Saturday, March 21, 2015

Leo Nimehojiwa na "African Global Roots"

Nimerejea mchana huu kutoka Minneapolis, kwenye mahojiano na African Global Roots (AGR). Wiki mbili hivi zilizopita, Ndugu Petros Haile, mkurugenzi wa AGR alikuwa ameniomba tufanye mahojiano hayo.

Ndugu Haile nami tumefahamiana kwa miaka kadhaa. Nimewahi kushiriki katika program zake kwa kupeleka vitabu vyangu. Vile vile, alivyovyofahamu kuwa nimepeleka wanafunzi Tanzania kwenye kozi ya Hemingway, aliniomba niandike makala, ambayo aliichapisha.

Kwa mahojiano ya leo, Ndugu Haile alitaka tuongelee kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, ambacho alishakisoma miaka iliyopita. Alitamani, kwa kutumia mawasiliano ya AGR kusambaza ujumbe katika jamii ya wa-Afrika hapa Marekani na ulimwenguni na kwa watu wengine, kuhusu umuhimu wa kuyaelewa masuala ninayoongelea katika kitabu changu.

Kwa kuwa nilijua kuwa Ndugu Haile alitaka kunihoji kuhusu dhughuli zangu za kuelimisha umma, nilichukua pia nakala ya kitabu changu cha Matengo Folktales, ambacho ni ushahidi wa namna ninavyojitahidi kujifunza kutokana na masimulizi ya jadi ya mababu na mabibi zetu wa Afrika, na namna ninavyotumia hazina hii kuuelimisha ulimwengu kuhusu mchango wa wahenga wetu katika dunia.

Mahojiano yalikuwa mazuri. Ndugu Haile alitunga masuali muhimu kutokana na yaliyomo katika kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences na pia aliniuliza masuali kuhusu utafiti wangu ulioniwezesha kuandika kitabu cha Matengo Folktales.

 Mahojiano haya tumefanyia katika kituo cha Afric Tempo, kinachomilikiwa na Ndugu Malick wa Senegal. Leo ilikuwa ni mara yangu ya kwanza kufika mahali hapo, ambapo pana mgahawa, stoo, na studio ya kurekodia programu za televisheni.

Sitaandika zaidi kwa leo. Nangojea hadi mahojiano yatakapopatikana mtandaoni, ndipo niwaeleze walimwengu. Inafurahisha sana kuweza kukutana na kushirikiana na watu kama Malick na Petros, wenye kupenda kujitolea kwa hali na mali ili kujenga maelewano katika jamii. Jambo moja tuliloongelea leo na kukubaliana ni kuwa tunaamini kuwa Mungu ametuweka duniani kwa madhumuni kama hayo.


No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...