Saturday, March 9, 2019

Kitabu Kinatumika Chuo Kikuu China

Tarehe 7 Februari, wakati namalizia maandalizi ya warsha kuhusu Culture and Globalization, niliyofanya Dar es Salaam, nilipata taarifa ya kufurahisha kutoka kwa kijana mTanzania asomaye China. Kijana huyu, Seleman Pharles Mabala, aliniambia kuwa siku moja profesa wao mChina aliwaambia wasome kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differenceskatika kozi ya "Cultural Differences and Cross-cultural Communication." Chuo hicho kiitwacho University of Electronic Science and Technology, kiko katika mji wa Chengdu, katika jimbo la Sichuan.
 Aliniambia kuwa alifurahi sana kumsikia profesa akisema kuwa kitabu kimeandikwa na mTanzania. Alipiga picha kama kumbukumbu akawapelekea marafiki nyumbani. Kijana aliendelea kuniambia: "Nakupa hongera sana na mimi hii kwa njia moja ama nyingine imenitia nguvu ya kuendelea kusoma kwa bidii nifikie angalau nusu yako!"

Ninafurahi kuwa nimeweza kumtia kijana huyu hamasa ya kusoma kwa bidii. Kwangu kama mwalimu, haya ni mafanikio mazuri. Jambo mojawapo lililotamkwa katika "Azimio la Arusha" kuhusu mapinduzi yaliyokusudiwa Tanzania ni kwamba kazi iwe jambo la kujivunia. Nami najivunia kazi yangu.

Vitabu vyangu kutumiwa katika vyuo vikuu si jambo geni kwangu. Vinatumiwa katika vyuo vya Marekani mara kwa mara. Lakini hii ni mara yangu ya kwanza kufahamu kuwa kitabu changu kinatumika China. Nimefurahi.


Ninamshukuru Seleman kwa kuniletea taarifa hii na kuniruhusu kuichapisha.

4 comments:

Unknown said...

Heshima kwako professor

Mbele said...

Shukrani kwa ujumbe wako. Pamoja na kufurahia taarifa hizi za ughaibuni, natamani jamii nchini mwangu izinduke na kuanza kutafakari masuala haya ya athari za tofauti za tamaduni katika ulimwengu wa utandawazi wa leo.

tzman said...

kitabu chako kinapatikana wapi

Joseph said...

Ndugu Raman, kitabu hiki kinapatikana patika duka la Kimahama Literature Center (Arusha) na duka liitwalo A Novel Idea lililopo Slipway, Msasani. Vile vile kinapatikana mtandaoni.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...