Monday, September 10, 2018

Mdau Wangu Mpya

Juzi, tarehe 8, nilikwenda Coon Rapids, Minnesota, kuhudhuria uzinduzi wa jarida liitwalo L Magazine. Jarida hilo linalohusu zaidi masuala ya uandishi, uchapishaji, na uuzaji wa vitabu, limeanzishwa na Bi Bukola Oriola mwenye asili ya Nigeria anayeishi hapa Minnesota.

Kati ya watu waliohudhuria ni Dr. Artika Tyner, rafiki wa karibu wa Bi Oriola. Dr. Tyner ni "Vice President for Diversity and Inclusion" wa Chuo Kikuu cha St. Thomas. Anaonekana pichani akiwa ameshika tuzo alizopewa hiyo juzi kwa mchango wake kwa jamii.

Alipotambulishwa kwangu kwenye meza nilipoweka vitabu vyangu, tuliongea kiasi kuhusu shughuli zake na zangu. Alinunua vitabu vyangu, zikiwemo nakala 9 za Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Vile vile alielezea hamu yake ya kuendelea kuwasiliana nami ili tutafakari namna ya kushirikiana katika programu zinazohusu Afrika na watu wenye asili ya Afrika yaani wanadiaspora.

Nilitambua kuwa Dr. Tyner ni mmoja wa waMarekani Weusi ambao wana mapenzi ya dhati na Afrika. Hata mavazi yake yanaashiria hivyo. Ametembelea Afrika na anahamasisha programu za kupeleka watu Afrika. Dr. Tyner ni mtu maarufu, na kwa upande wangu kigezo kimoja ni kwamba ameshatoa mhadhara wa TED kuhusu elimu na mabadiliko ya jamii.


Ninafurahi kumpata mdau huyu mpya. Ninategemea kuendelea kubadilishana naye mawazo na uzoefu na kufanya shughuli mbali mbali za kuelimisha.

Thursday, August 30, 2018

Vitabu Nilivyonunua Nairobi

Nilisafiri tarehe 15 Julai kwenda Tanzania. Nilishukia Nairobi, kwa shughuli binafsi, ikiwemo kununua vitabu vya ki-Swahili. Kitabu nilichotamani zaidi ni Sauti ya Dhiki cha Abdilatif Abdalla ambacho nilitaka kukisoma kwa makini kuliko nilivyowahi kufanya kabla. Ninawazia pia kutafsiri kwa ki-Ingereza baadhi ya mashairi.

Nilivyoingia tu katika duka la vitabu la Textbbook Center, Kijabe Street, nilikitafuta kitabu cha Sauti ya Dhiki. Nilikiona, kikiwa na jalada tofauti na lile la mwaka 1973. Nilinunua pia Kichwamaji, Kaptula la Marx, Mzingile, na Dhifa, vya Euphrace Kezilahabi; Mashetani, tamthilia ya Ebrahim Hussein, na Haini, cha Adam Shafi.

Tangu zamani, nimekuwa na baadhi ya vitabu vya Kezilahabi, Ebrahim Hussein, na Adam Shafi. Ninafurahi kujipatia vile ambavyo sikuwa navyo. Hata hivi, nimegundua kuwa sasa nina nakala mbili za Mashetani na mbili za Kichwamaji.

Sunday, June 24, 2018

Maongezi ya Kina Leo na Msomaji Wangu

Leo nimekuwa na maongezi ya kina na msomaji wangu, mchungaji ambaye nilishamtaja katika blogu hii. Tulikutana mjini Hastings, Minnesota, tukaongeaa kwa saa mbili na robo. Tulikuwa tumeahidiana kwamba nikasaini nakala ya kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, ambacho mchungaji alikuwa anampelekea mtu fulani wa karibu.

Tuliongea sana kuhusu shughuli zetu za kuelimisha na kuhamasisha jamii ya watu weusi juu ya masuala ya kujitambua. Mchungaji ameendelea kunifahamisha kuwa kitabu changu kinamsaidia kujitambua kama mtu mwenye asili ya Afrika, ingawa ana pia asili ya ki-Cherokee na ki-Faransa. Anataka kitabu hiki kitumike kuwaelimisha vijana wa-Marekani Weusi, waweze kujitambua na kujivunia walivyo na silika za u-Afrika, ili wasiwe wanabezwa na wazungu.

Nami naelewa vizuri tatizo lilivyo kwa hao vijana. Wanashinikizwa kubadili mwenendo, lugha, na mambo yao mengine, ili wafuate ya wazungu. Mashuleni wanashinikizwa, kudhibitiwa, na kuadhibiwa kwa mienendo yao ambayo mamlaka zinaitafsiri kama utovu wa nidhamu.

Jukumu lililopo, ili pawe na suluhu, ni kwa walimu na viongozi wa shule kufanya juhudi ya kujielimisha kuhusu utamaduni wa wa-Marekani Weusi ambao misingi yake kwa kiasi fulani, au kwa kiasi kikubwa, ni u-Afrika. Wa-Afrika walivyoletwa utumwani huku Marekani, walikuja na tamaduni zao, ambazo zimerithishwa tangu kizazi hadi kizazi, ingawaje zimekuwa zikiathirika na mabadiliko na mazingira kutoka kizazi hadi kizazi.

Hata hivyo, baadhi ya misingi na vipengele vya u-Afrika vimeendelea kuwepo. Kwa mfano, wa-Afrika tuna namna yetu ya kuongea, kama nilivyoelezea katika kitabu changu, hasa kurasa 32-39 na 44-45. Na nimeelezea kitabuni kwamba ninapokutana na wa-Marekani Weusi, ninatambua vipengele hivi vya u-Afrika katika tabia na mienendo yao.

Ninashukuru kufahamiana na mchungaji huyu ambaye ana tafakari za kina kuhusu masuala na ana ukarimu moyoni mwake wa kunielezea anavyojisikia na anavyowazia kuhusu ujumbe wowote uliomo katika kitabu changu. 

Friday, June 22, 2018

Nimehudhuria Mhadhara Kuhusu Frantz Fanon

Jioni hii nilikuwa St. Paul kuhudhuria mhadhara juu ya Frantz Fanon uliotolewa na Dr. Moustapha Diop. Mhadhara uliandaliwa na Nu Skool, jumuia ya wa-Marekani Weusi ambayo nimewahi kuiongelea katika blogu hii.

Niliona ni lazima nikahudhurie mhadhara huu, ambao mada yake ilikuwa "Becoming Fanon: A Portrait of the Decolonized" kwa kuzingatia umuhimu wa fikra za Fanon katika harakati za ukombozi sehemu mbali mbali za dunia, hasa ukombozi wa fikra.

Nilikutana  na fikra za Fanon kwa mara ya kwanza nilipokuwa mwanafunzi chuo kikuu cha Dar es Salaam, katika idara ya Literature, miaka ya 1973-76. Aliyetufundisha ni mwalimu Grant Kamenju, na vitabu vya Fanon alivyotumia ni The Wretched of the Earth na Black Skin White Masks. Katika kufundisha fasihi ya Afrika, ninaona umuhimu wa kurejea katika fikra za Fanon mara kwa mara. Sielewi utakosaje kurejea kwenye fikra za Fanon.

Katika mhadhara wake, Dr. Diop alielezea kifupi maisha ya Fanon, akajikita zaidi katika kufafanua jinsi baina ya mwaka 1956 hadi 1961 Fanon alivyobadilika na kuwa Fanon tunayemjua kama mwanamapinduzi. Fanon alikuja kuwa mwanaharakati hadi akafukuzwa nchini Algeria. Alikwenda Tunisia, ndipo alipoendesha harakati, ikiwemo kuwapiga msasa wapiganaji wazalendo wa Algeria kabla hawajaingia nchini mwao kupambana na jeshi la wakoloni.

Jambo jingine ambalo nimejifunza katika mhadhara huu ni kuwa The Wretched of the Earth hakukiandika, kutokana na hali ya afya yake, bali alimwelezea mke wake kwa mdomo, naye akaandika. Ilichukua miezi kadhaa. Dr. Diop alitoa muhtasari wa mambo muhimu aliyotufundisha Fanon na akawataja watu walioendeleza fikra  za Fanon Afrika na Marekani, wakiwemo Kwame Nkrumah na Steve Biko.

Tuesday, June 19, 2018

Vitabu Vinapobebana

Nadhani kila msomaji wa vitabu anatambua manufaa na raha ya kusoma vitabu vya aina mbali mbali. Hivi ninavyoandika, ninakaribia kumaliza kusoma Riding the Waves of Culture: Understanding Diversity in Global Business, kitabu ambacho nilikitaja siku kadhaa katika blogu hii.

Nimekifurahia sana kitabu hiki, kwa jinsi kinavyoongelea masuala ya tofauti za tamaduni, mada ambayo ninashughulika nayo sana. Kinanifanya nielewe undani wa yale niliyoandika katika Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Kwa mfano, sura ya kitabu hiki iitwayo "How We Manage Time," imenipa msamiati wa kuelezea yale niliyoelezea katika sura iitwayo "Time Flies But Not in Africa." Nimeelewa kwamba msimamo wetu wa-Afrika ni "synchronic" au "polychronic" na msimamo wa wa-Marekani ni "sequential." Tofauti zetu ambazo nimezielezea katika kitabu changu zimejengeka katika mitazamo hiyo miwili.

Nitoe mfano. Kama ninavyoeleza katika kitabu changu, sisi tunaonekana hatuna nidhamu ya kuchunga muda, katika mazingira yetu, wakati wa-Marekani wanachunga sana muda, katika mazingira yao. Hizi ni tofauti tu, wala si ishara kwamba utamaduni moja ni bora kuliko mwingine. Kila utamaduni una mantiki yake.

Dhana zilizomo katika Riding the Waves of Culture zimenipa mianya ya kufafanua yale niliyoandika katika kitabu changu. Tofauti kubwa kati ya vitabu hivi viiili ni kuwa Riding the Waves of Culture kimeandikwa kitaaluma na ni kikubwa, wakati Africans and Americans: Embracing Cultural Differences kimeandikwa kiwe rahisi kusomwa na yeyote na ni kifupi sana.

Thursday, June 14, 2018

Mwalimu Mwingine Aongelea Kitabu Changu

Ni jadi yangu kuwatambua wasomaji wanaosema neno kuhusu vitabu vyangu. Ni namna ya kuwashukuru kwa kutumia muda wao kukisoma kitabu na kutumia tena muda kuandika maoni yao. Ninatambua kwamba wanafanya hivyo kwa hiari, na wangeweza kutumia muda wao kwa namna nyingine. Ninawashukuru.

Wiki hii amejitokeza mwalimu Khalid Kitito, ambaye amekitumia kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences katika ufundishaji wake hapa Marekani, akaandka maoni kwenye mtandao wa PublicReputation:

Africans and Americans written by Joseph Mbele is an excellent book to read about cultural differences between Americans and Africans. He examined the deep culture and not surface culture. It brings out clearly the understanding as to why Americans and Africans have different perspective of time, relationships, work, family, love, respect among others. I used it to teach in my Culture and Identity Class and found it useful. The book provided a forum for insightful discussions and at the end of the course students were able to view other cultures as different and not weird. It is also easy to read and understand, thus suitable for general readers.

Napenda kugusia tathmini yake kuwa ninaibua "deep culture." Wanataaluma wa tamaduni wanasisitiza suala hili la "deep culture." Tunapokutana na utamaduni wowote, tunaona mambo mengi, lakini ili kuyaelewa yale tunayoyaona, tunatakiwa kuelewa msingi wake. Hii ndio "deep culture." Inachukua muda sana kuuelewa utamaduni kwa maana hiyo. Ndivyo ilivyokuwa kwangu, katika kutafakari utamaduni wa wa-Marekani. Ilinichukua miaka karibu ishirini ya kuishi na wa-Marekani kabla sijathubutu kuandika kitabu changu. Kwa upande mwingine, kwa kuwa mimi ni mtafiti na mwalimu wa fasihi na "folklore" na ni mw-Afrika, haikuwa shida kwangu kuelezea "deep culture" kwa upande wa wa-Afrika.

Pamoja na kumshukuru mwalimu Kitito, kwa kuandika maoni yake, ninatoa mwaliko kwa yeyote mwingine aliyesoma au kutumia kitabu changu chochote kuandika maoni yake katika ukurasa huu wa PublicReputation.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...