Saturday, November 10, 2018

Nimeongea na Lumen Christi Book Club

Miezi kadhaa iliyopita, nilipata mwaliko wa kwenda Lumen Christi Catholic Community kuongelea kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Aliyenialika ni Jackie ambaye alikuwa amekisoma kitabu hicho. Alisema kwamba jumuia ya waumini hao wana klabu yao ya usomaji vitabu, na kwa sasa wamejikita katika vitabu vinavyohusu Afrika.

Nilipoingia ukumbini, niliona meza imepangwa vizuri karibu na mlandoni, yenye vitabu vyangu na vya waandishi wawili ambao tunafahamiana: Maria Nhambu ambaye alizaliwa Tanzania, na Afeworki Ghorghis, jaji mstaafu wa mahakama kuu ya Eritrea.

Baada ya Jackie kunitambulisha, nilielezea kifupi nilivyokulia Tanzania, katika utamaduni wa wa-Matengo, na hatimaye nilivyokutana na utamaduni wa Marekani, nilipokuwa masomoni katika Chuo Kikuu cha Wisconsin-Madison, na kufikia kuwa mshauri kwa vyuo vinavyopeleka wanafunzi Afrika, kama nilivyoandika katika utangulizi wa kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Katika kuelezea uandishi wangu juu ya masuala ya utamaduni, nilianza na kitabu cha Matengo Folktales.

Baada ya hapo, Jackie alitaja vipengele vilivyomo kitabuni ili nielezee, na wengine waliniuliza masuali yao. Kati ya masuala tuliyoongelea ni "gifts" (sio kwa maana ya zawadi), uzee, na "African time." Nilielezea nilivyoandika kitabuni kuhusu masuala hayo. Klabu hii ya vitabu ni ya aina yake, kwa maana kwamba watu wanahudhuria hata bila kusoma kitabu kinachojadiliwa.

Mkutano ulikuwa mzuri na wenye manufaa. Binafsi, nilitoa shukrani kwa fursa ya kufahamiana na watu wapya, kwani inatajirisha maisha yangu. Nilifurahi kuweza kuwaelezea shughuli zangu kama mtoa ushauri chini ya mwavuli wa Africonexion.  Baada ya mimi kurejea nyumbani, Jackie aliniletea ujumbe kwamba atanitambulisha kwa mkurugenzi wa East Side Freedom Liabrary ambaye wakati huu anaandaa programu kuhusu Afrika. Sikuwa ninajua kuhusu maktaba hiyo. Ninasubiri.

1 comment:

Mbele said...

Jina "Lumen Christi" ni ki-Latini, maana yake "Mwanga wa Kristu." Nilisoma ki-Latini nilipokuwa seminari ya Hanga na Likonde, mkoani Ruvuma, Tanzania, kwa hiyo ninajua.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...