Leo hapa Chuoni St. Olaf tulitembelewa na mgeni maarufu, Keith Ellison, ambaye ni mwakilishi kutoka Minnesota katika Congress, ambalo ni bunge la Marekani. Keith Ellison ni mu-Islam wa kwanza kuwa mjumbe katika Congress.Aliongelea changamoto zinazoikabili Marekani na dunia katika mkabala wa kuwepo kwa tofauti za dini.
Kwa kutumia mifano ya Marekani, alisisitiza kuwa watu wa dini mbali mbali tuna uchaguzi wa kufanya. Tunaweza kuchagua kuheshimiana, kuelewana na kujenga dunia ya amani, upendo na mshikamano, au tunaweza kuchagua kuwa na uhasama, ubaguzi, chuki, mfarakano, na migogoro.
Alisema kuwa wahubiri wa dini wana wadhifa mzito. Wanapopanda kwenye mimbari au sehemu nyingine ya kuhubiria, wana ushawishi mkubwa mioyoni mwa waumini. Wana wajibu wa kujua hilo, kwani wanao uwezo wa kujenga umoja na maelewano katika jamii au wanaweza kujenga uhasama na chuki katika jamii.
Alisisitiza wajibu wetu wa kuwaheshimu watu wa dini mbali mbali, na watu wasio na dini. Wote wanastahili heshima, na wala hakuna mwenye haki ya kumshinikiza mwenzake kwenye masuala ya imani za dini.
Hotuba yake iliwagusa sana watu. Kitu kimoja kilichonivutia zaidi ni hoja yake kuwa mtu ukifanya juhudi ya kuifahamu dini kwa kusoma na kutafakari, utagundua kuwa inakupeleka kwenye mtazamo wa maelewano, upendo, kuwaheshimu wanadamu wengine, wawe wana dini au hawana dini.
Aliyoongelea yanatugusa sote. Nilitamani angekuja Tanzania kutoa mawaidha hayo. Hotuba yake HII HAPA.
