Wednesday, October 10, 2018

Naambiwa Niongeze Bei ya Kitabu

Katika matamasha ya vitabu ninayoshiriki, ninakutana na mambo mengi, zikiwemo tabia na mitazamo ya wateja. Moja ambalo linanigusa zaidi ni pale mteja anaposhauri niongeze bei ya kitabu changu. Hiyo imetokea mara kadhaa, kuhusiana na vitabu vyangu viwili: Africans and Americans: Embracing Cultual Differences na Matengo Folktales.

Vitabu hivi ninaviuza kwenye matamasha kwa dola 14 kila kimoja. Kwa kujua kwamba watu wengine wanatoa  noti ya dola 20 au noti mbili za dola kumi kumi, ninajitahidi kuwa na chenji. Ajabu ni kwamba watu wengine hawasubiri chenji, na wengine wanakataa. Wanachotaka ni kitabu waende zao. Ninakumbuka watu waliowahi kutoa noti ya dola 20 bila kutaka chenji. Mmoja wa hao, nilipojiandaa kumpa chenji, alisema hiyo chenji ni shukrani yake kwangu kwa kuandika kitabu.

Tarehe 4 mwezi huu nilikutana na jambo jingine kabisa. Mama moja, Jackie, ambaye nimemfahamu miezi michache iliyopita na akasoma hivi vitabu vyangu viwili, alinialika kwenye mhadhara wa rafiki yake Maria kuhusu vitabu na maisha yake. Alikuwa ameniambi nije na nakala za vitabu vyangu, ili aweze kuvipeleka katika tamasha la vitabu. Baada ya mhadhara, wakati tulipokuwa tunajumuika kwa viburudisho na maongezi, Jackie akanulizia bei ya vitabu vyangu, nami nikamwambia kuwa ni dola 14. Alisema nipandishe iwe 15, kwa ulinganisho na kitabu cha dola 10 na pia kwa urahisi wa chenji.

Alinitambulisha kwa rafiki yake, akamwambia kuhusu hivi vitabu vyangu. Alivyokuwa akielezea hayo, akaniambia nivitoe kwenye begi, nikampa. Huyu rafiki alichagua Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, akapanda ngazi kwenda kuchukua hela akaja akanipa na kitabu akachukua. Dakika chache baadaye, mama huyu alinitambulisha kwa mama mwingine, na akamwambia kuhusu vitabu. Naye akanunua Matengo Folktales.

Kwa hivyo nimejikuta nikiafiki wazo la kuongeza bei ya vitabu vyangu. Hata hivyo, bei hiyo ni ndogo kulingana na bei za mahali pengine za vitabu hivyo. Ninaamini kuwa taarifa hii ina ujumbe kuhusu watu wanaothamini vitabu kuliko fedha. Kama nilivyowahi kusema tena na tena, blogu hii ni sehemu ambapo ninajiwekea mambo yangu binafsi, kama vile kumbukumbu, hisia, na mitazamo. Ikitokea haja, siku zijazo, ya kuandika kitabu kuhusu maisha na kazi zangu, blogu hii itakuwa chanzo muhimu cha taarifa.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...