Monday, November 24, 2014

Mwaliko wa Profesa Barbara Zust

Asubuhi hii, nimefika ofisini na kukuta ujumbe kutoka kwa Profesa Barbara Zust wa Chuo cha Gustavus Adolphus, Minnesota. Ananiulizia iwapo naweza kwenda kuongea na wanafunzi wake tarehe 4 au 5 Januari, katika matayarisho yao ya kwenda Tanzania kimasomo. Nimempigia simu, tukakubaliana niende tarehe 5.

Profesa Zust amenialika mara kwa mara anapoandaa wanafunzi wake kwa safari ya Tanzania. Nimewahi kuandika taarifa hizo, kwa mfano hapa, hapa, na hapa. Wanafunzi hao huwa wamesoma kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Mihadhara yangu huhusu masuala ninayoongelea kitabuni, nami hupenda sana kujibu au kujadili masuali wanayokuwa nayo.

Nimefurahi kwa jinsi Profesa Zust alivyonieleza umuhimu wa mikutano yangu na wanafunzi hao. Nimefurahi pia kuwa yeye na wanafunzi wanaona ninachofanya kina faida kubwa kwao. Ni wazi kuwa, ingekuwa hawafaidiki, hawangekuwa wananialika tena na tena.

Kwa hivi, siku yangu ya leo imeanza vizuri, nami nimeona niweke kumbukumbu hii hapa.

Nimekumbuka pia jinsi Profesa Zust na mwenzake Profesa Paula Swiggum, walivyoanza kunialika kuongelea kitabu changu kwa wanafunzi ambao wanasomea uuguzi ("nursinng"). Nilijiuliza inakuwaje mimi, ambaye sina utaalam wowote katika uwanja huu, niwe na lolote la kuwagawia wanafunzi wa somo hilo.

Katika kutafakari suala hilo, nilianza kusoma maandishi mbali mbali, nikagundua kuwa kwenye huu uwanja wa uuguzi wameingiza kipengele kiitwacho "transcultural nursing." Maana yake ni kwamba wanawafundisha wanafunzi kuhusu athari za tofauti za tamaduni katika kuwashughulikia wagonjwa.

Watu wa tamaduni tofauti wanauchukulia au wanauelewa ugonjwa, au uponaji, au wadhifa wa muuguzi, kwa misingi tofauti, kufuatana na utamaduni wao. Muuguzi akijua jambo hilo, anakuwa amejiandaa kuepuka kutoelewana na mgonjwa, na ana nafasi nzuri ya kutoa huduma muafaka kwa mgonjwa.

Katika kujisomea kuhusu mambo hayo ya "transcultural nursing," nimejifunza na ninaendelea kujifunza mengi, na papo hapo naelewa kwa nini watu kama Profesa Zust wanapenda niongee na wanafunzi wao. Nimeelewa vizuri kuwa kuna dhana nyingine ambayo inamwangalia mgonjwa katika mkabala mpana kuliko tu kile kinachomsumbua. Kuna uwezekano wa kuwepo masuala ya kisaikolojia na ya mahusiano katika jamii, ambayo ni muhimu katika kumwelewa na kumshughulikia mgonjwa. Kwa ki-Ingereza hii huitwa "holistic approach." Kwa kuzingatia hiyo dhana, nimeelewa zaidi kwa nini mambo kama yale niliyoandika kitabuni yanathaminiwa hata katika fani hii ya uuguzi.

Jana katika blogu hii, mdau Malifa Michael alniuliza kama nina mpango wa kutoa mwendelezo wa kitabu changu, nami katika kumjibu, niliongelea mambo kadhaa, likiwemo hilo la kutoa mihadhara itokanayo na kitabu, kwamba ni sehemu ya mwendelezo.

Namshukuru Mungu kwa kunipa fursa hizi za kuwaandaa vijana wanapoenda nchini kwetu, kutembelea sehemu mbali mbali, kujionea taasisi zinazohusika na masuala ya afya na matibabu, na kujumuika na wa-Tanzania katika utamaduni wetu.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...