Showing posts with label The Merchant of Venice. Show all posts
Showing posts with label The Merchant of Venice. Show all posts

Saturday, September 3, 2016

Shakespeare Ametawala Mawazo Yangu Leo

Leo Shakespeare ametawala mawazo yangu, nami ninapenda kuelezea ilivyotokea. Ni maelezo yanayoweza kubainisha namna akili yangu inavyofanya kazi ninapohangaika kuandika makala ya kitaaluma.

Kwa miezi kadhaa, nimekuwa nikiwazia kuandika makala juu ya utangulizi wa The Dilemma of a Ghost, tamthilia ya Ama Ata Aidoo wa Ghana. Utangulizi huu umeitwa "Prelude" katika tamthilia hiyo, ambayo Ama Ata Aidoo aliitunga alipokuwa mwanafunzi wa chuo kikuu Ghana, Legon, ambapo alihitimu mwaka 1963. Tamthilia yake iliigizwa kwa mara ya kwanza mwaka 1964 na kuchapishwa mwaka 1965.

Nimefundisha tamthilia hii mara kadhaa, na kwa miezi kadhaa nimepata hamu ya kuchambua utangulizi wake, yaani "Prelude." Nimeona kwamba hakuna mhakiki yeyote ambaye ameichambua sehemu hii ya tamthilia hii kwa kiwango kinachoniridhisha. Hii "Prelude" si rahisi kuifafanua. Ninahisi hii ndio sababu ya wachambuzi kuiacha kando.

Katika kuitafakari hii "Prelude," nimeona kuwa ujuzi wangu wa taaluma ya "Folklore" utakuwa nyenzo muhimu. Vile vile, nimeona kuwa italazimu kugusia jadi ya tamthilia ya nchi za Magharibi kuanzia Ugriki ya zamani.

Ni katika kuwazia jadi hii ndio nikajikuta ninamkumbuka Shakespeare. Katika "Prelude" yake, Ama Ata Aidoo ametumia dondoo za lugha ambazo zinatupeleka kwa Shakespeare. Sishangai, nikizingatia kuwa Ama Ata Aidoo alisomea ki-Ingereza na fasihi katika mfumo wa elimu wa ukoloni wa ki-Ingereza. Kwa maana hiyo, Ama Ata Aidoo alilelewa katika mfumo ambao walilelewa waandishi wa enzi zake, na waliofuatia, kama vile Efua Sutherland, Wole Soyinka, na James Ngugi, ambaye baadaye alibadili jina na kujiita Ngugi wa Thion'go.

Baada ya kujiridhisha kwamba kuna athari za Shakespeare katika "Prelude" ya The Dilemma of a Ghost, ndipo nikawa nawazia kutafuta ushahidi katika tamthilia za Shakespeare. Kwa miezi yote hii, nilikuwa na uhakika kwamba baadhi ya athari zimetoka katika tamthilia kadhaa na pia mashairi ya Shakespeare, na baadhi ya athari nilihisi zilitokana na au tamthilia ya The Merchant of Venice au Hamlet.

Kwa hivi, leo nimeteremsha kabatini buku langu kubwa liitwalo The Yale Shakespeare, ambalo lina tamthilia zote za Shakespeare na mashairi yake yote. Kila tamthilia imetanguliwa na insha iliyoandikwa na mchambuzi mahiri na imeambatana na maelezo ya dhana, misemo na maneno ambayo watumiaji wa leo wa ki-Ingereza inaweza kuwawia vigumu kuelewa.

Kwa miezi kadhaa, kabla ya kuanza kufukuafukua maandishi ya Shakespeare leo, nimekuwa nikitafakari vipengele vya "Folklore" ambavyo ninavyoviona katika "Prelude." Pia nimekuwa nikitafiti zaidi vipengele hivyo, kwa kufuatilia maandishi ya wataalam kama William Bascom. Sina shaka kwamba tafakari hiyo na utafiti vitaniwezesha kuifafanua "Prelude" na matumizi ya "Folklore" katika tamthilia nzima ya The Dilemma of a Ghost.

Monday, April 25, 2016

Kumbukumbu ya Kifo cha Shakespeare

Wiki hii ni ya kumbukumbu ya kifo cha William Shakespeare. Ingawa siku ya kufariki kwake haijulikani kwa uhakika, mapokeo yameiteua tarehe 23 April, 1616, kuwa ndio siku ya kufariki kwake. Alizikwa tarehe 25 Aprili.

Sisi tuliosoma sekondari miaka ya sitini na kitu tuliweza kusoma maandishi ya Shakespeare na kuyafurahia. Tulisoma tamthilia kama Julius Caesar na The Merchant of Venice. Baada sekondari, sisi tuliokwenda "high school" tulipata fursa ya kusoma na kutafakari tamthilia zake ngumu zaidi, kama vile Hamlet na Othello.

Mwandishi maarufu wa ki-Swahili, Shaaban Robert, alimwenzi Shakespeare. Alisema kwamba akili ya Shakespeare ilikuwa kama bahari ambayo mawimbi yake yalitua kwenye fukwe duniani kote. Laiti kama wa-Tanzania tungefuata nyayo za Shaaban Robert, tukaachana na ufinyu wa fikra kuhusu umuhimu wa lugha mbali mbali na fasihi za ulimwengu, kwa kisingizio cha kukienzi ki-Swahili.

Maandishi ya Shakespeare yana kauli nyingi maarufu. Sijui kama kuna msomaji wa Shakespeare ambaye hakumbuki ile hotuba ya Hamlet inayoanza hivi:

To be, or not to be: that is the question:
Whether 'tis nobler in the mind to suffer
The slings and arrows of outrageous fortune,
Or to take arms against a sea of troubles,
And by opposing end them? To die: to sleep;
No more; and by a sleep to say we end
The heart-ache and the thousand natural shocks
That flesh is heir to, 'tis a consummation
Devoutly to be wish'd.

Sijui kama kuna msomaji wa Shakespeare ambaye hakumbuki ile hotuba ya Mark Antony iliyomo katika Julius Caesar, inayoanza hivi:

Friends, Romans, countrymen, lend me your ears;
I come to bury Caesar, not to praise him.
The evil that men do lives after them;
The good is oft interréd with their bones;
So let it be with Caesar. The noble Brutus
Hath told you Caesar was ambitious:
If it were so, it was a grievous fault,
And grievously hath Caesar answer'd it.

Kuna pia kauli maarufu katika tamthilia ya As You Like It, ambayo ni ya mhusika aitwaye Jaques. Anasema kuwa dunia ni jukwaa, ambapo kila binadamu ni kama mwigizaji:

All the world’s a stage,
And all the men and women merely players;
They have their exits and their entrances,
And one man in his time plays many parts,
His acts being seven ages.

Shakespeare aliona mbali. Kwa mfano, unaposoma The Merchant of Venice, unajionea jinsi Shakespeare alivyokuwa na upeo wa fikra wa kutambua tabia ya ubepari mapema kabisa, wakati ulipokuwa unachimbuka. Haishangazi kwa nini Mwalimu Nyerere, ambaye alikuwa katika harakati za kupambana na ubepari na kujenga ujamaa aliamua kuitafsiri tamthilia hii, akaiita Mabepari wa Venisi.

Shakespeare alizielezea kwa umakini tabia za binadamu, njema au mbaya. Katika tamthilia ya Macbeth, kwa mfano, tunashuhudia jinsi binadamu anavyoweza kuwa mbaya, na kama wewe ni msomaji wa Shaaban Robert utakumbuka jinsi naye alivyoielezea dhamira hii, kwa mfano katika Adili na Nduguze.

Shakespeare alikuwa mtunzi wa tamthilia na mashairi. Alitunga mashairi mengi, na baadhi ya hayo yako katika tamthilia zake. Haiwezekani kumtendea haki Shakespeare kwa kuelezea mchango wake katika makala ndogo kama hii. Kuna makala nyingi na vitabu juu yake na kazi zake, na maandishi yanaendelea kuchapishwa katika lugha nyingi. 

Kama Shaaban Robert alivyosema, akili ya Shakespeare ni kama bahari, ambayo mawimbi yake yanatua kwenye fukwe duniani kote. Ni miaka mia nne imepita tangu Shakespeare afariki, lakini mawimbi ya akili yake yataendelea kumwagika duniani kote.

Sunday, January 24, 2016

Nimemkumbuka Shakespeare

Leo, bila kutegemea, nimemkumbuka Shakespeare. Nimeona niandike neno juu yake, kama nilivyowahi kufanya. Nimekumbuka tulivyosoma maandishi yake tukiwa vijana katika shule ya sekondari.

Katika kiwango kile, tulisoma tamthilia tulizozimudu, kama The Merchant of Venice na Julius Caesar. "High school," ambayo kwangu ilikuwa Mkwawa, tulisoma tamthilia ngumu zaidi, kama Othello na Hamlet. Othello ilikuwa katika silabasi ya "Literature."

Nakumbuka sana kuwa hapo hapo Mkwawa High School tuliangalia filamu ya Hamlet, ambamo aliyeigiza kama Hamlet alikuwa Sir Lawrence Olivier. Huyu ni mmoja wa waigizaji maarufu kabisa wa wahusika wakuu wa Shakespeare. Niliguswa na uigizaji wake kiasi cha kujiaminisha kwamba sitaweza kushuhudia tena uigizaji uliotukuka namna ile. Nilipoteza hamu ya kuangalia filamu yoyote baada ya pale, kwa miaka mingi.

Ninavyomkumbuka Shakespeare, ninajikuta nikikumbuka mambo mengi. Kwa mfano, nakumbuka tafsiri murua za Mwalimu Julius Nyerere za tamthilia mbili za Shakespeare: The Merchant of Venice na Julius Caesar. Nakumbuka pia jinsi Shaaban Robert alivyomsifu Shakespeare, kwamba akili yake ilikuwa kama bahari pana ambayo mawimbi yake yalikuwa yanatua kwenye fukwe zote duniani.

Shaaban Robert alitoboa ukweli; Shakespeare ni mwalimu asiye na mfano. Aliingia katika nafsi za wanadamu akaelezea silika na tabia zao kwa ustadi mkubwa, na alitafakari uhalisi wa maisha yetu akatuonyesha maana na mapungufu yake. Alitukumbusha kwamba dunia ni kama jukwaa la maigizo, ambapo kila mmoja wetu anakuja na kutimiza yanayomhusu na kisha anatoweka.

Ningeweza kusema mengi juu ya Shakespeare. Ninapenda tu kuleta moja ya tungo zake ziitwazo "sonnets." Hii ni "sonnet" namba 2. Labda kuna siku nitapata hamu ya kuutafsiri utumgo huu, kujipima uwezo wangu wa kutafsiri na ufahamu wangu wa ki-Swahili.

Sonnet 2

When forty winters shall besiege thy brow
And dig deep trenches in thy beauty’s field,
Thy youth’s proud livery, so gazed on now,
Will be a tattered weed, of small worth held.
Then being asked where all thy beauty lies,
Where all the treasure of thy lusty days,
To say within thine own deep-sunken eyes
Were an all-eating shame and thriftless praise.
How much more praise deserved thy beauty’s use
If thou couldst answer, “This fair child of mine
Shall sum my count and make my old excuse,”
Proving his beauty by succession thine.
  This were to be new made when thou art old,
  And see thy blood warm when thou feel’st it cold.

Saturday, April 18, 2015

Misahafu na Balaa Linaloitwa Dini

Si kila kinachoitwa dini ni dini. Katika historia, kumekuwepo na uovu mwingi ambao umefanyika kwa jina la dini. Hadi leo, uovu wa aina hiyo unaendelea kufanyika. Siku nyingine, panapo majaliwa, nitaleta na kuongelea mifano, kwa uwazi na haki.

Misahafu imetumika na inaendelea kutumika kuhalalisha uovu. Kwa kiasi fulani hii ni kwa sababu mtu anaweza kuzipata nukuu kutoka katika msahafu ambazo zinapingana au zina utata. Lakini vile vile ni suala la tafsiri. Wataalam wa lugha wanatueleza kuwa matumizi ya lugha yanatoa mwanya wa tafsiri mbali mbali.  

Kwa msingi huo, watu waovu wanaweza kutafsiri nukuu za msahafu kwa namna ya kuhalalisha uovu. Katika tamthilia ya Shakespeare, The Merchant of Venice, Antonio anasema, "The devil can cite Scripture for his own purpose." Shetani anaweza kunukuu msahafu kwa faida yake mwenyewe. Historia imethibitisha ukweli huo tena na tena.
 

Tatizo jingine ni imani miongoni mwa waumini wa dini kwamba kila kilichomo katika misahafu sherti kikubaliwe na kufuatwa kilivyo, bila mabadiliko. Imani hii ni chanzo cha matatizo makubwa.

Mtu ukiusoma msahafu wowote bila upendeleo wala ushabiki, utaona kuwa msahafu ulitokea katika mazingira maalum ya kihistoria, kijamii, na kitamaduni. Kuna mambo katika misahafu ambayo yalikusudiwa kwa jamii za zamani, na hayatuhusu sisi watu wa leo.

Kwa msingi huu, ni muhimu tujijengee utamaduni wa kuichambua misahafu ili tuone ni yepi yanatufaa na yepi yaliwafaa watu wa zamani lakini hayatufai sisi watu wa leo.


Mungu ametujalia akili. Tuzitumie. Mungu ametuweka katika dunia tofauti na ile ya watu wa zamani. Tuna ufahamu  na akili tofauti na watu wa zamani, katika masuala kama haki za binadamu.

Utandawazi wa leo na tekinolojia imetupa ufahamu tofauti wa ulimwengu na watu wake, ufahamu wa mahusiano tunayoyahitaji katika dunia ya leo ambayo siku hadi siku inageuka kuwa kijiji.

Je, katika mazingira hayo, ni sahihi kuishikilia misahafu neno kwa neno, kikasuku, badala ya kupambanua yale yanayotuhusu na yale yaliyowahusu watu wa zamani? Je, ukasuku huu, unaosababisha au kuhalalisha balaa juu ya balaa, na maovu ya kila aina, ndio dini?

Kwa kumalizia ujumbe wangu, napenda kusisitiza mtazamo wangu kuwa mijadala ya dini ni muhimu, kama nilivyowahi kuelezea katika blogu hii.

 

Sunday, December 28, 2014

"As You Like It:" Kitabu cha Kumalizia Mwaka

Nimeanza kusoma As You Like It, moja ya tamthilia za Shakespeare. Ni wazi kuwa, nikizingatia kwamba leo ni tarehe 28 Desemba, hiki kitakuwa kitabu cha kumalizia mwaka.

Kama zilivyo tamthilia zingine za Shakespeare, As You Like It ni hazina kubwa ya mafundisho kuhusu mahusiano baina ya wanadamu na kuhusu maisha kwa ujumla. Tamthilia yoyote ya gwiji huyu, sawa na mashairi yake, ni hazina ya lugha ya ki-Ingereza.

Ningefurahi kama ningekuwa nimesoma angalau kitabu kimoja kwa kila wiki. Padre Lambert Doerr, OSB, mwalimu wetu wa ki-ingereza tulipokuwa tunasoma seminari ya Likonde, ambaye sasa ni abate askofu mstaafu, alitushinikiza kusoma angalau kitabu kimoja kwa wiki. Kila mmoja wetu alipewa daftari ambamo alitakiwa kuorodhesha vitabu alivyosoma, na alitegemewa kuweza kutoa maelezo mafupi kuhusu kila kitabu. Ningefurahi kama ningeweza kuendeleza jadi hii miaka yote.

Nirudi tena kwenye As You Like It. Simulizi inapoanza, tunamsikia Orlando akilalamika kuwa amedhulumiwa na kaka yake mkubwa, Oliver, kuhusu urithi. Anasema kuwa baba yao aliacha wosia kwamba Oliver amgawie yeye Orlando fungu fulani la mali yake na pia amsomeshe, lakini Oliver hakufanya hvyo. Dhuluma hii inamsononesha Orlando.

Mtindo huu wa kuanzia simulizi na mhusika akielezea masononeko tunauona pia katika tamthilia ya Shakespeare iitwayo The Merchant of Venice. Halafu katika sehemu hii ya mwanzo ya As You Like It kuna pia dhamira ya kiongozi kuporwa madaraka na ndugu yake, dhamira ambayo inajitokeza pia katika The Tempest, tamthilia nyingine ya Shakespeare. Hili suala la Shakespeare kurejea tena na tena kwenye dhamira au kipengele fulani cha sanaa yake nimeligusia kabla katika blogu hii.

Tangu mwanzoni mwa As You Like It, Shakespeare anatuweka katika hamaki ya kujua nini kitakachofuata katika mtiririko wa matukio. Vile vile, kama ilivyo kawaida yake, anatupeleka mbali katika ulimwengu wa fasihi na masimulizi na imani za zamani, kuanzia enzi za wa-Griki hadi wa-Ingereza wenyewe. Mifano ya wahusika wa masimulizi hayo ni Fortune na Robin Hood.

Sijui kama nitaweza kumaliza kusoma tamthilia hii kabla ya mwaka mpya kuanza, lakini nitajitahidi. Jambo moja linalonifanya nisome pole pole ni kuvutiwa na umahiri wa Shakespeare katika kutumia lugha kwa namna ambayo aghalabu haionekani katika ki-Ingereza cha leo. Ni aina ya chemsha bongo.

Sunday, November 30, 2014

Kuhusu "Macbeth"

Makala hii nilianza kuiandika mara tu baada ya kuanza kusoma Macbeth, tamthilia ya Shakespeare, ambayo niliitaja hapa na hapa. Jana usiku nimefika mwisho wake. Inafurahisha kujisomea namna hii, bila msukumo kutoka popote.

Hapa na pale katika Macbeth nimejikuta nikiyakumbuka maandishi mengine ya Shakespeare ambayo niliyasoma zamani, kama vile The Merchant of Venice, Othello, The Tempest, na Twelfth Night. Hii ni kwa sababu kuna mawazo ambayo yanajitokeza tena na tena katika maandishi ya Shakespeare. Wazo mojawapo ni kwamba dunia ni jukwaa ambapo sisi wanadamu ni waigizaji. Kuna misemo pia ambayo inajitokeza tena na tena.

Kwa mfano, nilivyosoma katika Macbeth kauli ya mchawi kuhusu meli kukumbwa na dhoruba (I, III, 25-26) nimekumbuka The Tempest. Nilivyokutana na usemi huu wa mfalme kwa kapteni shujaa: "So well thy words become thee as thy wounds; They smack of honor both," (I, II, 47-48) nimekumbuka hotuba ya Portia katika The Merchant of Venice, ambamo anaelezea thamani ya huruma.

Kati ya mambo anayosema kuhusu thamani ya huruma ni kwamba "It becomes the throned monarch better than his crown." Kwa tahadhari, niseme kuwa neno "becomes" anavyolitumia Shakespeare, lina maana tofauti kabisa na ile tunayoijua. Jambo hilo nilishaligundua katika kusoma tamthilia za Shakespeare.

Unaposoma Macbeth, sawa na kazi nyingi maarufu za fasihi, mahusiano ya namna hii hujitokeza, sio tu baina ya maandishi ya mwandishi mmoja, bali pia baina ya maandishi ya waandishi mbali mbali. Katika nadharia ya fasihi, mahusiano hayo huitwa "intertextuality" kwa ki-Ingereza.

Kufafanua zaidi wazo hili, napenda kusema kuwa jambo moja lililonistua katika Macbeth ni pale Fleance anaposema, "The moon is down; I have not heard the clock" (II, I, 2). Hapo nilikumbuka riwaya ya John Steinbeck, The Moon is Down, nikapata shauku ya kufuatilia kama kuna uhusiano. Lo, nimegundua kuwa Steinbeck alipata jina la riwaya yake hapo kwenye tamthilia ya Macbeth.

Ni wazi kuwa kusoma vitabu kunasisimua akili. Unaposoma masimulizi ya aina hii, ubongo unafanya kazi muda wote, kukumbuka hiki au kile, kuelewa kile unachosoma, na pia kubashiri kinachofuata katika mtiririko wa matukio.Kuelewa huko na kukumbuka vimefungamana. Akili hailali; inapata mazoezi, sawa na mazoezi ya viungo vyovyote vya mwili. Manufaa yake ni makubwa.

Ninavyosoma Macbeth, nakumbuka vizuri taarifa niliyosoma miaka kadhaa iliyopita kuhusu onesho la Macbeth lililofanywa Uingereza na kikundi cha waigizaji cha wa-Zulu. Niliisosoma makala hiyo, "The Zulu Macbeth," katika jarida la The New African, kama sikosei. Kuna ripoti kadhaa mtandaoni kuhusu onesho hilo la tamthilia ya Macbeth ya ki-Zulu, ambayo ilitungwa na Welcome Msomi na kupewa jina la "Umabatha." Kwa mfano, soma makala hii.

Ningeweza kuandika makala ndefu kuhusu Macbeth, nikijadili masuala kama dhamira, wahusika, mawaidha, falsafa, na umahiri wa Shakespeare katika kutumia lugha. Pamoja na mengine yote, Shakespeare ni mwanafalsafa anayefikirisha. Kwa mfano, tafakari kauli hii maarufu ya Macbeth mwenyewe, mhusika mkuu wa tamthilia hii, anapoambiwa kuwa mke wake amefariki:

She should have died hereafter;
There would have been a time for such a word.
Tomorrow, and tomorrow, and tomorrow
Creeps in this petty pace from day to day
To the last syllable of recorded time;
And all our yesterdays have lighted fools
The way to dusty death. Out, out, brief candle!
Life's but a walking shadow, a poor player,
That struts and frets his hour upon the stage
And then is heard no more. It is a tale
Told by an idiot, full of sound and fury,
Signifying nothing (V, V, 19-30).

Kwa kuhitimisha, napenda kusema kuwa nimefurahi sana kuisoma Macbeth hadi mwisho. Najisikia raha kuwa nimeongeza kitu cha thamani katika akili yangu. Ndivyo inavyokuwa katika kusoma vitabu vyenye thamani.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...