Thursday, May 11, 2017

Shukrani kwa Msomaji

Msomaji mwingine wa kitabu cha Africans and Americans; Embracing Cultural Differences amejitokeza na kuandika maoni yake kuhusu kitabu hiki. Ameandika maneno matatu tu, "Short and sweet," katika mtandao wa Goodreads, ambao ni maarufu miongoni mwa wasoma vitabu. Humo wanaweka maoni yao kuhusu vitabu walivyosoma au vitabu wanavyopangia kusoma.

Kama ilivyo kawaida yangu katika blogu hii, ninamshukuru kwa kujipatia kitabu hiki, kukisoma, na kuwajuza walimwengu maoni yake. Amefanya hivyo kwa hiari yake, akijua kwamba kauli yake itasomwa na watu wengi. Namshukuru kwa hisani yake; amenifanyia kazi bila malipo wala kutegemea shukrani.

Maoni ya wasomaji yana manufaa makubwa. Kwanza yananiwezesha kufahamu kama ninafikisha ujumbe wangu na unaeleweka vipi. Kila msomaji anapotoa maoni, hutaja jambo fulani au mambo fulani yaliyomgusa kwa namna ya pekee. Wasomaji wanaweza kuwa wamekipenda kitabu hicho hicho, lakini kwa misingi au namna mbali mbali.

Pili, kuwepo kwa maoni ya wasomaji kunaniondolea jukumu la kukiongelea kitabu changu, kwa watu wanaokiulizia. Badala ya mimi kuwaelezea, ninawaelekeza watu wakasome maoni hayo, ambayo wasomaji wameyatoa kwa hiari yao, bila msukumo wa aina nyingine.

Siku nne zilizopita, kwa mfano, m-Tanzania moja aishiye Marekani, aliniandikia ujumbe binafsi katika Facebook akinielezea kuwa anatakiwa kuongea na waalimu kutoka Marekani katika kuwaandaa kwa safari ya Tanzania. Hiyo ni programu baina yao na walimu wa Tanzania kuhusu tamaduni na ufundishaji. Alihitaji pendekezo la kitabu kuhusu tamaduni.

Nilimtajia kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, na baadaye nimemshauri kuwa ili ajiridhishe, aangalie maoni ya wasomaji kwenye mtandao wa Amazon na pia mtandao wa Goodreads. Kuna sehemu zingine pia ambapo maoni yamechapishwa, kama vile blogu, tovuti, na majarida.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...