Wednesday, May 11, 2011

Nimekutana na Mpiga Debe Wangu

Leo nimekutana na mzee Don Fultz na Mama Eunice Fultz katika mji wa Eagan, Minnesota. Nilienda kule na mfanyakazi mwenzangu wa chuo cha St. Olaf ambaye tunashughulikia programu za kupeleka wanafunzi nchi za nje. Katika picha hizi, Mzee Fultz na Mama Fultz wameketi katikati.

Mzee Fultz ni mchungaji wa kanisa la ki-Luteri, sinodi ya St. Paul. Anaishi hapa Minnesota na Iringa, akiendesha programu za ushirikiano.

Mchungaji Fultz ni mtu wa pekee kwangu. Ni mfuatiliaji makini wa shughuli zangu za kuwaelimisha wa-Marekani na wa-Afrika kuhusu tofauti za tamaduni zao. Ni mpiga debe mkubwa wa kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Tangu wakati kitabu hicho kilipokuwa ni kijimswada tu kisichokamilika, Mchungaji Fultz alikibeba na kukipigia debe hapa Marekani. Hakuwa peke yake katika kufanya hivyo. Nilivyoona hivyo nilishtuka, nikaamua kukifanyia kazi kimswada hiki na kukiboresha.

Kazi hiyo niliifanya kila siku kwa miezi minne, hadi nikakichapisha kitabu mwezi Februari 2005. Mchungaji Fultz alikiandikia makala kwenye kijarida cha kanisa mojawapo hapa Minnesota, mbali na kuendelea kukipigia debe kwenye mikutano mbali mbali na kwa watu binafsi katika maandalizi ya safari za Tanzania. Wa-Marekani wengi wameniambia kuwa walisikia habari za kitabu hiki kutoka kwake. Wengine wamewapelekea nakala wa-Tanzania.

Leo tulikutana kuongelea mambo ya Iringa, kwani ninapangia kuwepo kule kwa wiki mbili mwaka huu na wanafunzi katika programu ya LCCT ambayo ni ya ushirikiano na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Ingawa Iringa niliifahamu vizuri zamani, nimejifunza mengi kutoka kwa Mzee na Mama Fultz kuhusu Iringa ya leo.

9 comments:

Christian Sikapundwa said...

Ni jambo la pekee kabisa unalo lifanya la kumthamini mpiga debe wako.

Kuna baadhi ya watu hajali kama kuna watu wamewasaidia katika mafanikio yao.Wewe Profrsa ni mtu wa watu ndiyo unaenenda kwa mtindo wa maandiko matakatifu.

Mbele said...

Shukrani Mzee Sikapundwa kwa ujumbe wako. Nikizingatia kuwa huyu mzee ni mchungaji, juhudi yake inanifanya nitambue kuwa nina wajibu wa kufanya makubwa zaidi, kwa manufaa ya wanadamu. Naamini Mungu ndivyo atakavyo.

Simon Kitururu said...

Bomba sana yani!

Na inafurahisha kukutana na mtu athaminiye ya mtu kazi !

Mbele said...

Shukrani ndugu Kitururu. Nangojea pia siku ya kukutana nawe, maana nawe ni mpiga debe wangu wa kutupwa :-)

Simon Kitururu said...

@Prof: :-)

Mbele said...

Tena itabidi upewe angalau ka-Heineken kamoja na kamguu ka kuku :-)

Simon Kitururu said...

@Prof: Hiyo si itanifanya ninene kwa lugha kistaili ya wanenao kwa lugha ki kama kimakanisani fulani?


Ila ukweli mie kama ningekuwa tajiri kidoko TU nafikiri uandikayo ningesambaza dunia nzima!
Na mpaka sasa hivi najaribu niwezavyo kusambaza hekima zako kivyangu na nashukuru kama umestukia hilo!


Kwangu wewe ni bonge la SHULE!

Na ujuavyo kurahisisha topiki ngumu zieleweke kirahisi hapo ndipo najua wewe ni mwalimu wa aina gani!

Kwa kuwa naamini dunia ina walimu wengi kwa jina ingawa ukifuatilia unastukia ni walimu jina kwa kuwa hawaweki hata wafundishacho ki mkao watu wawalengaoKUWAFUNDISHA KITU kuelewa wanajaribu kufundisha nini!

Na nashukuru kukustukia mapema na samahani kwa kuwa kama nijifunzayo kwako ungetaka nikulipe nisingeweza Prof. :-(

Unknown said...

Huwa napita sana hapa lakini kimya kimya, leo nimeondosha ukimya kwa kuacha alama.

Uishi milele Prof.

Mbele said...

Ndugu Mcharia, shukrani kwa ujumbe wako wa mwanzo, nami nakutakia kila la heri. Kuhusu ujumbe wako wa pili, nami nimekuwa nikisoma malumbano kuhusu tuzo kwa wanablogu. Nimekuwa msikilizaji, na papo hapo nakumbuka kuwa nimekuwa nikisema kuwa kublogu kwangu naona ni hasa suala binafsi, kama nilivyosema katika makala hii.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...