Tangu ninunue kifaa hiki, yapata wiki mbili zilizopita, nimekuwa katika kujifunza namna ya kukitumia, maana kina mambo mengi sana. Angalau naweza kutembelea mitandao, kutuma na kupokea barua pepe, na kupiga picha na kisha kuziangalia. Hata video najua namna ya kupiga.
Kitu ninachotaka kukifanya hima ni kuingiza vitabu pepe kwenye hii iPad, nikianzia na kitabu changu kiitwacho Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, ambacho wadau wanakipata mtandaoni, pamoja na vitabu vyangu vingine, kwa njia hiyo.Kidogo najisikia vibaya kwamba nilikiweka kitabu hiki katika muundo wa kitabu pepe na wadau wanakinunua, wakati mimi mwenyewe sikuwa na kifaa cha kuingizia vitabu pepe wala sikuwahi hata kuona kinakuwaje katika umbo la kitabu pepe. Nimejisikia kama mpishi ambaye anawapikia wengine lakini yeye mwenyewe hata kuonja haonji. Sasa, na hii iPad yangu, ngoja nikae mkao wa kula, kwa vitabu vyangu na vya wengine.