Thursday, August 28, 2014

Marekani Hata Wazee Wananunua na Wanasoma Vitabu

Kama nilivyoandika katika blogu hii, nilishiriki tamasha la tamaduni za kimataifa lililofanyika mjini Faribault tarehe 23 mwezi huu. Kati ya mambo niliyoelezea ni shughuli niliyofanya ya kusaini vitabu, na kati ya picha nilizoweka, ni hiyo inayoonekana hapa kushoto, ambayo inamwonesha mama mmoja mzee niliyekuwa namsainia nakala ya Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, aliyokuwa ameinunua hapo hapo.

Sijui kama jambo hili linaweza kutokea mahali kama Tanzania. Kule watu wanachojua ni kuwa vitabu ni kitu kinachowahusu wanafunzi, labda kiwe kitabu cha hadithi, hasa hadithi za kusisimua na za mapenzi. Vitabu vya maarifa ya aina yoyote vinachukuliwa kuwa ni kwa ajili ya wanafunzi, na hao wanafunzi wanatafuta vitabu vinavyotumika mashuleni.

Hapa Marekani, hali ni tofauti. Hata wazee hununua na husoma vitabu. Ukienda kwenye maduka ya vitabu, utawaona. Kwenye matamasha ya vitabu, utawaona. Nenda maktabani, utawaona.

Nasema hayo kutokana na uzoefu wangu. Nisiende mbali. Hapo hapo Faribault nimeshiriki matamasha, mwaka hadi mwaka, na baadhi ya watu waliofika kwenye meza yangu na kununua vitabu ni wazee.

Tarehe 11 Oktoba, kutakuwepo na maonesho makubwa ya vitabu mjini St. Paul. Nimeshiriki maonesho hayo mwaka hadi mwaka, na nimewaona wazee, sambamba na watu wazima, vijana, na watoto. Nina uhakika kuwa hiyo tarehe 11 Oktoba, wazee watakuwepo.

Kuna mambo ya kujifunza hapo. Jambo moja ni lile alilotufundisha Mwalimu Nyerere, kuwa elimu haina mwisho. Lakini, kwa ujumbe kama huu, sitegemei kuwa jamii yetu ya Tanzania itashtuka au kubadilika hima. Hali ni mbaya sana. Itachukua miaka mingi kutokea mabadiliko, ambayo yatabidi yaendane na malezi tofauti kwa watoto wetu. Itabidi wazazi kujijengea utamaduni wa kununua vitabu, kuvisoma, na kuwasomea watoto wao wanapokuwa wadogo kabisa, na kuwakuza katika utamaduni huo, ili hata watakapokuwa wazee, wawe na hamasa ya kununua na kusoma vitabu.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...