
Tarehe 21 Machi, nilifanyiwa mahojiano na Ndugu Petros Haile Beyene, mkurugenzi wa
African Global Roots, katika studio ya
Afric Tempo mjini Minneapolis. Aliomba tufanye mahojiano kuhusu kitabu changu cha
Africans and Americans: Embracing Cultural Differences ambacho alikuwa amekisoma na kukipenda. Niliandika taarifa ya mahojiano hayo
katika blogu hii.
Hapa naleta picha mbili alizopiga Ndugu Malick, mmiliki wa studio, aliyerekodi kipindi kwa ajili ya televisheni. Amenitumia leo hii. Hapa kushoto anaonekana Ndugu Petros Haile akiwa nami, tayari kwa mahojiano, ambayo watakaoyaona katika televisheni watayafurahia. Kama wasemavyo mitaani, kaeni mkao wa kula.

Nimeona niweke picha hizi hapa, nikizingatia kuwa wako ambao wangependa kuona sura yangu ilivyo kwa sasa, baada ya muda mrefu wa kuumwa. Ninaendelea kupona vizuri, ingawa pole pole. Hata safari kama hizi za Minneapolis, umbali wa maili 45, ninaendesha gari mwenyewe. Na majukumu yangu niliyozoea, kama vile kutoa mihadhara na kufundisha, nayamudu bila shida. Namtegemea Mungu daima; alichonipangia ndicho kitakachojiri.
No comments:
Post a Comment