Kati ya taswira zilizotolewa kutokana na matukio haya ya Mbeya ni hili bango lisemalo Mbeya Nchi Raisi Sugu. Picha nimeipata kutoka blogu ya Francis Godwin. Bango hili naona lina ujumbe wa kufikirisha. Kwa upande mmoja, mtu anaweza kusema kuiita Mbeya nchi ni makosa na dharau kwa nchi ya Tanzania.
Lakini kwa upande mwingine, inakuwa vigumu kuthibitisha kosa liko wapi. Neno nchi limekuwa likitumika kwa namna nyingi katika maisha yetu. Miaka ya zamani na hadi leo, tunaposema u-Gogoni, au u-Sukumani, tunamaanisha nchi ya wa-Gogo na nchi ya wa-Sukuma. Hakuna ubaya wowote hapa. Katika hali hii, inakuwa vigumu kuwakosoa wenye hili bango lisemalo Mbeya Nchi.
Kuna wakati tulikuwa na nchi ya Tanganyika. Nchi hiyo ilipata Uhuru mwaka 1961 na mwaka 1964 ikatoweka. Pamoja na kuwa nchi ya Tanganyika haipo, mwaka huu kuna shughuli za kukumbuka uhuru wa nchi hiyo ambayo imetoweka.
Leo kuna nchi iitwayo Tanzania. Kesho na keshokutwa, watu wanaweza kuamua kuififisha nchi hiyo pia, kama walivyoififisha Tanganyika. Kwa mfano, wanaweza kuiunganisha hii Tanzania na nchi jirani, wakatunga nchi tofauti kabisa, na Tanzania ikafa kama ilivyokufa Tanganyika. Labda wenzetu wa Mbeya wanakazana kuhakikisha kuwa nchi yao haipotei kienyeji namna hiyo.
No comments:
Post a Comment