
Tarehe 29 Agosti niliendesha warsha Tanga, Tanzania, mada ikiwa ni "Utamaduni, Utandawazi na Maendeleo". Warsha hii ilifanyika katika kituo kiitwacho Meeting Point Tanga na ilidumu kuanzia saa nne asubuhi hadi saa kumi na moja jioni. Hapo juu anaonekana Mama Ruth Nesje, mkurugenzi wa kituo, akinitambulisha kwa washiriki wa warsha.
Niliamua kufanya warsha hii kutokana na uzoefu wangu wa kuelezea masuala haya ya utamaduni kwenye vyuo, taasisi, makampuni, makanisa, jumuia mbali mbali na watu binafsi huko Marekani. Warsha hii ilikuwa na mvuto mkubwa kwa washiriki na iliamuliwa kuwa zifanyike warsha hizi siku zijazo. Kitu kimoja kilicholeta msisimko na mjadala mkubwa ni makala yangu "Maendeleo ni Nini?"
Ninapangia kuandika zaidi kuhusu warsha hii, na nyingine ambayo niliendesha Dar es Salaam tarehe 5 Septemba, ila nimeona niweke hii taarifa fupi hapa, kwa sasa. Kama kianzio, nimeweka picha chache zilizopigwa siku hiyo.



