Sunday, February 8, 2015

Mwenyeji Wetu Longido, Tanzania

Picha hii ilipigwa Januari, 2013, nilipokuwa Longido, Tanzania. Niko na Ndugu Ally Ahamadou, mkurugenzi wa programu ya utalii wa utamaduni hapa Longido. Yeye ndiye alikuwa mwenyeji wa misafara yangu katika kozi kuhusu safari na maandishi ya Ernest Hemingway.

Programu ya utalii wa utamaduni Longido ni moja kati ya programu maarufu za aina hii nchini Tanzania. Taarifa kuhusu program hii zinapakana kirahisi mtandaoni.

Binafsi nimeshuhudia jambo hili kwa jinsi makala niliyochapisha katika blogu yangu ya ki-Ingereza kuhusu utalii wa utamaduni Longido inavyotembelewa na wasomaji wengi. Hali hii imenithibitishia kuwa blogu inaweza kuwa nyenzo yenye uwezo mkubwa wa kutangaza utalii.

Ingawa Ndugu Ally Ahmadou si mzaliwa wa Longido, bali Tanga, niliona anakubalika sana na watu wa Longido. Hata kwa kuongea naye muda mfupi tu, unapata picha kuwa huyu ni mpenzi Longido na shughuli za utalii wa utamaduni. Programu hii ya utalii wa utamaduni Longido niliona inapendwa na watu wa Longido, kwa kuwa faida zake katika jamii yao wanaziona.

Ndugu Ally Ahmadou nilimwona kuwa mtu mwepesi wa kuangalia fursa mpya katika shughuli ya utalii. Mfano ni jinsi tulivyoongelea suala la vitabu katika utalii, suala ambalo nimeliongelea katika kitabu changu cha CHANGAMOTO: Insha za Jamii na nililigusia pia katika blogu hii. Ndugu Ally alipofahamu kuwa nimechapisha vitabu vinavyoweza kuchangia katika sekta hiyo, alichukua nakala za kutosha za Matengo Folktales na Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, kwa ajili ya watalii ambao wangependa kuvinunua.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...