Showing posts with label maonesho ya vitabu. Show all posts
Showing posts with label maonesho ya vitabu. Show all posts

Friday, April 29, 2016

Ninajiandaa Kushiriki Tamasha Rochester

Jioni hii, ninajiandaa kwenda Rochester, Minnesota, kushiriki tamasha la kimataifa kesho. Nitaondoka asubuhi sana ili nikawahi kabla ya saa nne litakapoanza tamasha. Nimeshalipia meza. Nitapeleka vitabu vyangu kama kawaida.

Meza ya vitabu katika tamasha ni kivutio kwa watu, sawa na meza za bidhaa na vitu vingine mbali mbali vinavyokuwepo. Watu wanapenda kuangalia vitabu, kuuliza masuali juu ya vitabu hivi, na wengine kuvinunua. Mimi mwenyewe ninapenda kuongelea mambo yanayonisukuma kuandika, hasa fasihi, tamaduni, na changamoto zitokanazo na tofauti za tamaduni.

Nitabeba pia bendera ya Tanzania. Nilishawahi kuelezea katika blogu hii namna nilivyofikia uamuzi wa kununua bendera hii, kwa ajili ya matamasha na maonesho mbali mbali. Huku ughaibuni, bendera ya Taifa ina mguso wa pekee moyoni. Kwa vile tamasha la kesho ni la kimataifa, bendera hii itakuwa mahali inapohitajika.

Tamasha la kimataifa hufanyika kila mwaka mjini Rochester. Mji huu una wakaazi kutoka sehemu mbali mbali za dunia. Kufanyika kwa tamasha la kimataifa katika mji huu ni jambo lenye mantiki bora. Watu wanaonesha tamaduni za nchi zao, na wote wanajifunza kutoka kwa wenzao.

Mwaka jana nilihudhuria tamasha la Rochester kwa mara ya kwanza, na niliandika habari zake hapa, na hapa. Ninangojea kwa hamu kukutana tena kesho na baadhi ya watu niliokutana na kufahamiana mwaka jana.

Kwangu mimi mwalimu, matamasha ya aina hii ni kama darasa. Kila ninapohudhuria, ninajikuta nikifundisha na pia kujifunza siku nzima. Nategemea kuandika taarifa za tamasha la kesho hapa katika blogu yangu.

Wednesday, December 3, 2014

Wazo la Kutafsiri Kitabu

Kwa wiki kadhaa, nimekuwa nikiwazia kutafsiri kitabu cha CHANGAMOTO: Insha za Jamii. Siku chache zilizopita, niliandika kuhusu kitabu hiki katika blogu hii.

Nawazia kuzirekebisha insha zilizomo, na kuchapisha kitabu cha ki-Ingereza. Kufanya hivyo kutakipa kitabu hadhira kubwa zaidi kuliko ile ya wajuao ki-Swahili. Nina hakika, kwa mfano, kuwa wa-Marekani watakitafuta na kukisoma. Kwa ujumla wasomaji wa vitabu vyangu ni wa-Marekani.

Ninaposhiriki matamasha hapa Marekani, watu kadha wa kadha huja kwenye meza yangu na kuangalia vitabu, kuvinunua, au tu kuongea nami. Wako wanaoniuliza kama nimechapisha kitabu kingine, kwani vile vilivyopo mezani, vya ki-Ingereza, wanavyo au wamevisoma. Kauli hizi hata binti zangu, ambao hushirikiana nami, wamezisikia tena na tena.

Kwa miaka kadhaa, sijachapisha kitabu kipya. Sababu kubwa ni kuwa kuandika kitabu huchukua muda. Yaweza kuwa miezi au miaka. Kwa mfano, ilichukua miaka 23 hivi kuandaa kitabu cha Matengo Folktales. Vile vile, muda mwingi natumia katika kufanya utafiti na kuandika makala. Kutafsiri kitabu cha CHANGAMOTO, ni njia moja ya wazi ya kupatikana hicho kitabu kingine.

Kutafsiri CHANGAMOTO sio jambo la haraka. Kuna kitabu kingine katika lugha ya ki-Ingereza ambacho nataka kumaliza kukiandika kabla ya kuanza kutafsiri CHANGAMOTO. Hata hivi, siwezi kusema kuwa ni lazima ningoje. Muda wote ninakuwa na kazi kadhaa ninazoandika, na huwa sio rahisi kujua ni ipi itamalizika kabla ya ipi. Wanadamu tumejaliwa uwezo wa kufanya shughuli nyingi kwa pamoja, "multitasking" kwa ki-Ingereza. Ninachoombea ni uzima na akili timamu.

Monday, August 4, 2014

Furaha ya Kusainiwa Kitabu

Wapenzi wa vitabu wakishajipatia nakala ya kitabu cha mwandishi fulani, huguswa pale mwandishi anaposaini kitabu hicho. Aghalabu mwandishi huandika ujumbe mfupi kwa mteja huyu na kasha kuweka sahihi. Ni jambo linalowagusa sana wasomaji. Mimi mwenyewe, kama mwandishi, nimeshasaini vitabu vyangu vingi. Ninazo baadhi ya picha za matukio haya kutoka miaka iliyopita.

Msomaji makini na mwanablogu Christian Bwaya hivi karibuni ameelezea vizuri katika blogu yake, hisia zake baada ya kujipatia kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differencesambacho nilikuwa nimekisaini:

Namshukuru kwa dhati mwandishi wa kitabu hiki, Prof. Mbele kwa kunitumia kitabu hiki bila malipo, tena kwa gharama zake. Si jambo linalowatokea wengi. Ni furaha iliyoje hatimaye nimekipokea leo asubuhi. Naanza kukisoma kitabu hiki kwa mara nyingine, safari hii kikiwa na saini ya mwandishi. Ni upendeleo na muujiza wa pekee kunitokea katika siku za hivi karibuni. Ni lazima nimshukuru kwa dhati. Asante sana Profesa.

Utamaduni wa kusaini na kusainiwa vitabu nimeuzoea. Hata juzi tarehe 2 Agosti, niliposhiriki tamasha la Afrifest kule Brooklyn Park, Minnesota, nikiwa na vitabu vyangu, wadau kadhaa walionunua vitabu vyangu waliomba kusainiwa.

Hapa kushoto anaonekana mdau akiniangalia wakati nasaini nakala ya Matengo Folktales, ambayo alikuwa amenunua hapo.
Baada ya kusainiwa nakala yake, aliona furaha ya ziada kupiga picha nami huku akiwa ameshika kitabu hicho. Hiyo nayo ni kawaida hapa Marekani; wadau wakishanunua kitabu na kusainiwa, wanapenda kupiga picha na mwandishi, ikiwezekana.

Mdau huyu, aitwaye Adrian, m-Marekani Mweusi, alinifahamu tangu miaka kadhaa iliyopita. Alikuwa anasoma katika chuo fulani mjini Minneapolis. Kulikuwa na mkutano wa kitaaluma, nami nilikuwa mmoja wa wanajopo, nikitoa mada. Adrian alivutiwa sana. Halafu, alinisikiliza tena mwaka jana, nilipokuwa naongea katika jopo la watu wawili, nikiwa na Profesa Mahmud el-Khati, m-Marekani Mweusi, tukiongelea mbele ya umati, mahusiano baina ya wa-Afrika na wa-Marekani Weusi.

Adrian ni msomi kijana makini. Tayari naona nyota yake imeanza kung'ara katika medani ya uongozi katika jamii. Nina imani atafika mbali katika jamii ya wa-Marekani weusi na Marekani kwa ujumla.
Hapa kushoto ni picha nyingine, kutoka hiyo hiyo juzi katika tamasha la Afrifest, nikiwa na mdau kutoka Liberia, ambaye alikuwa amenunua kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, nami nikiwa nimekisaini. Inaonekana aliguswa sana, na hakuweza kujizuia kuniwekea mkono wake begani pangu.

Suala hili la kusaini au kusainiwa vitabu linastahili  kutafakariwa. Naamini lina vipengele kadhaa muhimu, kama vile kiutamaduni, kisoshiolojia, kisaikolojia, na kifalsafa. hata katika maduka ya vitabu hapa Marekani, aghalabu utaona vimepangwa vitabu vya mwandishi vikiwa na ujumbe "Signed copy." Jambo hili linaisukuma akili yangu kutaka kulielewa zaidi. Ningependa kujifunza zaidi kuhusu suala hili, kwa kusoma maandishi mbali mbali na kufanya tafakari mwenyewe.

Saturday, June 11, 2011

Waandishi Tumekutana Leo

Leo nilienda Minneapolis kushiriki mkutano wa waandishi wa-Marekani Weusi, kama nilivyoandika hapa. Mkutano huu, uliofanyika katika Center for Families, ni sehemu ya maandalizi ya maonesho ya vitabu ya tarehe 16 mwezi huu, katika maktaba ya Magers and Quinn. Waandaaji wa shughuli zote hizi ni Jeffrey Groves na Shatona Kilgore-Groves, wanaoonekana hapa juu.

Mkutano wa leo ulikuwa ni wa kufahamiana. Kila mtu alipata fursa ya kutoa maelezo mafupi kuhusu maisha na shughuli zake za uandishi. Baadhi ni chipukizi, ambao wamechapisha kitabu kimoja tu, na baadhi ni wazoefu, waliochapisha vitabu kadhaa. Baadhi ya vitabu vinahusu maisha binafsi; vingine vinahusu mafunzo mbali mbali, hadithi za kubuni, mashairi, na falsafa. Wengine wameandika vitabu vya watoto. Nami nilipata fursa ya kuongelea vitabu nilivyoandika.
Watu waliongelea maisha yao na kwa nini wanaandika. Baadhi, kama hao akina mama wanoonekana kushoto, wamepitia maisha machungu yasiyoelezeka, yanayowafanya baadhi ya wanadamu wajiue. Kuandika ni namna ya kujiponya ili kuendelea na maisha
Baadhi ya waandishi nilikuwa nimefahamiana nao kabla, kama vile Mahmoud el Kati, Joyce Marrie, Gerard Montgomery, na Jeff na Shatona Groves, ambao kitabu chao, A Black Parent's Memoir, ninakiandikia mapitio. Lakini imekuwa bahati leo kufahamiana na waandishi wengi kwa mpigo.

Mkutano wa leo umeleta msisimko mkubwa miongoni mwa washiriki. Tumekubaliana kuwa kukutana kwa namna hii ni hatua nzuri na muhimu; inatakiwa iwe jadi ya kuendelezwa. Kutokana na mafanikio ya mkutano wa leo, sote tunayangojea kwa hamu maonesho ya Juni 16, ambayo watu wengi wanategemewa kuhudhuria.

Saturday, October 16, 2010

Maonesho ya Vitabu Minneapolis, Oktoba 16

Nimerejea jioni hii kutoka Minneapolis, kushiriki maonesho ya vitabu ambayo huandaliwa na jarida la Rain Taxi na kufanyika mara moja kwa mwaka.





Kama kawaida, nilipeleka vitabu vyangu. Nilikuwa nimelipia meza ndogo. Lakini hii ilitosha kwa vitabu tu, bila maandishi mengine. Kwa vile idadi ya vitabu vyangu si ile ile ya mwaka jana au mwaka juzi, siku zijazo itanilazimu kulipia meza kubwa ili niweze kuweka maandishi mengine pia.








Leo ninaleta hapa picha mbali mbali nilizopiga, kama mfano wa namna wa-Marekani wanavyojali suala la vitabu.








Kama nilivyosema siku zilizopita, wa-Marekani wanafurika kwenye maonesho ya vitabu. Wanafika tangu asubuhi, milango ya ukumbi inapofunguliwa. Na siku nzima watu wanakuwa wengi katika ukumbi, wakienda na kuja.







Wanafika watu wa kila rika: watoto, vijana, watu wazima, na waze, wanawake kwa wanaume.







Pamoja na hali ya uchumi wa Marekani kuwa mbaya miaka hii, watu wanavichambua vitabu na kuvinunua.







Wana dukuduku na hamu ya kusoma. Ukisikiliza maongezi yao, utawasikia wakiongelea sifa walizosikia kwa wenzao kuhusu kitabu hiki au kile. Au utawasikia wale waliosoma kitabu fulani wakiwaeleza wenzao na kuwahamasisha wanunue.



Mimi kama m-Tanzania ninashinda kwenye shughuli hizi nikiwa na masikitiko makubwa, kwani hali kama hii haiko Tanzania. Ninajua, kwa sababu ninashiriki maonesho ya vitabu kule, kama ninavyoripoti mara kwa mara katika blogu hii.






Ni wazi kuwa wa-Tanzania tumeshajichimbia kaburi katika dunia hii inayoendeshwa na elimu, ujuzi na maarifa. Tusijidanganye.







Kwa mtazamo wangu, dalili ya kuelimika ni kuwa na duku duku na hamu ya kudumu ya kujitafutia elimu. Shule inapaswa iwe ni chanzo tu na kichocheo cha duku duku na hamu hii ya kujitafutia elimu.






Kupata digirii, kwa mfano, si mwisho wa elimu, bali hatua moja au chachu katika safari ya kutafuta elimu. Hayo niliyaelezea pia katika mahojiano katika Kombolela Show.


Kama ninavyosema mara kwa mara, napenda sana kushirikia maonesho ya aina hii, kwani ni fursa ya kukutana na watu walio katika fani za uandishi, uchapishaji, uhariri na uuzaji wa vitabu. Kila mmoja wao ana jambo la kunichangamsha akili au kunipanua mawazo.




Kukutana na watu wanaotaka kununua vitabu ni jambo jingine linalonigusa. Wakati mwingi natumia kujibu maulizo ya watu wanaotaka kujua maandishi yangu yanahusu nini.



Watu wengi wanapoona kuwa natoka Afrika, wanapenda kuelezea vipengele vya maisha yao. Kama walishafika Tanzania au sehemu yoyote ya Afrika, wanaelezea. Kwa maana hiyo, kushiriki tamasha la vitabu ni kweli fursa ya kuonana na kufahamiana na watu wa aina mbali mbali.

Tuesday, September 7, 2010

Watoto wa Tanzania Wanapenda Vitabu

Wengi wetu tunalalamika kuhusu kufifia au kutoweka kwa utamaduni wa kununua na kusoma vitabu miongoni mwa wa-Tanzania. Inaonekana kuwa hata pale ambapo vitabu vipo, kama vile maktaba, wa-Tanzania hawaendi kusoma.

Ukweli ni kuwa tabia hii inajengeka na umri. Watoto wa Tanzania, wanapenda vitabu, sawa na watoto wengine popote. Nimeshuhudia hayo katika pita pita zangu Tanzania. Kwa mfano, ukienda kwenye maonesho ya vitabu Tanzania, utawaona watoto.

Mwanzoni mwa Septemba, 2004, kulikuwa na maonesho ya vitabu katika uwanja wa hifadhi ya kumbukumbu za Taifa, Dar es Salaam. Kama kawaida, waliohudhuria zaidi ni watoto.

Katika maonesho hayo, watoto wa shule walifanya michezo ya kuigiza, kuhusu umuhimu wa vitabu.
Waliimba pia nyimbo, wakiwahamasisha wazazi kuweka vitabu nyumbani na kuwa na utaratibu wa kusoma pamoja na watoto. Lakini, ujumbe wao uliishia hewani, kwani wazazi wenyewe hawakuwepo.

Wakati wa kuigiza mchezo, watoto hao walishika vitabu, kama vilelelezo. Nilimwona mtoto mmoja ameshika kijitabu changu kuhusu Things Fall Apart. Anaonekana hapa juu, wa pili kutoka kulia. Niliguswa na jambo hilo.

Mwaka huu, tarehe 24-25 Juni nilishiriki maonesho ya elimu na ajira, ambayo yaliandaliwa na Tripod Media. Yalifanyika Diamond Jubilee Hall, Dar es Salaam.
Nililipia banda, nikaweka vitabu vyangu na machapisho mengine, nikawa naongea na watu kwa siku zote mbili.

Walifika watoto wengi, na hapo nilijionea mwenyewe jinsi watoto walivyo na ari ya vitabu. Walikuwa wanaviangalia na waliniuliza masuali kem kem.
Nami nilitumia fursa hii kuwaelezea umuhimu wa kusoma na kutafuta elimu kwa dhati muda wote.



Nilipata faraja kubwa katika kuwa na watoto hao na kuona moyo wao juu ya vitabu.



Suali la msingi linabaki: Tufanyeje ili watoto waweze kukua na moyo huu walio nao bila kulegea au kufifia? Kuna njia gani ya kuwafanya watu wazima wahudhurie maonesho ya vitabu?

Katika jarida la Tanzania Schools Collection, toleo la kwanza, Moris Mwavizo anaripoti, ukurasa 12, kuwa katika maonesho fulani ya vitabu Dar es Salaam, mratibu mmoja alimwona mtoto akizunguka mwenyewe katika viwanja. Alipomwuliza kwa nini baba yake hakuja naye, mtoto alijibu kuwa baba yake angekuja kama kungekuwa na bia hapa kwenye maonesho. Je, hii si aibu?

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...