Tuesday, August 26, 2014

Tamasha la Tamaduni Faribault, Minnesota, Agosti 23



Tamasha la tamaduni za kimataifa lilifanyika mjini Faribault tarehe 23 mwezi huu, kama ilivyopangwa. Nilihudhuria. Kati ya mambo yaliyonivutia ni bendera za nchi mbali mbali. Mwanzoni bendera hizi zilikuwa kwenye jukwaa kuu. Washiriki wa tamasha ambao nchi zao ziliwakilishwa na bendera hizi walikuja kwenye jukwaa kuu, wakasema machache kuhusu bendera hizi na nchi zao.







Baada ya hapo, waliandamana katika mstari mmoja wakiwa na bendera zao, kisha bendera zilisimikwa uwanjani, ambapo zilipepea muda wote wa tamasha.

Kama nilivyosema katika blog hii, kabla ya siku ya tamasha, sikuwa na bendera ya Tanzania. Kwa hivi, sikushiriki shughuli hii ya bendera.








Yalikuwepo mabanda mengi ambamo vitu mbali mbali vilikuwa vinauzwa, kama vile vyakula, maji ya kunywa, soda, nguo, vipodozi na vitu kadha wa kadha vya urembo.

















Vilikuwepo pia vikundi vya burudani, vikiwakilisha tamaduni mbali mbali.






























Nilipata fursa ya kukutana na kuongea na watu ambao hatukuwa tunafahamiana kabla. Hapa kushoto, naonekana na mama kutoka Ireland, ambaye yuko kulia kabisa, akifuatiwa na bwana mmoja kutoka Somalia, na huyu mama mwenye nguo nyeusi ni m-Marekani. Tulipiga picha hii baada ya wote watatu kununua vitabu vyangu.










Akina mama wanaoonekana pichani hapo juu wako tena hapa kushoto, na bwana mmoja kutoka Nigeria. Tuliongea sana kuhusu masuala ya tofauti za tamaduni, na mazungumzo yalikuwa ya kufikirisha na kutajirisha akili, hasa ukizingatia kuwa tulikuwa watu wa kutoka nchi mbali mbali kabisa.





Hapa naonekana na msichana mmoja kutoka Sudan. Aliniambia kuwa ananifahamu tangu miaka kadhaa iliyopita, alipokuwa mdogo.













Baadhi ya watu wanaonunua vitabu huomba kusainiwa vitabu hivyo. Shughuli hii ina maana ya pekee kwa mteja na mwandishi pia, kama tunavyojaribu kuelezea katika maongezi baina ya mwanablogu na msomaji makini wa vitabu Christian Bwaya na mimi.



























Na kama inavyotokea tena na tena, kuna wateja ambao, baada ya kununua kitabu au vitabu, hupenda kupiga picha na mwandishi. Bahati mbaya ni kuwa huyu dada hapa kushoto hakuniachia anwani. Ningependa kumpelekea picha hii, kwa kumbukumbu.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...