Showing posts with label Bemidji. Show all posts
Showing posts with label Bemidji. Show all posts

Monday, April 6, 2015

Bemidji Yamwenzi Mary, Mke wa Hemingway

Jioni ya tarehe 4 Aprili, baada ya kurejea kutoka Leech Lake Tribal College karibu na mji wa Bemidji, niliingia mtandaoni nikiwa na lengo la kuona kama kuna taarifa zozote kuhusu mkutano wetu. Katika ukurasa wa Facebook wa Chuo, niliona taarifa na picha za mkutano ule:

Hilo lilinivutia. Lakini niliona pia taarifa nyingine, kuhusu namna mji wa Bemidji unavyomwenzi Mary Welsh, aliyekuwa mke wa nne na wa mwisho wa Ernest Hemingway. Mary Welsh alizaliwa karibu na Bemidji akakulia na kusoma mjini hapo.

Kisha alienda kusoma katika Chuo Kikuu cha Northwestern karibu na Chicago. Alikuja kuwa mwandishi katika magazeti hapo Chicago na hatimaye London, akajipambanua kama mwandishi wa habari za vita. Huko ndiko alikokutana na Ernest Hemingway na baadaye wakafunga ndoa.

Nilifahamu hayo yote na mengine mengi, kutokana na utafiti wangu wa miaka kadhaa. Nilifahamu tangu zamani kuwa Mary Welsh alizaliwa eneo la Bemidji, na nilikuwa nawazia kwenda kule kufanya utafiti juu yake. Mary Welsh Hemingway alitanguzana na Ernest Hemingway katika safari ya Afrika Mashariki mwaka 1953-54. Walizunguka Kenya, Tanganyika, hadi Uganda, ambako walipata ajali mbili za ndege, mfululizo.

Mary Hemingway alisafiri hadi Mbeya, na ameelezea hayo na mengi mengine katika kitabu chake kiitwacho How it Was. Nasikitika kuwa wa-Tanzania, kwa kukosa utamaduni wa kununua na kusoma vitabu, hawafahamu hayo. Wangekuwa wana utamaduni huo, wangeweza kutumia habari na maandishi kama haya ya Mary Welsh Hemingway na Hemingway mwenyewe kwa manufaa makubwa, hasa katika utalii. Hali ni mbaya kwamba wa-Tanzania hawashtuki wakielezwa habari za vitabu namna hii. Nimethibitisha hayo, kama nilivyoandika katika blogu hii.

Wenzetu katika nchi kama Cuba, Hispania na Marekani wanafaidika sana na maandishi ya Hemingway. Cuba wanaitunza sana nyumba ya Hemingway, Finca Vigia, na hata baa alimokuwa anakunywa, mjini Havana, ni kivutio kikubwa cha watalii. Kule Hispania kuna mji wa Pamplona ambao ulipata umaarufu duniani na umaarufu huu unaendelea, baada ya Hemingway kuutembelea na kuangalia mchezo wa "bull fighting," akaandika juu yake katika riwaya iitwayo The Sun Also Rises. Maelfu ya watalii wanafurika Pamplona. Hapa Marekani, nyumba alimoishi Hemingway, kama vile kule Oak Park (Illinois)na Key West (Florida), ni vivutio vikubwa kwa watalii.

Hayo ndio yaliyonijia akilini wakati nasoma taarifa ya mji wa Bemidji kumwenzi Mary Welsh Hemingway. Jambo moja kubwa lililoelezwa katika taarifa ile ni utunzi wa tamthilia juu ya Mary Welsh Hemingway, unaofanywa na Catie Belleveau baada ya utafiti wa muda mrefu.

Hoja sio kwamba ni lazima nasi tujitose na kujishughulisha na Hemingway na mke wake, ingawa kufanya hivyo kungetuletea manufaa kama wanayopata wenzetu wa Cuba, Pamplona, Oak Park na Key West. Ninachotaka kusisitiza ni umuhimu wa kujifunza kutoka kwa hao wenzetu.

Sisi tunao waandishi maarufu kama Mgeni bin Faqihi wa Bagamoyo, aliyetunga Utenzi wa Ras il Ghuli. Je, tunajua habari zake? Tunaye Shaaban Robert. Je, ni wa-Tanzania wangapi wanajua angalau mahali alipozaliwa, sehemu alimoishi, na mahali alipozikwa? Je? wahusika katika wizara za utalii na utamaduni wanafahamu habari hizo? Na je, wanafahamu kuwa taarifa hizo ni hazina ambayo tungeweza kuitumi? Binafsi ninatekeleza wajibu wangu kwa kuandika kuhusu mambo haya, kama nilivyofanya katika kitabu cha CHANGAMOTO: Insha za Jamii, ambacho nitashangaa kikipata wasomaji Tanzania.

Thursday, April 2, 2015

Nimewasili Bemidji, Minnesota

Alasiri hii, nimewasili mjini Bemidji, nikiwa njiani na wenzangu watatu, ambao tumesafiri pamoja kutoka Minneapolis. Tutalala hapa, na kesho asubuhi tunakwenda Leech Lake Tribal College kwenye mkutano  kuhusu "Narratives of Identity." Mimi ni mmoja wa watoa mada wanne. Mada yangu itakuwa "Being African in America."

Tulipokuwa tunakuja, tulisimama kidogo katika mji uitwao Akeley, ili kuona sanamu ya Paul Bunyan, mhusika maarufu katika masimulizi ya jadi ya sehemu hii ya Minnesota, ambaye anajulikana sana pia Marekani na ulimwenguni. Sanamu hii inamwonyesha akiwa ameshika shoka lake. Ili kujionea jinsi sanamu hii ilivyo kubwa, ifananishe na sisi watatu ambao tumesimama hapo Mbele yake.


Tulipoingia Bemidji, tulikwenda moja kwa moja kwenye sanamu nyingine ya Paul Bunyan, ambayo inamwonyesha akiwa na fahali wake wa buluu ambaye ni sehemu muhimu ya masimulizi kuhusu mhusika huyu. Sanamu hiyo, sawa na ile ya Akeley, ni kubwa sana.

Kwa mujibu ya masimulizi, Paul Bunyan alikuwa jitu kubwa la ajabu, nadhani kumzidi hata Liongo Fumo, shujaa katika masimulizi ya jadi ya wa-Swahili, wa-Pokomo, na wengine katika mwambao wa Kenya.

Bemidji ni mahali ambapo niliwahi kufika miaka mitatu hivi iliyopita, lakini tangu muda mrefu kabla ya hapo nimetamani kuja kwa shughuli za utafiti wangu juu ya mwandishi Ernest Hemingway.

Mary Welsh, mke wa nne na wa mwisho wa Ernest Hemingway alizaliwa na kukulia eneo hili la Bemidji, kabla hajaenda kusoma katika Chuo Kikuu cha Northwestern, karibu na Chicago. Katika safari zake Kenya, Tanganyika, na Uganda, mwaka 1953-54, Hemingway alitanguzana na mke wake huyu.

Panapo majaliwa, nitakuja Bemidji kufanya utafiti huo. Kwa leo nimefurahi kuziona hizi sanamu, na kujionea jinsi Paul Bunyan alivyo maarufu eneo hili. Jina lake liko kila mahali. Nimeona mtaa wenye jina hilo, biashara mbali mbali, hata kampuni ya mawasiliano ya intanenti.

Hata katika hoteli tunamolala usiku huu, Hampton Inn, nimeona picha kubwa ya Paul Bunyan katika ukuta wa mgahawa. Kwangu mimi kama mtafiti wa masimulizi na mambo mingine ya jadi ("folklore"), nimeguswa sana na kupata hamasa ya kufanya utafiti juu ya Paul Bunyan.


Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...