Friday, January 15, 2010

Kitabu Kuhusu Mlima Kilimanjaro

Asubuhi ya leo, nikiwa nazunguka katika duka la vitabu hapa chuoni St. Olaf, niliona kitabu kipya kuhusu Mlima Kilimanjaro. Nilikichukua na kuanza kukisoma. Ni kitabu chenye maelezo yalioyoandikwa na Michael Moushabeck na picha zilizopigwa na Hiltrud Schulz.

Mwanzoni mwa kitabu, Moushabeck anasema kuwa wazo la kitabu hiki alilipata wakati anahudhuria tamasha la vitabu London. Pale alikutana na mwandishi ambaye alikuwa ana mswada wa kitabu kuhusu Kilimanjaro. Waliongea, na Moushabeck akaamua kusafiri kuja Tanzania.

Kitabu hiki ni rekodi ya safari hiyo, kwa maneno na picha. Moushabeck anasema kuwa alijiandaa kwa kusoma sana kuhusu Mlima Kilimanjaro na mambo mengine, kabla na wakati wa safari ya kuja Tanzania. Na katika kitabu hiki anatumegea mawili matatu aliyoyapata katika kusoma huko. Kwa mfano, amemnukuu Ernest Hemingway, yule mwandishi maarufu, alivyouelezea Mlima Kilimanjaro. Amewanukuu waandishi maarufu kama T.S. Eliot, Marianne Moore, na kadhalika. Kitabu hiki kinavutia, kwa maelezo yake mazuri na picha.

Kama ilivyo kawaida yangu, nilipokuwa nakisoma, nilishindwa kujizuia kuwazia uzembe wa wa-Tanzania. Jambo hili nimelilalamikia na nitaendelea kulilalamikia. Wa-Tanzania hawaonekani kwenye matamasha ya vitabu. Sasa je, akili wanayoipata wenzetu kwenye shughuli kama hizi wa-Tanzania wataipata? Wa-Tanzania hawana utamaduni wa kusoma vitabu. Je, wataweza kuitangaza nchi yao kwa ufanisi? Hazina kama Mlima Kilimanjaro imo nchini mwetu. Lakini wanaoitangaza na kufaidika zaidi na hazina hii ni wageni, wakati sisi tunashinda vijiweni tukiilalamikia serikali kwa kukosa sera.

Je, tunahitaji sera ili tununue kitabu na kukisoma? Tutajuaje dunia inavyokwenda? Ni wazi kuwa, katika mchakato wa maendeleo ya dunia, wa-Tanzania watakuwa wasindikizaji. Ni wazi kuwa wameamua hivyo, na wameridhika. Nimeelezea sana matatizo ya wa-Tanzania katika kitabu changu kipya, CHANGAMOTO.

2 comments:

Bennet said...

Sio mlima kilimanjaro tu bali hata vitu vingine vya kitalii, mbuga kama serengeti wakenya wanaitangaza kwa kutumia mgongo wa maasai mara

Halil Mnzava said...

Ni kweli utamaduni wa kusoma vitabu hatuna.
Kiasi tunabadilika na tutaanza kutoa hamasa.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...