Showing posts with label Zumbrota. Show all posts
Showing posts with label Zumbrota. Show all posts

Tuesday, April 7, 2015

Mhadhara Ujao, Lands Lutheran Church

Siku zimekwenda kasi. Wiki kadhaa zimepita tangu nilipopata mwaliko wa kwenda kutoa mhadhara katika mkutano wa Sinodi ya Kusini Mashariki ya Minnesota. Mkutano ulipangwa kufanyika mjini Zumbrota, kwenye Kanisa la Lands Lutheran, tarehe 11 Aprili.

Mama aliyenialika, kwa niaba ya kamati ya maandalizi, alisema kuwa wangependa niongelee masuala ambayo yameanza kujitokeza katika sharika mbali mbali za sinodi kutokana na kuingia kwa watu kutoka tamaduni mbali mbali. Aliniambia kuwa aliwahi kunisikiliza miaka kadhaa iliyopita katika kanisa lake la First English Lutheran Church, mjini Farbault, nikiongelea masuala hayo, akanunua kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Wiki zilizofuata, mama huyu nami tuliwasiliana ili kupanga mada ya mhadhara wangu. Nilitoa mapendekezo, naye aliyawasilisha kwenye kamati yao. Pendekezo walilolichagua ni "The Dilemma of Cultural Differences: Challenges and Opportunities."

Niliandika taarifa ya mwaliko katika blogu yangu ya ki-Ingereza. Sasa siku imekarbia, nami nangojea kwa hamu kwenda kujumuika na waumini hao kutoka makanisa mbali mbali, na kuwapa mawazo na mawaidha yangu kuhusu hali wanayoikabili ya kujikuta wana watu wa tamaduni mbali mbali. Azma yao ya kutaka kujua nini cha kufanya ni mfano wa kuigwa.

Kadiri dunia inavyoendelea kubadilika kutokana na utandawazi wa leo, jamii zote zitalazimika kutafuta njia za kuishi pamoja na watu wa tamaduni tofauti. Hili ni suala ambalo nimelitafiti, kulitafakari, na kuliongelea kwa miaka mingi.

Kama ilivyo kawaida hapa Marekani, niliulizwa malipo yangu ni kiasi gani. Nilijibu kama nilivyozoea, kwamba waamue wenyewe, kufuatana na uwezo wao. Nasukumwa na dhamiri yangu, kutumia vipaji alivyonipa Mungu kwa manufaa ya wanadamu. Pesa si msingi.

Ningekuwa na uchu wa pesa, kama fisadi, ningesema ngoja niwakamue. Lakini mtu unayemtegemea Mungu unajiuliza: Je, tunabarikiwa kwa kutanguliza pesa mbele badala ya ubinadamu? Ninashukuru ninavyofanikiwa kuwagusa wanadamu.

Sunday, November 16, 2014

Mwandishi Unapoitwa Kuongelea Kitabu Chako

Siku hizi, mara kwa mara, nawazia jukumu linaloningoja, la kwenda mjini Zumbrota, Minnesota, kutoa mhadhara. Mada ni "Incorporating Immigrants into our Culture and Worship," kama nilivyoeleza katika blogu hii. Mwaliko wa kutoa mhadhara huu umetokana na kitabu nilichoandika, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Sikualikwa nikaongelee kitabu hiki, lakini kwa hali yoyote, baadhi ya yaliyomo kitabuni yatajitokeza katika mhadhara na katika kipindi cha majibu na masuali. Napenda kusema machache kuhusu jukumu la kutoa mhadhara kuhusu kitabu ulichoandika.

Mara nyingi, hutokea kwamba watu utakaozungumza nao wanakuwa wameshakisoma kitabu. Ni lazima utafakari kabla kwamba utaongelea nini, na jambo hilo hutegemea aina ya kitabu.

Kama ni riwaya, watu hutegemea utawaeleza mambo kama vile nini kilikuwa chanzo cha wewe kuandika, yaani nini kilichokufanya uandike, njia uliyopitia katika kuandika, maandishi au waandishi waliokuathiri, matatizo uliyokumbana nayo, na mambo uliyojifunza.

Lakini, watu hutegemea pia, au labda zaidi, kuwa utasoma angalau kurasa kadhaa za riwaya yako, ili wasikie sauti yako na sauti ya wahusika katika hadithi yako kwa mujibu wako wewe kama mtunzi.

Hapa kushoto tunamwona mwandishi Nuruddin Farah wa Somalia, alipokuwa anaongelea riwaya yake mpya ya Crossbones, chuoni Carleton. Anaonekana akisoma kurasa kadhaa.

Wasikilizaji huvutiwa kumsikia mwandishi namna hiyo, kwani usomaji wake ni aina ya tafsiri sio tu ya kile alichoandika, bali kilichokuwa mawazoni mwake wakati anaandika. Watu huamini kuwa usomaji wa mwandishi una ukweli na uhalisi ambao msomaji mwingine hawezi kuufikia.


Hiyo ndiyo halisi inavyokuwa, iwapo kitabu ni riwaya au mashairi. Sauti na usomaji wa mwandishi vina mvuto huo niliouelezea, ingawaje kwa kifupi.

Lakini kuna pia vitabu vya aina tofauti, kama hiki changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Unapokuwa umealikwa kuongelea kitabu cha aina hiyo, ni lazima utafakari vizuri suala zima.

Iwapo watu hao wameshakisoma, nadhani jukumu lako sio kuwasomea kurasa za kitabu, bali ni kuongelea mambo yatokanayo na yale uliyoandika. Jukumu lako ni kufafanua baadhi ya yale uliyoandika, ambayo unaamini yanakidhi mahitaji ya watu watu wale, kufuatana na mwaliko wao.

Pengine, inawezekana uzungumze bila kufungua kitabu, ingawa unacho mbele yako. Kwa mfano, kwenye hii mada ya mhadhara wangu wa Zumbrota, siamini kama nitahitaji kuwasomea kurasa zozote kutoka kitabuni. Badala yake, ikibidi, nitajumlisha mafundisho yatokanayo, yenye kukidhi mategemeo ya mada.

Aina hii ya mhadhara nimeshatoa mara nyingi. Kwa mfano, hapa kushoto ninaonekana nikiongea na wanachuo waliokuwa wanajiandaa kwenda Afrika Kusini kwenye ziara ya kimasomo. Walishasoma kitabu changu, na profesa wao aliniita kuja kuongelea masuala ya aina niliyozungumzia kitabuni, kama sehemu ya maandilizi ya safari ya wanafunzi wale. Kwa vile wanafunzi walikuwa wameshasoma kitabu, mhadhara huu ulitawaliwa zaidi na masuali na majibu. Profesa wao aliandika kuhusu mhadhara wangu katika blogu yake.

Kwa ujumla, fursa hizi hunifurahisha, sio tu kwa sababu nakutana na wasomaji na wadau wengine ana kwa ana, bali pia napata wasaa wa kujipima ni kiasi gani naifahamu mada husika na vipengele vyake.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...