Thursday, October 25, 2018

Nimepeleka Vitabu kwa wa-Matengo

Mwezi Julai mwaka huu nilikwenda Tanzania, nikiwa nimechukua vitabu vingi. Baadhi ni vile nilivyoandika mwenyewe, ambavyo niliviwasilisha katika maduka ya Kimahama, na A Novel Idea. Nilichukua pia nakala 16 za Matengo Folktales kwa ajili ya kuzipeleka kwa wa-Matengo, wilayani Mbinga, katika mkoa wa Ruvuma.

Ninasema hivyo, na kutaja kabila langu, nikijua kwamba kwetu wa-Tanzania, hii ni kauli tata, isiyopendeza, kwani inaashiria upendeleo au ubaguzi kwa msingi wa kabila. Utamaduni wa Tanzania, uliojengwa na chama cha TANU, hauafiki ubaguzi wa makabila au wa aina nyingine. Sasa kwa nini nimetoa kauli hiyo? Kwa nini niliamua kupeleka nakala hizi za Matengo Folktales kwa wa-Matengo? Napenda kuthibitisha kwamba nilifanya jambo muafaka.

Matengo Folktales ni mkusanyo wa hadithi za jadi ambazo nilizirekodi nyumbani u-Matengo miaka ya sabini na kitu. Nilizirekodi katika kaseti, kisha nikachagua hadithi kumi na kuzitafsiri kwa ki-Ingereza. Niliandika uchambuzi wa kila hadithi na nikaongezea insha ya kitaaluma kuhusu hadithi. Huu ukawa ni mswada ambao ulichapishwa kama Matengo Folktales.

Mimi ni mwanataaluma katika taaluma hii inayojulikana kama "Folklore." Kama ilivyo katika taaluma zingine, tuna taratibu na maadili ya utafiti, uandishi na uchapisahji. Kati ya hayo ni utaratibu wa kuwarudushia fadhila watu wanaowezesha utafiti wetu. Watafiti tusiwe tunachukua yale tunayopewa bila kuwarejeshea kwa namna moja au nyingine wale wanaotupa hayo tunayotafuta. Dhana hiyo huitwa "reciprocity" kwa ki-Ingereza.

Kuna nämna mbali mbali za kurudisha fadhila, kufuatana na mila na desturi za mahali husika na kufuatana na ridhaa ya mtu binafsi anayetuwezesha. Kuna namna mbali mbali za kutoa shukrani. Kwa upande wangu, na kwa watafiti wengi, namna bora kabisa ya kurudisha fadhila ni kuwapa nakala ya yale ninayorekodi na kuondoka nayo, kama vile kaseti au picha ninazopiga.

Kwa msingi huo, baada ya kuchapisha Matengo Folktales, nilijua kwamba nina wajibu wa kupeleka nakala kwa wa-Matengo. Kwa kuwa nimechapisha kitabu kwa ki-Ingereza, ilibidi nisubiri hadi ipatikane sehemu muafaka ya kupeleka.

Fursa imepatikana kwa kuwepo kwa shule za sekondari. Hizi nakala 16 nilimkabidhi mwalimu Frank Kinunda mjini Mbinga, baada ya mawasiliano naye, naye amezisambaza kwenye hizo shule. Zitawaelimisha vijana na walimu kuhusu utamaduni wa wahenga, na pia kuhusu taaluma ya "Folklore." Vile vile, kwa kuwa  nimeandika kwa uangalifu mkubwa kama mwalimu wa lugha ya ki-Ingereza, Matengo Folktales ni kitabu cha kujiongezea ujuzi wa ki-Ingereza. Kitabu hiki kinatumika kufundishia katika vyuo hapa Marekani, na ninafurahi kimeanza kuwa mikononi mwa wanafunzi na walimu Tanzania

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...