Sunday, January 31, 2010

Nimefika Chuoni Augustana

Jana nilifika chuoni Augustana, Illinois, kutoa mihadhara. Jana jioni niliongea na walimu wachache kuhusu masuala ya utamaduni na utandawazi katika dunia ya leo na umuhimu wa kuwaandaa wanafunzi wetu ipasavyo. Leo nimepata fursa ya kuongea na wanafunzi wapatao 40, ambao wanaenda Ghana na Senegal kwa masomo.Nimekuja hapa chuoni Augustana kusaidia kukuza mpango wa masomo kuhusu Afrika. Profesa John Tawiah Boateng, kutoka Ghana, aliyesimama nami hapa juu, kulia, ni mmoja wa wahusika wa mpango huu, chini ya mratibu wa masomo yahusuyo nchi za nje katika chuo cha Augustana, Dr. Kim Tunicliff. Hapa chini wanaonekana wote wawili, Dr. Tawiah Boateng akiwa katika kunitambulisha kwa waliohudhuria.
Dr Tunicliff tulifahamiana miaka iliyopita, alipokuwa makamu rais wa jumuia ya vyuo vinavyoshirikiana katika eneo la Marekani ya Kati, Associated Colleges of the Midwest (ACM). Nilikuwa mwanabodi katika bodi ya uongozi wa jumuia ya vyuo hivi, nikiwa mshauri wa mipango ihusuyo ushirikiano kati ya vyuo hivi na Zimbabwe na Tanzania. Ingawa yeye alishaondoka ACM, mimi bado ni mwanabodi. Ni wakati huo wa uongozi wa Dr. Tunicliff ndipo nilipohamasika kuandika kitabu cha Africans and Americans, ili kuchangia suala la kuwaandaa wanafunzi waendao Afrika. Hayo nimetaja katika utangulizi wa kitabu.. Katika kunitambulisha, Dr. Tawiah Boateng aliongelea mengi kuhusu shughuli zangu za utafiti na ufundishaji na pia shughuli za kuendeleza mipango ya kuwapeleka wanafunzi Afrika. Yeye, sawa na Dr. Tunicliff wanakipenda kitabu changu na wanakitumia katika matayarisho ya wanafunzi waendao Afrika. Nilitumia muda wa saa moja na nusu kuongelea masuala mbali mbali ya kuwatayarisha wanafunzi hao kwa safari yao ya Ghana na Senegal. Nilisema kuwa kuishi katika utamaduni tofauti na wetu ni changamoto inayotuelimisha kuhusu mapungufu yetu na pia kutupa fursa ya kuwaelimisha wengine. Mapungufu hayo ni pamoja na tabia ya kudhani kuwa tunavyofanya katika utamaduni wetu ni sahihi, na watu wa utamaduni tofauti wanahitaji kurekebishwa. Huo ni mtego unaotukabili sote. Katika kuandika kuhusu utamaduni wa wengine kazi kubwa ni ya kujisafisha roho ili tuweze kuandika kwa kutumia misingi ya kila utamaduni, badala ya kutumia misingi ya utamaduni wetu kama kigezo cha ubora. Baada ya mhadhara wangu na masuali, tulitawanyika, tukaenda kupata chakula cha jioni.

Kwa mwandishi yeyote ni faraja kuona maandishi yake yanasomwa kwa makini. Nami nilifurahi kuona kuwa wote waliohudhuria walikuwa wamesoma kitabu changu. Masuali waliyouliza yalionyesha kuwa wamefuatilia kwa makini yale niliyoandika. Baada ya yote, baadhi ya wanafunzi waliendelea kuongea nami, na niliombwa kuweka sahihi kwenye nakala za vitabu vyao, kisha tukapiga hii picha ya mwisho.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...