
Tulizungumza na kushauriana mambo ya manufaa kuhusu elimu na kadhalika, nao walinialika kutembelea shule yao. Haya ndio mambo tunayohitaji katika nchi yetu. Na hao watoto katika picha wanasikia tunachoongea sisi watu wazima. Tuwaleavyo ndivyo wakuavyo.
Ninapowakumbuka na kuwaangalia watoto, kama hao waliomo katika picha, hisia zangu za kiualimu zinaibuka. Kwa upande mmoja, nafurahi na kushukuru kuwa nimejaliwa uwezo na fursa ya kuwaelimisha watoto hao. Ninawapenda. Soma, kwa mfano, makala yangu hii hapa.
Papo hapo, ninapowawazia watoto wa Taifa letu, najiwa na wasi wasi kwa jinsi baadhi ya watu wanavyoeneza mitazamo na mawazo kama udini, ubaguzi na uhasama baina ya makundi mbali mbali ya jamii. Hizo ni sumu, nami nahofia athari zake kwa watoto wetu.
Ualimu ni wito, nami nilisikia wito huu wakati nikiwa bado mdogo, sijaanza hata shule. Ni wito wa kuwa mtafuta elimu muda wote, wito wa kuwalea wanafunzi wawe wanaothamini na kutafuta elimu; wawe watu wema kwa mujibu wa maadili ya jamii yao. Elimu haina mwisho. Mimi ni mwalimu wa madarasa ya chuo kikuu, kuanzia mwaka 1976, lakini ningefurahi kama ningekuwa pia na utaalam wa kuweza kufundisha shule ya msingi. Nimeelezea hayo katika kitabu cha CHANGAMOTO.