Thursday, February 26, 2015

Leo Nimefundisha Darasa Kwa Kutumia "Skype"

Asubuhi ya leo, nimefundisha darasa kwa kutumia "Skype." Ni darasa la Mwalimu Kristofer Olsen la somo la "Mythologies," katika Chuo Kikuu cha Montana, Marekani. Chuo hiki kiko mjini Bozeman, maili 995 kutoka hapa nilipo, Northfield, Minnesota. Niliandika kuhusu mpango wa kufundisha darasa hili katika blogu hii.

Katika mawasiliano ya barua pepe na Mwalimu Olsen, aliniuliza iwapo ningeweza kuongea na darasa lake la "Mythologies," ambalo lilikuwa linasoma kitabu changu cha Matengo Folktales. Aliniletea silabasi ya somo, inayoonyesha kuwa tarehe 24 na 26 wangejadili Matengo Folktales.

Jana jioni, binti yangu Zawadi alinielekeza tena namna ya kutumia "Skype," na alinisajili. Leo asubuhi, kipindi kilianza kama ilivypoangwa, saa nne na nusu za hapa Minnesota, ambayo ni saa tatu na nusu kule Montana. Nilikuwa mbele ya kompyuta, na wanafunzi na profesa wao walikuwa wananiona na kunisikia, nami nilikuwa nawaona na kuwasikia.

Tulifanya mengi. Niliombwa kusimulia hadithi mojawapo, ambayo ingechukua muda mfupi, nami nikasimulia hadithi ya "Hawk and Crow," iliyomo kitabuni. Niliwaambia wanafunzi kuwa kokote niendako kuongelea hadithi za jadi, huzisimulia papo kwa papo, badala ya kuzisoma. Katika kusimulia hadithi ya "Hawk and Crow," niliwaeleza machache kuhusu namna hadithi inavyosimuliwa, tofauti na inavyoonekana kimaandishi.

Masuali yao yalikuwa ya maana sana. Suali moja lilihusu jinsi nilivyorekodi hadithi na kuandaa kitabu cha Matengo Folktales. Suali jingine lilihusu mchakato wa kutafsiri. Jingine lilihusu vifo na mauaji katika hadithi hizo. Jingine lilihusu mhusika mjanja ("trickster") katika hadithi, kama vile Anansi na Sungura.

Niliwaeleza mambo kadhaa kuhusu mhusika huyu, katika tamaduni mbali mbali. Mhusika huyu hujitokeza kama mnyama (kama vile Anansi au Gizo, Kobe na Sungura), na katika tamaduni zingine hujitokeza katika umbo la binadamu, kama vile Nasreddin Hodja na Abu Nuwas. Niliongelea asili na maana ya mhusika huyu katika jamii, kwa kutumia nadharia za kisaikolojia za Carl Jung.

Niliguswa kwa namna ya pekee nilipoulizwa nifafanue dhana iliyomo katika blogu yangu kwamba ninaliona darasa kuwa ndio mahali pekee penye uhuru kamili wa kufikiri na kujieleza. Kumbe kuna watu wanaosoma blogu yangu kwa makini kiasi hiki.

Mawasiliano kama haya ya kutumia "Skype" ni maendeleo ya tekinolojia, ambayo yanatuwezesha kufanya mambo ambayo hatukuweza kuyafanya kabla. Jambo moja la kujifunza ni kuwa tunaweza kuendesha darasa bila kukutana katika chumba kimoja. Mimi kama mwalimu, ninaweza kuwafundisha wa-Tanzania ingawa niko nje ya Tanzania. Tuachane na mawazo kwamba sherti nirudi Tanzania ili kujenga nchi.

Wakati tekinolojia inasonga mbele na kutufungulia milango mipya, inashangza kuona jinsi wa-Tanzania kwa ujumla wanavyoendelea kuwa na mawazo yaliyopitwa na wakati. Kila ninapowasikia wakidai kuwa wataalam walioko nje warudi nyumbani wakajenge Taifa, nawazia suala hilo. Najiuliza ni lini wataamka usingizini na kutambua kuwa maendeleo ya tekinolojia ya mawasiliano yanazidi kuififisha mipaka ya kijiografia tuliyoizoea. Tunaingia kwenye dunia isiyo na mipaka, dunia ambamo mtu popote alipo anaweza akatoa mchango wake kwa walimwengu popote.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...