Monday, September 10, 2012

Ziara Chuo Kikuu cha Kanisa Katoliki, Songea

Kama nilivyoelezea tena na tena, napenda kutembelea vyuo ninapokuwa Tanzania. Soma kwa mfano, hapa. Ni fursa ya kujiweka sawa katika ufahamu wa nini kinachoendelea, changamoto zilizopo, mikakati ya kuboresha elimu ya juu. Napata fursa ya kujadiliana na wahusika namna ya kushirikiana na kuchangia vyuo hivi. Tarehe 21 mwezi Julai, mwaka huu, nilitembelea tawi la Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustin, mjini Songea. Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustin ni mradi wa Kanisa Katoliki Tanzania. Ni mtandao ambao tayari una vituo sehemu mbali mbali za nchi. Kwa taarifa zaidi, soma hapa.

Hapa kushoto naonekana na Profesa Donatus Komba, makamu wa mkuu wa chuo hicho mjini Songea. Yeye ndiye alikuwa mwenyeji wangu siku ya ziara yangu, akinitembeza kila mahali na kunipa maelezo.








Hapa kushoto naonekana nikitia sahihi katika kitabu cha wageni.


Hapa kushoto ni jengo la utawala. Chuo cha Mtakatifu Augustin kina mipango mikubwa ya kupanua mtandao wake. Kwa upande wa Songea, tayari Seminari Kuu ya Peramiho imeshafanywa sehemu ya Chuo Kikuu, kwa masomo ya falsafa. Wanaofahamu taratibu za seminari za Katoliki wanajua kuwa tangu zamani, mapadri walitakiwa kusoma masomo ya kawaida tunayosoma sisi wengine, na baada ya hapo kwenda seminari kuu kusomea masomo ya teolojia na falsafa.  Basi Peramiho sasa ni sehemu ya Chuo Kikuu, kwa masomo haya ya falsafa.

Kanisa Katoliki jimbo la Songea limetoa majengo yaliyowezesha chuo hiki kuanzishwa. Chuo kina mipango ya kuongeza majengo. Nilionyeshwa sehemu mbali mbali, kama vile madarasa, kumbi kubwa, na maktaba. Nilivutiwa kusikia kuwa, mapadri wastaafu wamekuwa wakichangia hazina ya vitabu vyao katika juhudi za kuitajirisha maktaba.


Tayari, chuo kikuu cha Songea kinaendesha masomo ya aina mbali mbali. Mimi kama mwalimu wa "Literature" nilifurahi kusikia kuwa hilo ni somo mojawapo katika chuo hiki, na nilifurahi kukutana na mhadhiri wa somo hili.



Kwamba hiki ni chuo cha Kanisa Katoliki haimaanishi kuwa wanaosoma, kufundisha, au kufanya kazi hapo, ni wa-Katoliki tu. Chuo hiki kinawapokea watu wa dini na madhehebu mbali mbali. Angalia, kwa mfano, orodha ya wanafunzi wapya kwa mwaka huu.

Nilijifunza mengi katika ziara yangu hii, na hapa juu nimetoa dondoo chache tu.







Mdau jipatie taarifa zaidi kwa kuangalia video hii inayoelezea ufunguzi wa chuo hiki:

 

4 comments:

Yasinta Ngonyani said...

Ni furaha ya pekee kusikia hili kuwa Songea yetu imepata chuo. maana ni kweli wengi walikuwa wakishindwa kwenda kupata elimu ya juu kwa ajili ya familia hasa akina mama.

Thobias nyoni said...

Hakika ni jambo la kumshukuru Mungu kwa mkoa wa Ruvuma kupata chuo kikuu.
Iwe ni fursa kwa wazawa wa mkoa huo kukitumia chuo hicho kujitaalumisha kwa manufaa ya mkoa wetu na Taifa kwa ujumla.

Mbele said...

Dada Yasinta na Ndugu Nyoni, tuko pamoja katika mtazamo huo.

Mimi nilifundishwa na kanisa katoliki kama ifuatavyo: shule ya msingi Litembo (1959-62), Seminari ya Hanga (1963-1966), na Seminari ya Likonde (1967-70), kabla ya kwenda Mkwawa High School na Chuo Kikuu Dar es Salaam.

Leo mimi ni profesa. Lakini msingi wa mafanikio yangu niliwekewa na kanisa Katoliki, katika masuala ya uwajibikaji na maadili kazini, ikiwemo kumtendea kila mwanafunzi kwa msingi wa haki, sio vinginevyo.

Kwa msingi huo, utaona kuwa nina wajibu wa pekee kutafakari namna ya kuchangia hicho chuo kikuu. Katika ziara yangu hapa chuoni, nilionana na mhadhiri wa somo la "Literature," ambalo ni somo mojawapo ninalofundisha muda wote. Itakuwa ni utovu wa nidhamu na utovu wa shukrani nisipowajibika kwenye hiki chuo.

Thobias Nyoni said...

Shikamoo profesa.
mimi nakushukuru sana kwa kutambua mchango wa kanisa katoliki hasa katika elimu.Maana ingawa bado ni kijana mdogo lakini mpaka sasa nami sina budi kuliambioa kanisa katoliki asante sana.
Profesa, mchango wako katika chuo hiki ni muhimu na wathamani sana katika maendeleo ya watanzania hasa ya wale wa mikoa ya kusini maana wao ndio waliosahaulika kwa miaka mingi kitaaluma. Mimi ni kijana mdogo tu lakini nikijaliwa makusudio yangu yana mawanda mapana sana kitaaluma ingawa sasa nachukua shahada yangu ya kwanza katika moja ya chuo cha kanisa hilo.Miezi michache mwaka huu nataraji kuhitimu. HIVYO NIMEFURAISHWA SANA NA UTAMBUZI WAKO JUU YA MCHANMGO WA KANISA KATOLIKI HASA KITAALUMA.Maana bila hilo sijui prefesa leo hii ungekua wapi.
Mimi nakushukuru sana pia nakutakia kazi njema.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...