Showing posts with label minneapolis. Show all posts
Showing posts with label minneapolis. Show all posts

Sunday, June 2, 2013

Nimehudhuria Ibada ya Ki-Swahili, Minneapolis

 Leo, baada ya kukosekana kwa miezi mingi, nilienda kuhudhuria ibada ya ki-Swahili Minneapolis. Ni ibada ya madhehebu ya ki-Luteri, ambayo hufanyika katika kanisa la Holy Trinity Lutheran Church.

Ibada iliendeshwa na mchungaji Dr. Mwalilino. Kwaya iliendeshwa na ndugu Smart Baitani, mwanzilishi na mkurugenzi wa COSAD. Nilipopata fursa ya kuongea na Baitani, ambaye tumefahamiana kwa zaidi ya miaka ishirini, nilimtania kuwa sikutegemea kumwona Minneapolis wakati huu, kwani nilidhani yuko Muleba (Bukoba).

Kwenda kwangu leo kulitokana na mwaliko wa rafiki yangu, Mzee Paul Bolstad, anayeonekana wa pili kutoka kulia hapo pichani.

Aliniambia kuwa leo angekuwepo mchungaji mgeni, Herb Hafermann, ambaye anaonekana kushoto kabisa. Mchungaji huyu anaifahamu sana Tanzania, na ameishi kule miaka mingi. Mara yake ya kwanza kuja Tanzania ni mwaka 1963, na bado yuko kule. Alitoa mahubiri leo, kwa ki-Swahili. Anaongea ki-Swahili sawa na wa-Swahili, na michapo juu. Wakati huu mchungaji huyu yuko Lutheran Junior Seminary, Morogoro.

Nilimwambia kuwa nimewahi kufika katika chuo kile. Mzee Bolstad alimweleza kuhusu shughuli zangu za uandishi, na alitaja hasa kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Tulikubaliana kuwa niandae nakala nimpelekee mchungaji wakati akiwa bado hapa Marekani, ili ikawekwe katika maktaba ya Lutheran Junior Seminary. Mzee Bolstad ni mdau na mpiga debe mkubwa wa kitabu hicho, na pia mdau mkubwa wa blogu hii ya hapakwetu. Alizaliwa Tanganyika (Tanzania) na kukulia kule.

Nilikutana na watu wengi, wale tunaofahamiana na wengine tukafahamiana leo hii. Nilikutana na hata mdau wa blogu yangu, ambaye nilikuwa simjui. Aliniambia anaitwa Eric. Alinikosoa kwa kutoweka taarifa kila siku katika blogu, akatoa mfano wa namna taarifa yangu kuhusu safari ya Montana kumwona Mzee Patrick Hemingway ilikaa kwenye blogu siku nyingi, bila kuwekwa nyingine. Nami nilikubaliana naye kwamba huu ni udhaifu, nikaongezea kuwa Michuzi ndio anaiweza kazi hii, kwani anaweka taarifa nyingi kwenye blogu yake kila siku. Nilikiri wazi kuwa mtu kama mimi nababaisha tu kadiri ninavyoweza. Hata hivi, nilimwambia kuwa nimeguswa kumkuta mdau kama yeye, na kwamba itabidi nijitahidi kufuata ushauri wake, ili angalau iwe ni shukrani yangu kwa wadau wanaofuatilia blogu yangu.

Huyu mwenye Kaunda suti ni ndugu Charles Semakula, mratibu wa ibada ya ki-Kiswahili.

Saturday, October 16, 2010

Maonesho ya Vitabu Minneapolis, Oktoba 16

Nimerejea jioni hii kutoka Minneapolis, kushiriki maonesho ya vitabu ambayo huandaliwa na jarida la Rain Taxi na kufanyika mara moja kwa mwaka.





Kama kawaida, nilipeleka vitabu vyangu. Nilikuwa nimelipia meza ndogo. Lakini hii ilitosha kwa vitabu tu, bila maandishi mengine. Kwa vile idadi ya vitabu vyangu si ile ile ya mwaka jana au mwaka juzi, siku zijazo itanilazimu kulipia meza kubwa ili niweze kuweka maandishi mengine pia.








Leo ninaleta hapa picha mbali mbali nilizopiga, kama mfano wa namna wa-Marekani wanavyojali suala la vitabu.








Kama nilivyosema siku zilizopita, wa-Marekani wanafurika kwenye maonesho ya vitabu. Wanafika tangu asubuhi, milango ya ukumbi inapofunguliwa. Na siku nzima watu wanakuwa wengi katika ukumbi, wakienda na kuja.







Wanafika watu wa kila rika: watoto, vijana, watu wazima, na waze, wanawake kwa wanaume.







Pamoja na hali ya uchumi wa Marekani kuwa mbaya miaka hii, watu wanavichambua vitabu na kuvinunua.







Wana dukuduku na hamu ya kusoma. Ukisikiliza maongezi yao, utawasikia wakiongelea sifa walizosikia kwa wenzao kuhusu kitabu hiki au kile. Au utawasikia wale waliosoma kitabu fulani wakiwaeleza wenzao na kuwahamasisha wanunue.



Mimi kama m-Tanzania ninashinda kwenye shughuli hizi nikiwa na masikitiko makubwa, kwani hali kama hii haiko Tanzania. Ninajua, kwa sababu ninashiriki maonesho ya vitabu kule, kama ninavyoripoti mara kwa mara katika blogu hii.






Ni wazi kuwa wa-Tanzania tumeshajichimbia kaburi katika dunia hii inayoendeshwa na elimu, ujuzi na maarifa. Tusijidanganye.







Kwa mtazamo wangu, dalili ya kuelimika ni kuwa na duku duku na hamu ya kudumu ya kujitafutia elimu. Shule inapaswa iwe ni chanzo tu na kichocheo cha duku duku na hamu hii ya kujitafutia elimu.






Kupata digirii, kwa mfano, si mwisho wa elimu, bali hatua moja au chachu katika safari ya kutafuta elimu. Hayo niliyaelezea pia katika mahojiano katika Kombolela Show.


Kama ninavyosema mara kwa mara, napenda sana kushirikia maonesho ya aina hii, kwani ni fursa ya kukutana na watu walio katika fani za uandishi, uchapishaji, uhariri na uuzaji wa vitabu. Kila mmoja wao ana jambo la kunichangamsha akili au kunipanua mawazo.




Kukutana na watu wanaotaka kununua vitabu ni jambo jingine linalonigusa. Wakati mwingi natumia kujibu maulizo ya watu wanaotaka kujua maandishi yangu yanahusu nini.



Watu wengi wanapoona kuwa natoka Afrika, wanapenda kuelezea vipengele vya maisha yao. Kama walishafika Tanzania au sehemu yoyote ya Afrika, wanaelezea. Kwa maana hiyo, kushiriki tamasha la vitabu ni kweli fursa ya kuonana na kufahamiana na watu wa aina mbali mbali.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...