Tuesday, March 3, 2015

Utamaduni wa Kuwasomea Watoto Vitabu

Nimeandika mara kwa mara kuhusu suala la elimu, sio tu katika blogu hii, bali pia katika kitabu changu cha CHANGAMOTO: Insha za Jamii, kitabu ambacho nilitegemea kitasomwa na wa-Tanzania wenzangu, lakini mambo yamekuwa kinyume.

Kati ya mambo ambayo nimekuwa nikiyaongelea ni umuhimu wa kuwasomea watoto vitabu, jambo ambalo limejengeka katika utamaduni wa wa-Marekani. Nimekumbuka yote hayo leo baada ya kusoma makala hii hapa
kama uthibitisho na changamoto.

Hili ni kati ya mambo ambayo wa-Tanzania tunapaswa kujifunza. Nimethibitisha mwenyewe kuwa watoto wa Tanzania wanapenda vitabu, bali, kadiri wanavyokua, mapenzi hayo huzimishwa na watu wazima na jamii kwa ujumla.

Kama wahenga walivyosema, mtoto umleavyo ndivyo akuavyo. Baada ya muda, watoto wa ki-Tanzania hufuata utamaduni wa jamii wa kutothamini vitabu, na Taifa linaendelea kuzorota kielimu., wakati wenzetu wa-Marekani wanawalea watoto wao katika kupenda vitabu.

Mwalimu Nyerere alikuwa mstari wa mbele katika kuwahamasisha watu wawe na tabia ya kutafuta elimu. Alikuwa mwandishi na msomaji makini. Alionyesha mfano kwa vitendo. Aliongoza njia.

Leo tuna watu ambao tunawaita viongozi ambao sielewi kwa nini wanaitwa viongozi. Wangekuwa ni viongozi, wangetambua kuwa elimu ni msingi wa maisha na maendeleo. Wangekuwa wanaihamasisha jamii kwa kauli na vitendo katika kutafuta elimu. Lakini, badala yake, hawaonekani kujali kabisa kwamba wanachangia katika kuliangamiza Taifa badala ya kuliongoza, yaani kulipeleka mbele.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...