Showing posts with label Afrifest Foundation. Show all posts
Showing posts with label Afrifest Foundation. Show all posts

Saturday, April 22, 2017

Yatokanayo na Ziara Ubalozi wa Tanzania Marekani

Wiki hii, tarehe 19, binti yangu Zawadi na mimi tulikwenda kwenye Ubalozi wa Tanzania mjini Washington DC kushughulikia pasposti mpya baada ya paspoti zetu kwisha muda wa matumizi yake. Nimeona niandike mambo yaliyoibuka mawazoni mwangu kutokana na ziara hiyo.

Kwanza tulijisikia vizuri kuingia katika jengo la Ubalozi, na kujisikia tumo katika ardhi ya Tanzania. Nilimweleza binti yangu jambo hilo, nikaongezea kwamba mtu wa taifa lolote akiingia humu kutafuta hifadhi na akapata, mamlaka ya nchi yake haiwezi kuingia na kumkamata. Itabidi wajaribu bahati yao kwa kufanya utaratibu wa kuiomba Tanzania ili wakabidhiwe huyu mtu wao. Tulitaja mfano wa Julian Assange wa WikiLeaks ambaye amejichimbia katika Ubalozi wa Ecuador, London.

Wazo jingine lililonijia tulipokuwa ndani ya Ubalozi ni jinsi wadhifa wa kuiwakilisha nchi ulivyo mkubwa na mzito nikilinganisha na uchache wa wawakilishi wetu katika Ubalozi. Ni wazi kuwa watu wachache tunaowapa wadhifa wa kuiwakilisha nchi yetu katika ofisi ya ubalozi hawawezi kufika kila mahali katika nchi kubwa kama hii ya Marekani. Kwa kuzingatia hilo, ni wazi kuwa sisi Wa-Tanzania wanadiaspora vote tunawajibika kuiwakilisha nchi yetu pale tulipo na tunapopata fursa ya kuwepo katika maeneo mengine.

Mimi ninakaa katika mji wa Northfield, jimbo la Minnesota, ambao ni mdogo sana lakini ni maarufu kwa kuwa na vyuo vikuu viwili: St. Olaf na Carleton. Katakana na wadhifa wangu kama mwalimu ninayeshughulika na watu kutoka sehemu zote za Marekani na sehemu mbali mbali duniani, nina fursa ya kufanya mengi pasipo kutegemea Ubalozi.

Ninashiriki matamasha, ninatoa mihadhara, na ninashiriki mikutano ya aina aina. Ninashiriki katika uendeshaji wa jumuia zinazowajumlisha watu wa mataifa mbali mbali hapa Minnesota, kama vile Afrifest Foundation. Wakati huu, baada ya kuteuliwa katika bodi ya Rochester International Association, nina wadhifa mwingine muhimu. Katika nafasi zote hizo, ninajiwakilisha mwenyewe lakini pia kama raia wa Tanzania.

Ingawa nilijua tangu zamani kuwa sisi wananchi tuna wajibu wa kuiwakilisha nchi yetu popote tulipo, ziara yangu Ubalozini imenipa hamasa zaidi katika mwelekeo huo. Nimesukumwa zaidi na ukweli kwamba wafanyakazi wa Ubalozini hawatoshi kabisa kwa majukumu yaliyopo ya kuiwakilisha na kuihudumia nchi huku ughaibuni.

Friday, July 31, 2015

Tamasha la Afrifest ni Kesho, Agosti 1

Kesho ndio siku ya tamasha la Afrifest, mjini Brooklyn Park, Minnesota. Ni fursa ya watu kukutana, kujifinza kuhusu mambo mbali mbali ya historia, siasa na tamaduni za wa-Afrika na wanadiaspora wenye asili ya Afrika. Ni fursa ya kuuenzi mchango wa watu weusi katika dunia.

Afrifest inafuata nyayo za viongozi maarufu waliofanya juhudi katika kujenga mshikamano miongoni mwa watu wenye asili ya Afrika, mshikamno ulioendana na ajenda za kujitambua na kupigania uhuru na ukombozi.

Watu hao maarufu ni kama Henry Sylvester-Williams,  Marcus Garvey, George Padmore, W.E.B. DuBois,  Kwame Nkrumah, Jomo Kenyatta, Nnamdi Azikiwe, Julius Nyerere, Kenneth Kaunda na Walter Rodney.

Katika sanaa, tunawakumbuka watunzi na waandishi maarufu kama Antar bin Shaddad (Saudi Arabia), Alexander  Pushkin (Urusi), Claude McKay (Jamaica na U.S.A), Peter Abrahams (Afrika Kusini na Jamaica) na Leopold Sedar Sengor (Senegal). Tunawakumbuka wanamuziki kama Bob Marley (Jamaica) na Miriam Makeba (Afrika Kusini). Wanamitindo wa mavazi  nao huonesha ubunifu wa watu weusi.

Mbali na michezo ya watoto, kutakuwepo na mambo mengine kemkem, siku nzima, ya kuelimisha na kuburudisha. Bora kuja kujionea, kuliko kusimuliwa. Tamasha litafanyika kesho, tarehe 1 Agosti, Northview Junior High School, Brooklyn Park, Minnesota, kuanzia saa nne asubuhi hadi saa tatu usiku.

Monday, December 8, 2014

Vitabu Nilivyonunua Juzi

Juzi, Jumamosi,  nilienda Minneapolis, kuhudhuria mkutano wa bodi ya Afrifest Foundation, ambayo mimi ni mwenyekiti wake. Wakati wa kurudi, nilipitia Apple Valley, nikaingia katika duka la Half Price Books, ambalo nimeliongelea mara kadhaa katika blogu hii.

Ingawa ilikuwa jioni sana,  watu walikuwa wengi humo dukani: watu wazima, vijana, na watoto. Nami nilijichanganya nao, nikaangalia angalia sehemu zenye vitabu vya fasihi. Nilinunua vitabu vinne, ambavyo nitavielezea leo.

Lakini kabla ya kuelezea vitabu hivi, napenda kujikumbusha kitu kimoja kilichonigusa, wakati nimesimama katika foleni ya kulipia vitabu. Mbele yangu walikuwepo baba na mama na watoto wadogo wawili wasichana. Walikuwa wameshaweka vitabu vyao kwenye kaunta ya kulipia, huku wakiwaelezea wale watoto jinsi watakavyowasomea vitabu. Kati ya vile vitabu kwenye kaunta, niliviona viwili vikubwa vikubwa vya Harry Potter. Muda wote wale watoto walikuwa na furaha na msisimko. Kwa mara nyingine tena, nilishuhudia jinsi wenzetu wanavyowalea watoto wao katika utamaduni wa kupenda kusoma vitabu.

Kitabu kimojawapo nilichonunua ni Much Ado About Nothing, ambayo ni tamthilia ya Shakespeare iliyohaririwa na Barbara A. Mowat na Paul Werstine. Wasomaaji wa Shakespeare wanajua kuwa tamthilia zake zimehaririwa na wahariri mbali mbali katika hii miaka 500 tangu kufariki kwake.

Tamthilia za Shakespeare, ambazo ni 37, hupatikana pia zikiwa zimekusanywa katika kitabu kimoja kikubwa sana. Ingawa ninazo nakala za kitabu hiki--nakala mbili hapa Marekani na nyingine Tanzania--huwa napenda, mara moja moja kununua hivi vitabu vya tamthilia moja moja, kwa vile ni rahisi kubeba katika mkoba na kwenda navyo popote.

Kitabu kingine nilichonunua ni The Pickwick Papers, kilichotungwa na Charles Dickens. Wengi wetu tuliosoma sekondari miaka ya sitini na kitu na sabini na kitu tunamkumbuka Dickens na riwaya zake, kama vile Oliver Twist na A Tale of Two Cities. Binafsi, nilimpenda sana Dickens, na nilisoma vitabu vyake kadhaa. Nimewahi kumwongelea Dickens katika blogu hii.

Kitabu cha tatu nilichonunua ni Hemingway on Hunting. Nimenunua toleo lililochapishwa na The Lyons Press, mwaka 2001. Kitabu hiki ni mkusanyo wa maandishi ya Ernest Hemingway yanayohusu uwindaji. Mhariri wake ni Sean Hemingway, mjukuu wa mwandishi mwenyewe. Pia kuna utangulizi mfupi ulioandikwa na Patrick Hemingway, mtoto pekee wa Ernest Hemingway aliyebaki. Sean amekusanya maandishi kutoka katika vitabu  kama vile Green Hills of Africa, For Whom the Bell Tolls, Across the River and into the Trees, na pia makala na barua mbali mbali alizochapisha Ernest Hemingway katika magazeti.

Ingawa mengi ya maandishi hayo ninayo, niliona ni vema kuwa na kitabu hiki ambacho kinahusu hili suala la uwindaji. Ningependa kusema pia kuna kitabu cha aina hiyo hiyo, ambacho ni mkusanyo wa maandishi ya Hemingway kuhusu uvuvi, na kingine kuhusu uandishi. Hemingway, katika falsafa na nadharia zake, aliongelea uhusiano baina ya  uandishi na uwindaji.

Kitabu cha nne nilichonunua ni Minaret, riwaya iliyotungwa na Leila Aboulela, ambaye alikulia Khartoum na anaishi Dubai na Aberdeen. Ni mwandishi maarufu, ambaye ameshajitwalia tuzo kadhaa kwa uandishi wake. Ingawa nimesikia habari zake kwa miaka kadhaa, sikuwahi kusoma kitabu chake hata kimoja. Leila Aboulela anajulikana kwa umahiri wake kisanaa, pia kwa jinsi anayowaelezea suala la wanawake katika u-Islam kwa mtazamo tofauti na ilivyozoeleka. Nina dukuduku ya kusoma Minaret, kwa kuanzia, na nitapenda pia kusoma riwaya zake zingine.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...