Showing posts with label East China Normal University. Show all posts
Showing posts with label East China Normal University. Show all posts

Thursday, April 21, 2011

Ziara Yangu Shanghai

Mwaka 2003 nilipata bahati ya kutembelea China. Hii ni kati ya ziara ambazo nazikumbuka sana. Nilialikwa kwenda kutoa mihadhara East China Normal University, mjini Shanghai.



Mihadhara ilikuwa kama ifuatavyo:

25 Novemba, "My Folklore Research Experience,"
25 Novemba "American Folklore Studies Today,"
26 Novemba, "My Folklore Research Experience"
1 Desemba, "African Folklore Research."

Picha zinazoonekana hapa ni za wanafunzi wa shahada ya juu. Mwalimu wao, ambaye amevaa jaketi jekundu, alinialika niongee na hao wanafunzi darasani kwao kuhusu "My Folklore Research Experience" na vile vile "Women in African Folklore" hiyo tarehe 26Novemba.

Nilifurahi kupata fursa hii ya kubadilishana mawazo na watafiti wa China. Walikuwa na masuali mengi. Huyu bwana aliyesimama pembeni alikuwa katika ngazi ya juu kuliko hao wanafunzi wengine. Wao walikuwa wanasomea shahada ya uzamili, wakati yeye alikuwa katika shahada ya udaktari. Alivyokuwa na masuali mengi magumu na niliongea naye muda mrefu.

Tarehe 27 Novemba, wenyeji wangu, wakiongozwa na huyu mwalimu mwenye jaketi jekundu, walinitembeza hadi kwenye mji wa Suzhou, ambao ni maarufu kwa historia na utalii. Tulifikia Sheraton Suzhou. Kuna vivutio vingi vya utalii Suzhou, kama vile bustani za kale.

Tarehe I Desemba alifika hapo Chuoni mwandishi wa gazeti la "Oriental Morning Post," akiwa na mpiga picha Zhang Dong, akanifanyia mahojiano ya saa nzima kuhusu utafiti wa Folklore, fasihi, na uhusiano baina ya taaluma hizo. Baada ya mahojiano hayo, walihudhuria mhadhara wangu kuhusu "African Folklore Research." Kisha tukafanya tena mahojiano ya saa nzima na nusu. Mwandishi huyu alikuwa makini kwa masuali na nakumbuka aliniulizia hata kuhusu mwandishi J.M. Coetzee wa Afrika Kusini, ambaye alikuwa amepata tuzo ya Nobel wiki chache tu zilizotangulia, mwanzoni mwa mwezi Oktoba. J.M. Coetzee amehamia Australia.

Fursa ya kutembelea China ilikuwa ni jambo la pekee sana kwangu, kutokana na historia ya urafiki baina ya Tanzania na China. Nami nilianza mihadhara yangu yote kwa kukumbushia urafiki huo, ambao ulianza miaka ya mwanzo baada ya Uhuru wa Tanganyika.

Wakati naandaa safari ya China, nilipewa jina la Mchina ambaye anaifahamu Tanzania na Zambia. Aliyenipa jina hili ni profesa katika Chuo cha St. Olaf ambapo nafundisha. Ni profesa wa lugha na fasihi ya China, ambaye ana uzoefu sana na China. Alinielezea habari za huyu Mchina, kuwa alikuwepo Tanzania miaka ile ya ujenzi wa reli baina ya Tanzania na Zambia.

Nilipelekwa nyumbani kwake mjini Shanghai na tuliongea sana. Alikuwa na vinyago vya ki-Makonde nyumbani mwake, na vitu vingine vya aina hiyo. Ni mtu ambaye anaisifu Tanzania na Zambia kwa mambo mengi. Kwa kifupi, ziara yangu ilikuwa nzuri sana, na nitakumbuka daima ukarimu wa wenyeji wangu.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...