Showing posts with label man eaters. Show all posts
Showing posts with label man eaters. Show all posts

Saturday, December 8, 2012

Simba wa Tsavo

Leo napenda kuongelea habari ya simba wa Tsavo. Ni habari iliyokuwa inatusisimua sana tulipokuwa shuleni, baina ya darasa la tano na la nane. Kulikuwa na kitabu, Simba wa Tsavo, ambacho kilichapishwa mwaka 1966. Ni tafsiri ya kitabu cha J.H. Patterson kilichoitwa The Man Eaters of Tsavo.

Kitabu hiki kilielezea matukio ya kutisha wakati ujenzi wa daraja la reli kwenye mto Tsavo, nchini Kenya, miaka mia na kitu iliyopita. Kilielezea namna simba walivyokuwa wakiwavizia, kuwadaka na kuwaua wafanya kazi kwenye eneo la hili daraja wakawaua watu zaidi ya mia, hadi, hatimaye, Patterson alipofanikiwa kuwaua, mwezi Desemba 1898. Hiyo ndio habari tuliyosoma tukiwa shuleni, miaka hiyo ya sitini na kitu.

Lakini, kwa miaka hii ya karibuni, yapata miaka kumi, nimekutana na taarifa nyingine nyingi kuhusu simba wa Tsavo. Je, unajua wale simba waliishia wapi? Katika kusoma habari za mwandishi Ernest Hemingway, ambaye alizaliwa mwaka 1899 eneo la jirani na Chicago, nimegundua kuwa alipokuwa mtoto alipelekwa na baba yake katika hifadhi ya Field Museum of Natural History mjini Chicago. Hapo alipata kuziona maiti za wanyama mbali mbali kutoka Afrika ambazo zilikuwa zimehifadhiwa kitaalam ili zionekane kama vile ni wanyama hai.

Kati ya wanyama hao ni wale simba wa Tsavo, ambao picha yao inaonekana hapa juu. Habari hii ilinishtua sana, kwani sikujua kabisa kuwa simba wa Tsavo wamehifadhiwa na kwamba wako Chicago. Hiyo ni faida ya wazi ya kusoma vitabu, kwamba mtu unagundua mambo ambayo hukuyajua. Pamoja na kuangalia wanyama hao waliohifadhiwa, mtoto Hemingway alisoma kitabu cha The Man Eaters of Tsavo. Hayo yote yalichangia katika kumjengea Hemingway mapenzi makubwa aliyokuwa nayo juu ya Afrika kwa maisha yake yote.

Mwaka 1933, Hemingway na mke wake Pauline walifunga safari wakitokea Ulaya, wakaja Afrika Mashariki. Walishuka meli Mombasa, wakapanda treni kuelekea Nairobi. Walipita Tsavo, wakaenda hadi Machakos, kisha Tanganyika. Kuhusu safari yake ya Tanganyika, Hemingway aliandika kitabu maarufu kiitwacho Green Hills of Africa, ambacho ni kimoja ya vitabu vyake ambavyo nimevisoma na kuwafundisha wanafunzi.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...