Showing posts with label ulabu. Show all posts
Showing posts with label ulabu. Show all posts

Friday, April 15, 2011

Hatimaye, Bia Zitazinduliwa Ikulu

Ni juzi tu hapo niliandika makala kuhusu jinsi wa-Tanzania wanavyowajibika katika unywaji wa ulabu. Makala hiyo ni "Kazi ya Kunywa". Katika kuhitimisha, nilitamka kuwa, kwa mwendo tunaokwenda, huko mbele ya safari ulabu utakuwepo hadi shuleni na Bungeni.

Ni kama vile niliota. Wiki hii wabunge wa Tanzania wameweka historia kwa kuzindua vinywaji vikali huko Dodoma. Soma hapa.

Nchi yetu ni ya pekee. Tunauenzi ulabu kiasi hiki, ingawa unasababisha au kuchangia matatizo mengi, kuanzia ajali barabarani zinazosababisha vifo vingi na watu wengi kuumia, uharibifu wa mali, magomvi katika jamii, kuharibika akili na matatizo ya kisaikolojia.

Tunakwenda kwa kasi na ari kiasi kwamba siku si nyingi kuanzia sasa, bia zitakuwa zinazinduliwa Ikulu. Na siku ya kuzindua bia itakuwa ni ya kukumbukwa ki-Taifa.

Enzi za uongozi wa Mwalimu Nyerere, wabunge wangekuwa wanazindua maktaba, si ulabu. Hakuna mtu aliyethubutu kufanya mambo yanayofanyika leo. Lakini mambo ndio hayo: akiondoka paka, panya hutawala.

Sunday, March 20, 2011

Kazi ya Kunywa

Ukiondoa kazi ya kukaa vijiweni, kazi muhimu ya wa-Tanzania wengi ni kunywa. Huyu jamaa kwenye katuni ni m-Tanzania halisi. Yuko kazini, wala hafanyi mchezo. Ameshaamrisha kuwa kaunta ihamie hapa alipo, tena haraka sana.



Wako wa-Tanzania ambao wanajifunza kunywa tangu utotoni. Wanapofikia ujana wanakuwa wameshahitimu.

Kazi ya kunywa ni muhimu kwa wa-Tanzania wengi kiasi kuwa wamehamia baa, na wanaishi huko, kama nilivyoandika hapa.

Shughuli nyingi za jamii Tanzania zinawezekana tu iwapo zinaendana na kunywa. Yaani ili watu waje kwenye hizi shughuli, ni muhimu ulabu uwepo. Hata kwenye uzinduzi wa kitu kama kitabu, ni muhimu pawe na ulabu, kama nilivyoelezea hapa.

Nilisoma kwenye jarida la Tanzania Schools Collection, 1, (2009), kuwa mtoto mmoja wa miaka kumi alionekana kwenye maonesho ya vitabu Dar es Salaam akiwa mwenyewe. Mratibu mojawapo wa maonesho alipomwuliza kwa nini hakuja na baba yake, mtoto alijibu kuwa baba angefika kama kungekuwa na bia (uk. 12).

Kwa mwendo huu, naweza kusema kuwa miaka ijayo, itabidi tuwe na bia kila mahali, kuanzia shuleni hadi Bungeni.

(Katuni nimeipata katika kitabu cha Kula...Mtoto wa Bosi, kilichoandikwa na Simon Regis na kuchapishwa na Regis Art Production, Dar es Salaam. Sikumbuki ni wapi nilipata hii picha nyingine. Ningependa kuweka taarifa ipasavyo)

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...