Thursday, February 11, 2010

Mwaliko wa Mhadhara: Kampuni ya RBC Wealth Management

Nimealikwa na kampuni ya RBC Wealth Management mjini Minneapolis, kwenda kutoa mhadhara tarehe 19 Februari. Kampuni hii ambayo shina lake ni nchini Canada, inafanya shughuli zake sehemu mbali mbali duniani, ikiwa na wafanyakazi wanaozidi 80,000.

Kama ninavyosema mara kwa mara katika blogu zangu na maandishi mengine, dunia ya leo inavyozidi kuwa kijiji, na watu wa mataifa na tamaduni mbali mbali kujikuta wakifanya kazi pamoja maofisini, vyuoni, katika biashara, na kadhalika, ni muhimu kujielimisha na masuala ya tofauti za tamaduni. Kujielimisha huko ni msingi mojawapo wa mafanikio.

Kampuni ya RBC Wealth Management imenialika makusudi ili kuongelea suala la mahusiano baina ya watu wa tamaduni mbali mbali wanaofanya kazi katika kampuni hiyo, kwani wafanyakazi hao wanatoka sehemu mbali mbali za dunia. Kampuni hii ilishanialika miaka michache iliyopita, kuongea na viongozi na maofisa wa kampuni kuhusu masuala haya haya. Walitaka kupata mawaidha kuhusu namna ya kushughulika na wafanyakazi wao kwa jinsi ya kujenga na kuimarisha mahusiano mema. Hii ni njia ya kuboresha ufanisi na kujiimarisha kibiashara.

Katika mwaliko wa awali, na katika mwaliko wa sasa, nimeombwa nikaongelee masuala yaliyomo katika kitabu changu cha Africans and Americans na yatokanayo. Wameagiza nakala za kuwatosha watakaohudhuria. Naafiki wazo hilo, kwani mtu anaweza kusahau yasemwayo katika mhadhara, lakini kitabu ni kitu cha kudumu, nyenzo ya elimu endelezi.

Kuanzia mwaka juzi nimeenda Tanzania na kuendesha warsha kuhusu utamaduni na utandawazi. Niliamua kufanya hivyo kwa kutambua umuhimu wa suala hili la kujiandaa. Nimeona jinsi taasisi, makampuni na jumuia za huku Marekani zinavyojiandaa. Na kwa vile ninashuhudia mwenyewe, nina uhakika na ninachosema. Ili wa-Tanzania waweze kushindana vizuri na kupata mafanikio katika dunia hii inayozidi kuwa kijiji, ni muhimu wajiandae pia. Huu ndio ujumbe wangu.

Mihadhara ninayotoa huku Marekani, ambayo naiongelea kwenye blogu zangu, inanijengea ujuzi na uzoefu. Si tu kwamba nawafundisha wale ninaoongea nao, bali nami naelimika. Ninapoenda kwenye sehemu kama hii kampuni ya RBC Wealth Management, ninasikiliza masuali kwa makini na kuelewa hali halisi ya sehemu hii. Ni uzoefu ambao naamini utawafaidia wa-Tanzania, wa-Afrika, na wengine hapa duniani. Huwa daima napenda kukutana na watu wenye ari ya kujielimisha, kwani mimi mwenyewe sichoki kutafuta elimu na kuwapa wengine. Ni mzunguko ambao naamini unainufaisha dunia.

Ratiba ya warsha zangu Tanzania mwaka huu inaandaliwa. Warsha ya kwanza, "Culture and Globalization," itafanyika Arusha Community Church, tarehe 3 Julai, kuanzia saa 4 hadi saa 7. Itafanyika kwa lugha ya ki-Ingereza kwani wahudhuriaji huwa ni wa mataifa mbali mbali. Karibuni.

3 comments:

Unknown said...

Kila la kheri Prof.

Mbele said...

Shukrani kwa ujumbe. Nangojea kwa hamu kukutana nao.

Mbele said...

Nimepata ujumbe leo kutoka RBC Wealth Management kuwa mazungumzo yangu yatarushwa hewani ili wasikilize hata walio nje ya Minneapolis na wapate fursa ya kuuliza masuali.

Nafurahi kupata fursa hii. Nina hakika nitawasisimua vilivyo.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...