Sunday, December 17, 2017

Tumetoka Darasani

Picha hii ilipigwa tarehe 29 Novemba. Niko na wanafunzi wangu, tukiwa tumetoka darasani. katika somo la "First Year Writing." Hili ni somo la uandishi bora wa ki-Ingereza. Ninalipenda somo hili kama ninavyoyapenda masomo yangu mengine. Darasa letu lina wanafunzi 19.

Baada ya kumaliza kipindi tulitawanyika, lakini dakika chache baadaye nilikutana na hao wawili katika jengo la Buntrock Commons karibu na maktaba, tukapiga picha. Huyu wa katikati anatoka Norway, na huyu mwenzake ni wa hapa Marekani.

Nina bahati na ninafurahi kuwa mwalimu, kushughulika na wanafunzi na vitabu muda wote. Ni kazi ambayo niliitamani tangu nilipokuwa kijana mdogo. Nilipofundishwa ualimu katika chuo kikuu cha Dar es Salaam, ambapo nilisomea Literature, English, na Education, nilifundishwa kuwa mwalimu anashika nafasi ya wazazi, in loco parentis, kwa ki-Latini. Ninawaona wanafunzi kama watoto wangu.

Ninachukulia jukumu langu la kuwaelimisha na kuwalea wanafunzi kwa dhati. Tangu nilipoanza kufundisha, chuo kikuu cha Dar es Salaam, mwaka 1973, nimezingatia wajibu na maadili ya ualimu, ambayo ni kujielimisha kwa bidii, kufundisha kwa uwezo wangu wote, na kuwatendea haki wnafunzi wote bila upendeleo.

Ninafurahi kufundisha hapa chuoni St. Olaf. Walimu wanachapa kazi na uongozi wa chuo unawaheshimu. Wanafunzi wanajua wajibu wao. Wana heshima, na ni wasikivu, wenye dukuduku ya kuhoji na kujua mambo. Ninawapenda. Pamoja na kuwafundisha kwa moyo wote, ninapenda kuwatania. Popote tunapokutana, tunafurahi kama inavyoonekana pichani.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...