
Hapa kushoto ni picha niliyopiga tarehe 16 Novemba katika duka la vitabu la Barnes and Nobel mjini Burnsville. Inaonyesha kabati la vitabu vilivyopendekezwa na wahudumu wa duka. Nilipiga picha hiyo kwa sababu kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, kipo hapo. Kimekuwepo kwa wiki nyingi. Bila shaka kuna wateja wanaoingi na kuchungulia kwenye kabati hilo ili kupata wazo juu ya kitabu cha kununua, kwani tayari kimependekezwa na watu wazoefu wa vitabu.
Utamaduni wa kuvihesabu vitabu kama zawadi muafaka kwa sikukuu au mazingira yeyote mengine unanivutia, kama nilivyowahi kueleza katika blogu hii. Ninatamani utamaduni huu uote mizizi katika nchi yangu. Nawazia furaha watakayokuwa nayo watoto kwa kupewa vitabu kama zawadi, kwa sababu ninajua kuwa watoto wanapenda vitabu, kama nilivyowahi kuandika katika blogu hii. Nawazia namna ambavyo mitazamo na fikra za watu zingeboreka kwa kuwa na utamaduni wa kuthamini na kusoma vitabu vya aina mbali mbali.
No comments:
Post a Comment