya Chuo cha St. Olaf, hapa Minnesota. Idara hii ilinialika kuja hapa kuanzisha kozi katika somo la "Post-Colonial Literature," na pia kufundisha uandishi wa ki-Ingereza. Nilichukuliwa, mwaka 1991, kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, ambapo nilikuwa nafundisha katika idara ya "Literature."
Hakuna kozi ya ki-Swahili katika chuo hiki cha St. Olaf. Mbali ya ki-Ingereza, lugha zinazofundishwa hapa ni ki-Jerumani, ki-Japani, ki-China, ki-Spaniola, ki-Norway, ki-Latini, na ki-Griki cha kale.

Mtu huwezi kukurupuka tu, ukafundisha ki-Swahili chuoni, au hata katika shule ya msingi. Lazima ujue mambo mengi yanayohusu lugha hiyo na uwe na utaalamu wa kuifundisha, ambao una vipengele vingi kufuatana na kiwango cha wanafunzi. Sikusomea taaluma hiyo, kwa hivyo siwezi kujitupa katika uwanja ambao siufahamu itakiwavyo.
Kwa kawaida, hao watu wanaoniuliza kama nafundisha ki-Swahili hapa Marekani nadhani wanaamini kuwa kwa mtu kama mimi kufundisha ki-Swahili Marekani ni jambo rahisi tu. Hawaonekani kufahamu hayo niliyosema hapa juu, kwamba inahitaji elimu ya pekee ya lugha husika na ufundishaji wake.
Wanashtuka ninapowaeleza kuwa nafundisha ki-Ingereza. Hawategemei kusikia m-Swahili anawafundisha wa-Marekani ki-Ingereza, ambayo ni lugha yao. Kwa upande wangu, kila ninapoulizwa kama nafundisha ki-Swahili hapa Marekani, huwa najichekea moyoni, ingawa sionyeshi kwao kwamba suali lao linanichekesha. Sio vizuri, wala uungwana kumcheka mtu, na kumfanya ajisikie vibaya, kwa suali kama hilo.
No comments:
Post a Comment