Friday, February 17, 2012

Wadau Wangu wa Canada

Mara moja moja, katika blogu zangu, nimekuwa nikiandika kuhusu wadau wangu kama mwandishi wa vitabu. Kwa mfano, nimewahi kuandika kuhusu wadau wa Arusha, na Nebraska. Leo napenda kuwakumbuka wadau wangu wa Canada.

Hapa kushoto ni picha iliyopigwa Dar es Salaam mwaka 2004, wakati wa maonesho ya vitabu kwenye viwanja vya kumbukumbu za Taifa. Niko na dada yangu na wadau wa Canada, waliokuwa wanaishi Tanzania. Wakati ule nilikuwa nimechapisha vitabu viwili tu: Matengo Folktales na Notes on Achebe's Things Fall Apart.

Hao akina mama walipita kwenye meza yangu, wakaviangalia vitabu, halafu wakasema watapita tena baadaye kununua kitabu cha Matengo Folktales. Baada ya kusema hivyo, waliendelea na mizunguko yao katika vibanda vingine. Kwa kawaida, watu wakipita namna hii, huwa si rahisi kukumbuka kurudi tena. Lakini hao, baada ya muda mrefu, walirudi, wakanunua kitabu na tukapiga hiyo picha.

Hapa kushoto ni Jeff Msangi, mmiliki na mwendeshaji wa blogu maarufu ya Bongocelebrity. Alihusika katika kuinukia kwangu kwenye ulimwengu wa kublogu, kama nilivyoelezea hapa. Yeye ni mdau na mpiga debe mkubwa wa kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, kama inavyodhihirika hapa, na hapa. Sijawahi kuonana naye, ila namwona mtu wa karibu kwangu, kutokana na mawasiliano yetu.





Mdau mwingine ni Rene Kakou. Huyu ni bosi wa kampuni ya Groupe Macrobell, Inc. Anatoka Ivory Coast, lakini anaifahamu Tanzania vizuri, na anaipenda kama vile nchi yake. Tulionana mara moja tu, katika ndege kutoka Tanzania kwenda Ulaya, tukafahamiana na kubadilishana anwani na namba za simu.

Hatimaye alikisoma kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences." Ana michapo mikali kuhusu jinsi mambo yalivyokuwa wakati anakisoma kitabu hicho. Mara kwa mara ananikumbuka, kwa simu au katika ukumbi wa Facebook.

Ndoto ya mwandishi ni kuona maandishi yake yanasomwa. Nami nawashukuru wadau hao, na wengine wote ambao siwajui.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...