Wednesday, February 17, 2010

Maongezi Mjini Faribault, Minnesota

Asubuhi leo nilikwenda mji wa Faribault, mwendo wa nusu saa. Nilikuwa nimealikwa na Mama Delane James, mkuu wa maktaba ya Faribault, kwenda kuongea na wafanyakazi wa maktaba kuhusu masuala ya utamaduni wa wa-Afrika.

Mji wa Faribault unazidi kuwa na watu kutoka pande mbali mbali za dunia, wengine wakiwa wakimbizi au wahamiaji wa kawaida au watafuta ajira. Miji mingi hapa Marekani inajikuta katika hali hiyo. Matokeo yake ni kuwa wenyeji wa miji hiyo na hao wageni wanakumbana na masuala yatokanayo na tofauti za tamaduni. Wahudumu wa maktaba wanakumbana na masuala hayo pia, kwani wageni hao nao ni wateja wa maktaba, ambapo wanatafuta ujuzi wa aina mbali mbali, kama vile lugha, ili kuweza kuyafahamu mazingira na maisha katika nchi ya Marekani.

Ingawa nilishafika katika maktaba ya Faribault mara kadhaa, sikutambua kuwa ina wafanykazi wengi kama niliowaona kwenye mkutano wa leo. Nilipata fursa ya kutoa mawaidha ya msingi kuhusu umuhimu wa kujifunza suala la tofauti za tamaduni, ili kuepusha matatizo. Nilizingatia uzoefu wangu na juhudi ninazofanya katika kujielimisha kuhusu tofauti hizo na kuwaelimisha wengine, iwe ni hapa Marekani au Tanzania.

Mji wa Faribault umewapokea watu wengi kutoka Afrika, hasa Somalia na Sudan. Kwa hivi, suala muhimu lililomfanya mkuu wa maktaba anialike ni kuelezea utamaduni wa watu hao. Mkuu wa maktaba na baadhi ya waliohudhuria walikuwa wameshasoma kitabu changu cha Africans and Americans, na waliuliza masuali kutokana na yaliyomo kitabuni. Pia waliwahamasisha wengine wote wakisome.

Mkutano ulikuwa wenye manufaa, na wahudhuriaji walisisitiza kuwa mazungumzo ya aina hii yanapaswa yafanyike sehemu zingine pia, kama vile shuleni na katika taasisi mbali mbali. Wanafanya mpango niende tena Faribault kutoa mhadhara kwa jamii na kusaini vitabu. Hayo nitaelezea yatakapotokea, panapo majaliwa.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...