Profesa wao aliniomba nikaongee nao kuhusu masuala ya aina hiyo kwa mapana kufuatia yale niliyoandika katika kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, ambacho watakuwa wamekisoma kabla ya mimi kukutana nao.
Kutokana na kusoma hiki kitabu, wanachuo hao watakuwa wameandaa masuali. Kama ilivyotokea siku zilizopita, masuali mengine yatazuka hapo hapo.
Jukumu hili linanifanya nikipitie tena kitabu changu, angalau kijuujuu, kwani sina mazoea ya kusoma sana yale ambayo nimeshayaandika na kuyachapisha. Napendelea kutumia muda wangu na akili yangu katika kutafiti, kutafakari na kuandika mambo mapya. Ingawa yale yaliyomo kitabuni sijayabadili, na sijaona sababu ya kuyabadili, ninafahamu mengi zaidi na naendelea kujifunza, kwani elimu haina mwisho.
Kutokana na ukweli huu, mazungumzo yangu na hao wanachuo wa safari hii hayawezi kuwa sawa na yale ya miaka iliyopita. Hata kama kutakuwa na masuali yanayofanana na yale ambayo nimeshaulizwa kabla, majibu yangu yatajengeka katika upeo mpana zaidi. Fursa za aina hii zinachangia kupanua upeo huo.
Tutakutana, kama siku zilizopita, Mount Olivet Conference & Retreat Center, pembeni mwa mji wa Lakeville, Minnesota. Nangojea kwa hamu kuonana tena na Profesa Zust, na kuonana na hao wanachuo wapya. Panapo majaliwa, nitaweka ripoti katika blogu hii, kama nilivyozoea.
No comments:
Post a Comment