Tuesday, May 10, 2011

Kitabu Kuhusu Mwanamuziki Salif Keita

Mchana huu nilikuwa kwenye chuo jirani cha Carleton kuhudhuria uzinduzi wa kitabu kuhusu Salif Keita, kilichoandikwa na Profesa Cherif Keita.

Profesa Keita ambaye anafundisha Carleton anatoka kijiji kimoja na Salif Keita, na walikua wakicheza pamoja utotoni. Ni marafiki hadi leo, na Profesa Keita alishamleta Salif Keita kwenye mji wetu huu wa Northfield kutumbuiza.

Profesa Keita ni mtafiti aliyezama sana katika masuala ya utamaduni, fasihi na falsafa ya jadi ya watu wa Mali. Ndiye hasa mtu anayeweza kutueleza kwa undani kuhusu maisha, sanaa na falsafa ya mwanamuziki Salif Keita.

Salif Keita ni miongoni mwa wanamuziki wa ki-Afrika ambao ni maarufu kabisa. Salif Keita ni albino, na maisha yake tangu alipozaliwa yamekuwa na misukosuko ya kusikitisha. Profesa Keita katika maelezo yake leo alidokezea hayo.

Salif pia ni mwanaharakati katika kutetea haki na maslahi ya albino. Ameanzisha na anaendesha taasisi inayoshughulikia suala hilo. Kiasi fulani cha mauzo ya kitabu hiki kitasaidia taasisi hiyo.

Nimenunua kitabu hiki leo na ninangojea kwa hamu kukisoma. Kama ilivyo kawaida ya blogu hii, Insh'Allah nitaandika habari zake baada ya kukisoma.

3 comments:

Goodman Manyanya Phiri said...

Salif Keita Salif Keita!!!



Hamna jina tamu kama hilo katika wanamuziki wa Afrika!

Tunashukuru kitabu!

emu-three said...

Tunasubiri kwa hamu utuwekee maelezo yake

Mbele said...

Mzee Phiri, Profesa Keita, ingawa hajui kiSwahili, nilimweleza kuwa nimeandika hiki kitaarifa kwenye blogu yangu.

Amefurahi kuona jina lako, akaniletea ujumbe huu:

"It is interesting that a South African acquaintance of mine posted a response in Swahili. His name is Goodman Manyanya Phiri. Please ask him if he remembers communicating with Cherif Keita about the Seme family in KZN, namely Vezi Seme."

Kwanza nimefurahi kusikia kuwa anakufahamu. Yeye ni jirani yangu na rafiki yangu tangu mwaka 1991 nilipofika katika mji huu.

Huwa ananieleza habari za mizunguko yake na utafiti wake huko Afrika Kusini, hasa kuhusu mtu maarufu wa zamani aitwaye John Dube. Alitengeneza filamu kuhusu John Dube iitwayo "Obderlin-Inanda," kuhusu John Dube, na nyingine iitwayo "Cemetery Stories" kuhusu m-Misionari mMarekani aliyekuwa katika nchi ya waZulu miaka ile ya zamani, karne ya 19. Ni huyu m-Misionari ndiye aliyemleta John Dube huku Marekani kusoma, katika chuo cha Oberlin. Ohio.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...