Showing posts with label Haji Gora Haji. Show all posts
Showing posts with label Haji Gora Haji. Show all posts

Wednesday, December 9, 2015

Mtunzi Haji Gora Haji

Leo nimeamua kuongelea kifupi utunzi wa Haji Gora Haji wa Zanzibar, mmoja wa waandishi maarufu wa ki-Swahili wa zama zetu hizi. Nafurahi kuwa niliwahi kuonana naye mjini Zanzibar na kuzungumza naye. Panapo majaliwa, nitaandika taarifa ya mazungumzo yetu, ambayo yalihusu maisha yake katika sanaa. Ni muhimu kuutangazia ulimwengu kazi murua inayofanywa na watu wetu wenye vipaji kama Haji Gora Haji.

Nina vitabu vyake vinne: Kimbunga (Dar es Salaam: Dar es Salaam University Press, 1994), Utenzi wa Visa vya Nabii Suleiman Bi Daudi (A.S.) (Zanzibar: Al-Khayria Press Ltd, 1999), Kamusi ya Kitumbatu (Zanzibar: Express Printing Services, 2006), na Siri ya Ging'ingi (Dar es Salaam: Taasisi ya Taaluma za Kiswahili Chuo Kikuu Dar es Salaam, 2009).

Kadiri siku zinavyopita, wasomaji na wahakiki wanajitokeza na kuongelea uandishi wa Haji Gora Haji. Mifano ya kutambuliwa huko ni taarifa ya Amanda Leigh Lichtenstein, ya Ridder Samson, na ya Pascal Bacuez. Nami nimetafsiri mashairi yake mawili nikayachapisha hapa, hapa, na hapa.

Haji Gora Haji, kama walivyo watunzi wengi, wa zamani hadi leo, wamejengeka katika jadi ya fasihi simulizi. Wanaitumia jadi hii katika utunzi wao, iwe ni mashairi kama walivyofanya W.B. Yeats na Derek Walcott, au riwaya, kama walivyofanya Charles Dickens na Chinua Achebe, au tamthilia, kama walivyofanya William Shakespeare, Wole Soyinka na Ebrahim Hussein, au hadithi fupi, kama walivyofanya Lu Hsun na Ama Ata Aidoo.

Ni hivyo hivyo kwa Haji Gora Haji, kama nilivyowahi kutamka. Utumiaji wa mbinu, miundo, na hata dhamira zitokanazo na fasihi simulizi kunachangia uwezo wa tungo kugusa fikra na hisia za hadhira kwa namna ya pekee kutokana na kwamba fasihi simulizi ni urithi wa wanadamu wote. Maudhui yatokanayo na fasihi simulizi ni ya thamani kwa wanadamu wote.

Kuthibitisha zaidi namna Haji Gora Haji alivyojengeka katika fasihi simulizi, sikiliza anavyosimulia hadithi ya Paa na Pweza.


Thursday, October 29, 2015

Shairi la "Kimbunga" (Haji Gora Haji)

Kutafsiri kazi ya fasihi ni kazi ngumu ya kuchemsha bongo. Inahitaji ufahamu wa hali ya juu wa lugha husika, na pia hisia makini za kifasihi. Tofauti na inavyoeleweka katika jamii, kutafsiri ni suala pana kuliko kuwasilisha ujumbe kutoka lugha moja kwenda lugha nyingine, bali ni kutunga upya kazi ya fasihi inayotafsiriwa. Hili suala linajadiliwa sana na wataalam wa lugha, fasihi, na falsafa.

Pamoja na matatizo yote, ninapenda kuchemsha akili yangu kwa kutafsiri kazi za fasihi. Kwa mfano, nimetafsiri hadithi za ki-Matengo, na shairi la Mama Mkatoliki.

Hapa naleta shairi la Haji Gora Haji, mshairi maarufu wa Zanzibar, ambaye niliwahi kukutana naye. Shairi hilo ni "Kimbunga" ambalo limo katika kitabu chake kiitwacho Kimbunga. Jisomee shairi hilo na ujionee nilivyopambana na lugha katika kutafsiri. Ni mapambano, na kuna wakati unajikuta umepigwa butwaa au mwereka.
-----------------------------------------------------------------------------------------------------------------

                               Kimbunga

1.     Kimbunga mji wa Siyu, kilichowahi kufika
       Si kwa yule wala huyu, ilikuwa patashika
       Kimeing'owa mibuyu, minazi kunusurika
       Nyoyo zilifadhaika.

2.     Yalizuka majabali, yakabirukabiruka
       Zikadidimia meli, ngarawa zikaokoka
       Kimbunga hicho kikali, mavumbi hayakuruka
       Nyoyo zilifadhaika.

3.     Nyumba kubwa za ghorofa, siku hiyo zimeruka
       Zikenenda kwa masafa, kufikia kwa kufika
       Vibanda vyao malofa, vyote vikasalimika
       Nyoyo zikafadhaika.

4.     Chura kakausha mto, maji yakamalizika
       Pwani kulikuwa moto, mawimbi yaliyowaka
       Usufi nusu kipeto, rikwama limevunjika
       Nyoyo zikafadhaika.

5.     Kuna kikongwe ajuza, viumbe kimewateka
       Hicho kinamiujiza, kila rangi hugeuka
       Wataokiendekeza, hilaki zitawafika
       Nyoyo zikafadhaika.


                                 A Hurricane

1.     A hurricane once arrived in Siyu town
       Sparing neither that one nor this one, it was sheer mayhem
       It uprooted babobab trees, the coconut trees surviving
       Hearts went panicking.

2.     Big rocks turned up, tumbling over and over
       Ships were sinking, while mere boats survived
       Fearsome as the hurricane was, it raised no dust
       Hearts went panicking

3.     Great storied houses were blown away that day
       They flew quite a distance, landing wherever they landed
       The huts of the lowly, all survived intact
       And hearts went panicking

4.     The frog drained the river, the water all dried up
       On the shore was conflagration, of the waves flaming
       Half a container of kapok, broke the coolie's cart
       And hearts went panicking

5.     A wizened hag there was, who held beings captive
       She is given to magical powers, changing hues at will
       Those who let her be, perdition will be their lot
       And hearts will go panicking.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...