Showing posts with label migogoro ya jamii. Show all posts
Showing posts with label migogoro ya jamii. Show all posts

Tuesday, April 19, 2011

Mawaidha ya Mwakilishi Keith Ellison

Leo hapa Chuoni St. Olaf tulitembelewa na mgeni maarufu, Keith Ellison, ambaye ni mwakilishi kutoka Minnesota katika Congress, ambalo ni bunge la Marekani. Keith Ellison ni mu-Islam wa kwanza kuwa mjumbe katika Congress.

Aliongelea changamoto zinazoikabili Marekani na dunia katika mkabala wa kuwepo kwa tofauti za dini.

Kwa kutumia mifano ya Marekani, alisisitiza kuwa watu wa dini mbali mbali tuna uchaguzi wa kufanya. Tunaweza kuchagua kuheshimiana, kuelewana na kujenga dunia ya amani, upendo na mshikamano, au tunaweza kuchagua kuwa na uhasama, ubaguzi, chuki, mfarakano, na migogoro.

Alisema kuwa wahubiri wa dini wana wadhifa mzito. Wanapopanda kwenye mimbari au sehemu nyingine ya kuhubiria, wana ushawishi mkubwa mioyoni mwa waumini. Wana wajibu wa kujua hilo, kwani wanao uwezo wa kujenga umoja na maelewano katika jamii au wanaweza kujenga uhasama na chuki katika jamii.

Alisisitiza wajibu wetu wa kuwaheshimu watu wa dini mbali mbali, na watu wasio na dini. Wote wanastahili heshima, na wala hakuna mwenye haki ya kumshinikiza mwenzake kwenye masuala ya imani za dini.

Hotuba yake iliwagusa sana watu. Kitu kimoja kilichonivutia zaidi ni hoja yake kuwa mtu ukifanya juhudi ya kuifahamu dini kwa kusoma na kutafakari, utagundua kuwa inakupeleka kwenye mtazamo wa maelewano, upendo, kuwaheshimu wanadamu wengine, wawe wana dini au hawana dini.

Aliyoongelea yanatugusa sote. Nilitamani angekuja Tanzania kutoa mawaidha hayo. Hotuba yake HII HAPA.

Saturday, January 22, 2011

Kwa wa-Tanzania, Dini Imekuwa Bangi

Katika hali ya kawaida, dini ni kitu cha manufaa kwa wanadamu, kwa maana kwamba inatufundisha kumtambua na kumcha Mungu, na kwa wale wanaoamini miungu wengi, ni hivyo hivyo. Dini inatufundisha maadili ya kumtendea binadamu mwingine kama tunavyopenda kutendewa. Kwa ufafanuzi zaidi maadili hayo ni kama kupendana, kusikilizana, kuheshimiana, kusameheana, na kutakiana mema.

Kwangu mimi m-Katoliki, maadili hayo yalielezwa kwa uwazi na Yesu katika mafundisho yake mengi, hasa pale aliposema kuwa amri kubwa kuliko zote ni kumpenda Mungu kwa moyo wetu wote, nguvu yetu yote na akili yetu yote, na kumpenda jirani kama tunavyojipenda wenyewe na pia kuwapenda adui zetu. Kwa lugha rahisi ni kuwa tunapowachokoza wengine au kuumiza hisia zao kwa makusudi, au tunapokosa uvumilivu na badala yake tunatunisha misuli na kujibu mapigo, tunaasi dini na kuwa makafiri.

Kwa kuzingatia hayo, niliandika makala kuwa penye dini hapana magomvi, na kwamba kuwepo kwa magomvi ni ushahidi wa kukosekana kwa dini. Dhana ya mgogoro wa kidini haina mantiki; ni sawa na kusema "usiku wa mchana," dhana ambayo haina mantiki. Soma hapa na hapa.

Hata kitu kizuri kinaweza kutumiwa vibaya. Na ndivyo ilivyo Tanzania, kwenye suala la dini. Dini imegeuzwa kuwa bangi. Dhana ya dini kuwa bangi ilielezwa na Karl Marx katika Critique of Hegel's Philosophy of Right, lakini naitafsiri kwa namna yangu.

Kadiri siku zinavyoenda, bangi hii inazidi kuenea katika Tanzania na kukolea vichwani. Imekuwa kichocheo cha malumbano, magomvi, uhasama, ubaguzi, majungu na chuki.

Sehemu za ibada zimegeuzwa kuwa majukwaa ya kueneza sumu hizo, kwa kutumia vipaaza sauti. Papo hapo, wahusika wanaamini kuwa ni wafuasi na watetezi wa dini. Wanaendelea kujenga nyumba wanazoziita za ibada, kumbe wanazitumia kuendeleza ukafiri. Hawakumbuki busara za wahenga kuwa kucha Mungu si kilemba cheupe.

Kilichonisukuma kuandika hayo niliyoandika ni wasi wasi wangu kuhusu hali ya nchi yangu. Dini yangu hainiruhusu kuwahukumu wengine. Kama nimekiuka angalizo hili, mwenye kujua ni Mungu.

Thursday, January 20, 2011

Tamko Kuhusu Matamko ya Wa-Tanzania

Tanzania sasa imekuwa nchi ya matamko. Kila kukicha linatolewa tamko kutoka kikundi au jumuia fulani. Katika siku za karibuni, kwa mfano, tumeshasikia matamko kutoka vyama vya siasa, jumuia za kidini, na taasisi mbali mbali, za serikali na zisizo za serikali.

Matamko ya wa-Tanzania yanahusu zaidi masuala tata ya jamii, au migogoro. Yanahusu mambo kama sera za serikali au vitendo vya watendaji mbali mbali, kama vile polisi, au taasisi zingine. Mara kwa mara, matamko yanakuwa na hisia za kulalamika, kuonya, au kutangaza msimamo.

Kila mtu anaweza kuwa na mtazamo wake kuhusu jambo hilo. Binafsi, naliona ni jambo zuri, kwa maana kwamba watu wanatumia uhuru wao wa kuelezea hisia, mawazo na mitazamo yao. Kwa hivi, sishangai kuyasikia matamko hayo. Kila mtu ana haki ya kutoa tamko lake, ili mradi havunji sheria au kuingilia uhuru wa wengine wa kutoa matamko.

Utamaduni wa matamko ni mzuri. Ni bora kuliko tunayoyaona au kuyasikia yakitokea katika jamii za wenzetu, ambao migogoro yao inawapeleka katika kupigana na kuvunjika kwa amani.

Kwa watu wasiopendezwa na jambo, au wenye hasira, fursa ya kujieleza kwa namna yoyote, kama hii ya matamko, ni njia nzuri ya kupooza hisia za kusumbua. Ni aina ya tiba kisaikolojia, hata kama wanayosema katika haya matamko ni upuuzi. Kuzuia uhuru na fursa ya kujieleza ni jambo lenye athari mbaya.

Kwa upande mwingine, utamaduni wa wa-Tanzania wa matamko unanichekesha, kwa jinsi matamko yanavyofumuka kama uyoga au kumiminika kama mvua.

Tungeweza kuendeleza utamaduni wa kufanya mazungumzo ya ana kwa ana au kuwatumia wawakilishi wetu. Tungeweza hata kufuata utamaduni wa zamani wa mabibi na mababu, kama alivyouelezea Mwalimu Nyerere, kwamba wahenga walikuwa wanakaa chini ya mti na kujadili masuala hadi kukubaliana. Lakini nafurahi nami nimetoa tamko langu.

Sunday, December 19, 2010

Kitabu Kimetua St. Cloud, Minnesota

Wasomaji wa blogu zangu, hii na ile ya ki-Ingereza, wanafahamu ninavyopenda kujishughulisha na masuala ya tofauti za tamaduni na athari zake katika ulimwengu wa leo.

Nafanya shughuli hizi si kwa ajili ya kutafuta umaarufu, bali naamini ni wajibu kwa wanadamu kusaidiana katika maisha na kuifanya dunia iwe bora kuliko ilivyo.

Miezi ya karibuni nimejishughulisha sana na matatizo yanayowapata wahamiaji wa ki-Somali katika jimbo la Minnesota, ambalo linaongoza kwa idadi ya wahamiaji wa ki-Somali. Wasomaji wa blogu zangu watakumbuka taarifa za shughuli zangu katika mji wa Faribault.

Matatizo kama haya ya Faribault yako pia katika miji mingine, kama vile St. Cloud. Kutokana uzoefu nilioupata Faribault, nimeanzisha mawasiliano na ndugu Mohamoud Mohamed, mkurugenzi wa SASSO, jumuia inayoshughulikia masuala ya wa-Somali mjini St. Cloud.

Nilimpelekea nakala ya kitabu cha Africans and Americans, kama mchango wangu na changamoto. Jana ameniambia kuwa kitabu amekipata, anaendelea kukisoma, na anakipenda. Atawaonyesha wadau wa St. Cloud: halmashauri ya mji, shule na vyuo, idara ya polisi, mahospitali, na kadhalika. Nami nilimhakikishia kuwa ni jambo bora. Badala ya watu kununiana tu au kugombana, ni vema wakaanza utaratibu wa kuzungumzia matatizo kama ilivyofanyika Faribault, na ikapokelewa vizuri.

Kama ninavyosema katika mihadhara, blogu na maandishi mengine, matatizo ya aina hii yanayoikumba miji ya Faribault na St. Cloud yanajitokeza katika miji na jamii nyingine duniani: Afrika, Asia, Australia, Marekani, Ulaya, na kwingineko, na yataongezeka, kutokana na mwenendo wa utandawazi wa leo. Ninapokuwa Dar es Salaam, kwa mfano, nasikiliza na kutafakari minong'ono na majungu kuhusu wa-China, ambao wanaendelea kuja katika mji ule. Niliwahi pia kuongelea tafrani iliyotokea Zanzibar. Kinachobaki ni sisi kujizatiti kwa kuelimishana kuhusu tofauti zetu na kutafuta namna ya kuishi bila matatizo.

Najiandaa kushiriki katika masuala ya St. Cloud. Mbali ya umuhimu wake kwa jinsi hali ilivyo, ni fursa ya mimi kujiongezea ujuzi na uzoefu nitakaoutumia katika kuwasaidia wengine.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...