Monday, March 23, 2015

Mwandishi Grace Ogot Amefariki

Wikiendi hii, habari zimetapakaa kuwa mwandishi Grace Ogot wa Kenya amefariki. Habari hizi zimenishtua na zimenikumbusha mengi kuhusiana na mwandishi huyu.

Nilipokuwa kijana, miaka ya sitini na kitu, ndipo nilianza kusikia habari zake. Nilikuwa nasoma masomo ya sekondari katika seminari ya Likonde. Shule ilikuwa na maktaba nzuri sana, chini ya usimamizi wa Padri Lambert, OSB, ambaye alikuwa mwalimu wetu wa ki-Ingereza na historia.

Nilikuwa msomaji makini wa vitabu, na nilikuwa nafuatilia kwa karibu uandishi katika Afrika Mashariki, Afrika, na sehemu zingine za dunia. Ndipo nilipoanza kuyafahamu maandishi ya Grace Ogot.

Riwaya yake, The Promised Land, ilikuwa na maana sana katika ujana wangu, kwani ilichangia kunifanya niipende zaidi fasihi. Hadithi fupi ya "The Rain Came" ilinigusa kwa namna ya pekee. Miaka ya mwishoni mwa sabini na kitu, wakati nafundisha katika Idara ya "Literature" ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, nakumbuka nilifundisha kitabu cha Gikuyu Folktales cha Grace Gecau. Humo niliona hadithi ambayo ilinikumbusha "The Rain Came," nikapata kuelewa vizuri jinsi Grace Ogot alivyotumia urithi wa hadithi za jadi katika uandishi wake.

Miaka ile nilikuwa navutiwa na waandishi wengine wa Afrika Mashariki, kama vile Okot p'Bitek, Taban lo Liyong, James Ngugi (ambaye baadaye alibadili jina lake na kujiita Ngugi wa Thiong'o), Austin Bukenya, Laban Erapu, Barbara Kimenye, na wengine kadha wa kadha.

Ile ilikuwa ni miaka ya kukumbukwa, kwani ni wakati ule ndio nami nilihamasika kuandika hadithi kwa ki-Ingereza. Nilifurahi kwa namna isiyoelezeka hadithi yangu ya "A Girl in the Bus" ilipochapishwa katika jarida maarifu la Busara, mwaka 1972, nilipokuwa mwanafunzi Mkwawa High School.

Kumbukumbu zote hizi, na nyingine kem kem zimenijia na zinazunguka kichwani mwangu tangu niliposikia kuwa Grace Ogot amefariki. Ametoa mchango uliotukuka katika fasihi. Astarehe kwa amani.

2 comments:

Ndugu Nkwazi N Mhango said...

R.I.P guru Grace Ogot. You did a tremendous job.

mandela pallangyo said...

Duu. Ndio hivi tu, kila nafsia itaonja mauti.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...