Showing posts with label mijadala. Show all posts
Showing posts with label mijadala. Show all posts

Saturday, June 24, 2017

Eti Tundu Lissu Anapinga Kila Kitu

Kuna wa-Tanzania wanaomlalamikia au kumshambulia Tundu Lissu eti anapinga kila kitu. Napenda kusema kuwa malalamiko na mashambulio haya ni ujinga.

Kutoa mawazo na kujieleza ni haki ya kila binadamu, ambayo imetambuliwa katika tangazo la kimataifa la haki za binadamu na imetambuliwa katika katiba ya Tanzania. Tundu Lissu anatumia haki yake. Haingilii wala kuzuia haki ya mtu yeyote kutoa mawazo. Watu wajibu hoja zake. Watu wenye akili hufanya hivyo.

Kama Tundu Lissu hakubaliani na yale wanayosema wengine, na anahoji au kupinga muda wote, tatizo liko wapi? Masuala yenyewe yanahusu maslahi ya Taifa. Kila mzalendo anawajibika kutoa mchango kadiri ya uwezo wake. Mawazo ni mchango mmoja wapo. Na hiki ndicho Tundu Lissu anachofanya. Akae kimya kwa nini? Hata mimi sikai kimya ninapoona maslahi ya nchi hayafuatiliwi ipasavyo au yanahujumiwa. Kutoa mawazo ni muhimu, na kukosoana, inapobidi.

Ni ujinga kutotambua kuwa anavyofanya Tundu Lissu anatoa changamoto ya kuwafanya watu wafikiri nje ya upeo waliozoea au nje ya upeo wanaouwazia wao. Elimu haisongi mbele kama hakuna watu wachochezi wa fikra kama Tundu Lissu. Watu wanaohoji fikra zinazokubalika na jamii wanaipa jamii fursa ya kufungua milango mipya ya fikra. Siafiki uwekaji wa mipaka katika kufikiri na kutafuta ukweli. Elimu haiwekewi mipaka.

Mimi kama mwalimu ninawajibika kuwalea vijana wawe watu wa kuhoji mambo bila ukomo. Vinginevyo, kuna sababu gani ya kujiita mwalimu? Kuna sababu gani ya kuwa na vyuo na kusema kuwa tunaelimisha? Watu makini ulimwenguni kote wanatambua kuwa dunia inazidi kuwa ya "knowledge economy." Bila tabia ya udadisi usiokuwa na mipaka, tutajengaje "knowledge economy"? Kwa maana hiyo, ninamwona Tundu Lissu kama mtu muhimu kwa maendeleo ya nchi, na ni mfano wa kuigwa.

Thursday, January 20, 2011

Tamko Kuhusu Matamko ya Wa-Tanzania

Tanzania sasa imekuwa nchi ya matamko. Kila kukicha linatolewa tamko kutoka kikundi au jumuia fulani. Katika siku za karibuni, kwa mfano, tumeshasikia matamko kutoka vyama vya siasa, jumuia za kidini, na taasisi mbali mbali, za serikali na zisizo za serikali.

Matamko ya wa-Tanzania yanahusu zaidi masuala tata ya jamii, au migogoro. Yanahusu mambo kama sera za serikali au vitendo vya watendaji mbali mbali, kama vile polisi, au taasisi zingine. Mara kwa mara, matamko yanakuwa na hisia za kulalamika, kuonya, au kutangaza msimamo.

Kila mtu anaweza kuwa na mtazamo wake kuhusu jambo hilo. Binafsi, naliona ni jambo zuri, kwa maana kwamba watu wanatumia uhuru wao wa kuelezea hisia, mawazo na mitazamo yao. Kwa hivi, sishangai kuyasikia matamko hayo. Kila mtu ana haki ya kutoa tamko lake, ili mradi havunji sheria au kuingilia uhuru wa wengine wa kutoa matamko.

Utamaduni wa matamko ni mzuri. Ni bora kuliko tunayoyaona au kuyasikia yakitokea katika jamii za wenzetu, ambao migogoro yao inawapeleka katika kupigana na kuvunjika kwa amani.

Kwa watu wasiopendezwa na jambo, au wenye hasira, fursa ya kujieleza kwa namna yoyote, kama hii ya matamko, ni njia nzuri ya kupooza hisia za kusumbua. Ni aina ya tiba kisaikolojia, hata kama wanayosema katika haya matamko ni upuuzi. Kuzuia uhuru na fursa ya kujieleza ni jambo lenye athari mbaya.

Kwa upande mwingine, utamaduni wa wa-Tanzania wa matamko unanichekesha, kwa jinsi matamko yanavyofumuka kama uyoga au kumiminika kama mvua.

Tungeweza kuendeleza utamaduni wa kufanya mazungumzo ya ana kwa ana au kuwatumia wawakilishi wetu. Tungeweza hata kufuata utamaduni wa zamani wa mabibi na mababu, kama alivyouelezea Mwalimu Nyerere, kwamba wahenga walikuwa wanakaa chini ya mti na kujadili masuala hadi kukubaliana. Lakini nafurahi nami nimetoa tamko langu.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...