Tuesday, February 3, 2015

Wa-Marekani na wa-Tanzania: Tofauti za Tamaduni

Leo, katika ukurasa wake wa "Facebook," Ndugu Maggid Mjengwa aliandika: "Leo Nimepokea Wafanyakazi Wa Kujitolea Kutoka Marekani..."

Wa-Marekani hao, ambao anaonekana nao katika picha hapa kushoto, wamefika Iringa kujitolea katika Kwanza Jamii, kampuni inayoendesha gazeti na redio. Maggid hakutuambia watakaa muda gani hapo Iringa, lakini nilijibu ujumbe wake "Facebook" namna hii:

"Safi sana. Ninapoona au kusikia mambo ya aina hii, wazo linalonijia akilini ni kuwa muhimu wageni wapate mtu wa kuwaelezea angalau yale ya msingi kuhusu tofauti kati ya utamaduni wa-Marekani na ule wa wa-Bongo, na wa-Bongo pia waelezwe kuhusu tofauti kati ya utamaduni wao na ule wa wa-Marekani. Hii ni kwa ajili ya kurahisisha shughuli na maisha kwa pande zote mbili. Kila la heri."

Suala hili nililoongelea ni muhimu hasa katika dunia ya utandawazi wa leo. Hao wageni wanapokuja kwetu na sisi tunapoenda kwenye nchi zao, ni mihumu kulizingatia, ili kufanikisha shughuli na mahusiano baina yetu. Nimeandika kuhusu tofauti baina ya utamaduni wa wa-Marekani na wa-Afrika katika kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, ambacho nashukuru kwa jinsi kinavyowasaidia watu wanaokisoma, kama ilivyoelezwa hapa na hapa.

Hilo ni suala ninalolishughulikia sana katika utafiti, mihadhara na warsha. Hiyo picha hapa juu tayari inanipa vidokezo muhimu. Ninaona jinsi hao wasichana walivyomwangalia Maggid usoni, na yeye ameangalia chini. Hapo Mjengwa anaonyesha heshima kwao, kwa mujibu wa utamaduni wetu wa ki-Tanzania na ki-Afrika kwa ujumla.

Nao hao wasichana, kwa mujibu wa utamaduni wa Marekani, wanaonysha heshima kwa kumwangalia Maggid usoni. Huenda wanashangaa kwa nini hawaangalii usoni. Hilo suala la kuangaliana usoni ni moja ya yale ninayoyaongelea katika kitabu changu:

Kama hii picha ingekuwa ni video, ingenipa fursa ya kusema mengi zaidi.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...